KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 11, 2015

SIMBA YAKAIDI AGIZO LA TFF, YAMNG'ANG'ANIA MESSI


SIMBA SC imesema haitafanya kikao chochote na mchezaji wake, Ramadhani Yahya Singano ‘Messi’ kama ilivyoshauriwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Rais wa Simba SC, Evans Elieza Aveva amesema katika taarifa yake kwa vyombo vya Habari mchana huu kwamba, Kikao cha Kamati ya Utendaji ya klabu kilichofanyika jana, pamoja na mambo mengine kilijadili suala la Singano.
“Kwa kuwa mchezaji Ramadhan Yahya Singano alivunja makubaliano yaliyoamriwa katika kikao cha pamoja kati ya klabu ya Simba, mchezaji mwenyewe, SPUTANZA na Sekretarieti ya TFF, kutozungumzia yaliyojadiliwa na kupendekezwa kwenye kikao, kwa kuyazungumza kwenye vyombo vya habari kwa kusema yeye ni mchezaji huru, klabu ya Simba imeamua kutokufanya mazungumzo na mchezaji huyo kwa sasa, kwa kuwa bado ina mkataba naye ambao utaisha Julai 1 mwaka 2016,”imesema taarifa ya Aveva
Hata hivyo, Aveva amesema klabu itakuwa tayari kufanya naye mazungumzo muda muafaka utakapofika, kwa mujibu wa kanuni na taratibu za mikataba.
“Ni matarajio yetu mchezaji Singano ataheshimu maamuzi hayo na mkataba ambao pia upo TFF na kwenye mtandao TMS,”amesema.
Juzi, TFF iliitaka Simba SC kuketi na Singano ‘Messi’ kujadili namna ya kuingia Mkataba mpya, baada ya pande zote kuafiki Mkataba wa sasa una hitilafu.
Katika kikao hicho kilichofanyika, makao makuu ya TFF, Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam, Simba SC iliwakilishwa na Mjumbe wa Kamati yake ya Utendaji, Collins Frisch wakati Messi aliandamana na Mussa Kisoky wa Chama cha Wanasoka Tanzania  (SPUTANZA). 
TFF ilisema kaatika kikao hicho pande zote zilitambua utata ulio ndani ya mikataba iliyokuwepo ambayo kimsingi iliingiwa kabla ya uongozi wa sasa wa Simba SC.
TFF ikasema, pande hizo mbili zimekubaliana kuanza mazungumzo ya makubaliano mapya kwa ajili ya Mkataba utakaoanza msimu mpya wa 2015/2016
Messi aliyeibukia timu ya vijana ya Simba SC miaka minne iliyopita, hivi karibuni ameibua shutuma dhidi ya klabu yake hiyo kwamba imeghushi Mkataba wake.
Messi anadai Mkataba wake halali ulikuwa unamalizika mwaka huu, na si huu wa sasa ambao inaelezwa utamalizika mwakani.
Lakini baada ya kikao pamoja na taarifa rasmi ya TFF, Messi alizungumza na vyombo vya Habari akisema yeye ni mchezaji huru ana hiari ya kuzungumza na Simba au klabu yoyote kwa ajili ya Mkataba mpya.
Na Kisoky wa SPUTANZA akasema wanalihamishia suala hilo kwenye Kamati ya Sheria Maadili na Hadhi za Wachezaji kutafuta haki zaidi.
IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BIN ZUBEIRY

No comments:

Post a Comment