KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 16, 2011

ZFA yajitetea hati za wachezaji kuzuiwa

CHAMA cha Soka Zanzibar (ZFA) kimesema, kuzuiwa kwa hati za kusafiria za wachezaji wa Zanzibar Heroes walioko katika timu ya Taifa Stars, kulilenga kuepusha usumbufu wakati wa mechi ya kufuzu fainali za Kombe la Dunia dhidi ya Chad.
Msemaji wa ZFA, Hafidh Ali Tahir alisema hayo juzi mjini hapa alipokuwa akijibu maswali kutoka kwa waandishi wa habari katika hoteli ya Bwawani.
Tahir alisema katika mashindano ya kimataifa, hati za kusafiria za wachezaji ndizo zinazotambuliwa kama leseni, hivyo ni lazima ziwasilishwe wakati wa mechi maalumu kama za Kombe la Dunia.
Awali, mmoja wa viongozi wa ZFA, aliyefuatana na timu ya Zanzibar nchini Misri, alikaririwa akililaumu Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kitendo cha kuzizuia hati hizo huku viza za safari zikiwa hazijapatikana.
Akitoa ufafanuzi, Tahir alisema kwa kutambua umuhimu wa Taifa Stars, ZFA haikuona sababu ya kuwang’ang’ania wanandinga wake wa Zanzibar kwenda Misri mapema.
Alisema wachezaji hao waliondoka nchini jana kwenda Misri baada ya kumalizika kwa mchezo wa marudiano kati ya Taifa Stars na Chad uliochezwa juzi mjini Dar es Salaam.
Tahir alisema ZFA imetuma vivuli vya hati zao za kusafiria kwa TFF, ambayo ilizigongesha viza na kwamba zilishashughulikiwa na ofisa wake mmoja, aliyepelekwa huko.
Alipoulizwa kuhusu Kocha Mkuu wa Zanzibar Heroes, Stewart Hall, ambaye alikwama kusafiri timu hiyo ilipoondoka nchini Novemba 10 mwaka huu, msemaji huyo alisema, anatarajiwa kuondoka wakati wowote.
Tahir alisema hati ya kusafiria ya kocha huyo ilikuwa na makosa sehemu ya kugonga viza hivyo anatarajiwa kutumia hati ya muda.
Zanzibar Heroes imeweka kambi Misri kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya Kombe la Chalenji, itakayoanza Novemba 25 mwaka huu katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment