KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 16, 2011

MAJUTO: Vichekesho vimenipa manufaa kimaisha


KWA watazamaji wa kipindi cha Comedy Show, kinachoonyeshwa kila siku za Alhamisi usiku, kupitia kituo cha televisheni cha Channel Ten, jina la King Majuto sio geni kwao.
Ni mmoja wa wasanii wakongwe wa maigizo na vichekesho nchini, lakini akiwa bado na kipaji cha hali ya juu katika kutunga vichekesho vinavyoonyeshwa kupitia katika kipindi hicho.
Umahiri wa Majuto katika fani hiyo haukuanza miaka ya hivi karibuni kama watu wengi wanavyofikiria. Safari ya Majuto ni ndefu, ikiwa ni pamoja na kukutana na vikwazo vingi vilivyomkatisha tamaa na kumfanya ajiweke pembeni ya fani hiyo.
Kama fani ya maigizo na vichekesho ingekuwa ikiwatajirisha wasanii wa fani hiyo, basi Majuto angekuwa bonge la milionea. Kabla ya kuanzishwa kwa vituo vya televisheni na wasanii kupata fursa ya kurekodi kanda za video, Alikuwa ametunga zaidi ya maigizo 1,000, lakini hakuna chochote cha maana alichoambulia.
Jina lake kamili ni Amri Athumani. Alipewa jina la King Majuto kutokana na umahiri wake katika fani hiyo na pia kumudu vyema kucheza nafasi alizokuwa akijipangia.
Majuto amepitia makundi mengi ya sanaa za maonyesho kama vile DDC Kibisa, Wazazi Dancing Troup na mengineyo kadhaa akiwa na Mzee Pembe, Mzee Uzegeni, Tomato na wengineo.
Akiwa ndani ya vikundi hivyo, alishirikiana navyo kuonyesha maigizo kwenye kumbi mbalimbali za burudani za mjini Dar es Salaam kama vile DDC Kariakoo, DDC Magomeni Kondoa, Super Mini, Temeke, Diluxe Bar na zinginezo.
Hata hivyo, kutokana na fani hiyo kutokuwa na manufaa makubwa kwa wasanii wake, Majuto aliamua kujiweka kando na kurejea nyumbani kwake Tanga kwa ajili ya kuangalia shughuli zingine za kufanya.
Kuanzishwa kwa vituo vingi vya televisheni nchini pamoja na wasanii wa fani hiyo kupata fursa ya kutengeneza kanda za video za vichekesho, ndiko kulikompa fursa Majuto ya kurejesha makali yake na pia kuanza kunufaika na fani hiyo.
Hadi sasa, Majuto ametengeneza kanda nyingi za vichekesho kupitia Kampuni ya Al-Riyami ya mjini Dar es Salaam. Baadhi ya kanda hizo ni pamoja na Inye, ambayo imepigwa marufuku kutokana na kukiuka maadili ya kitanzania.
Nyingine ni Ngoma kubwa, In the Court, Inye Plus na zinginezo, ambazo zimetokea kuwakuna mashabiki wengi wa fani hiyo kutokana na kujaa vichekesho vya kuvunja mbavu.
Akizungumza na Burudani mjini Tanga hivi karibuni, Majuto alisema anamshukuru Mungu kwamba fani hiyo kwa sasa imeyainua maisha yake, tofauti na miaka iliyopita.
Majuto alisema japokuwa sanaa ya maigizo na vichekesho imeanza kumlipa uzeeni, anamshukuru Mungu kwa kuweza kunufaika na kipaji chake kuliko angekufa masikini.
“Pamoja na misukosuoko yote niliyoipata kupitia sanaa ya vichekesho, namshukuru Mungu kwamba nimefanikiwa kujenga nyumba ya kuishi na pia ninamiliki magari mawili,”alisema.
Licha ya kukabiliwa na vikwazo vingi katika sanaa hiyo, Majuto alisema kamwe hakufikiria kuiacha kwa sababu ya umri wake kuwa mkubwa.
Majuto alisema anamshukuru Mungu kwamba pamoja na umri alionao, ana uwezo wa kuigiza nafasi zote, ikiwa ni pamoja na ya kijana wa kawaida, muhuni, mvuta unga na mzee.
Alisema anawashangaa watu wanaofikiria kwamba, atastaafu kazi hiyo hivi karibuni kutokana na uzee. Alisema watu hao wanasahau kwamba, hiyo ndiyo kazi aliyopangiwa na Mungu katika maisha yake.
“Nawashangaa, wanadhani nitaacha kuigiza leo au kesho, eti kwa sababu umri wangu mkubwa, mbona kwenye mashindano mbalimbali nawafunika,"alisema Majuto.
Msanii huyo mkongwe alisema, ameshiriki kwenye mashindano mengi ya vichekesho na kuibuka na ushindi, lakini kamwe hajawahi kupewa zawadi zilizoahidiwa na waandaaji.
Kutokana na kutapeliiwa huko, Majuto amesema kamwe hatarajii kushiriki tena katika mashindano ya aina hiyo kwa sababu amebaini kuwa, waandaaji huyaandaa kwa lengo la kuwatumia kujinufaisha.
King Majuto anao watoto na wajukuu kadhaa, lakini hapendi kutaja idadi yao. Alisema hayo ni mambo yanayohusu maisha yake binafsi.

No comments:

Post a Comment