KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 23, 2011

Suma Lee azusha kasheshe



WIMBO mpya wa ‘Hakunaga’ uliopigwa na msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Ismail Sadiki umezua kasheshe baada ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kutishia kuufungia.
Wimbo huo uliotokea kupendwa na mashabiki wengi nchini, umekuwa ukishika chati za juu kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni kutokana na ujumbe na mpangilio wa ala.
Hata hivyo, lugha iliyotumiwa na Ismail, maarufu zaidi kwa jina la Suma Lee, imeonekana kuikera BASATA kwa vile Kiswahili kilichotumika sio fasaha.
Katibu Mkuu wa BASATA, Gonche Materego alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, kwa sasa bado hawajafikia uamuzi wa kuufungia wimbo huo, lakini bado wanaujadili.
“Tunachokifanya kwa sasa ni majadiliano makubwa kuhusu nyimbo nyingi za wasanii wa Tanzania, ambazo tungo zake zinaharibu lugha ya Kiswahili,”alisema.
Akitoa mfano, Materego alisema wimbo wa Hakunaga ndio uliozua majadiliano makali kwa sababu Kiswahili kilichotumiwa na Suma Lee sio sahihi.
“Kusema ukweli, wimbo huu ulizungumzwa sana na hata watu wengine wa kawaida, ambao hawafanyikazi na BASATA walisema kwamba, unapotosha Kiswahili,”alisema Materego.
“Na kwa vile wasanii ni walimu wakuu wa Kiswahili, ni rahisi sana kwa watu wa kawaida kutumia lugha za wasanii wakidhani kuwa ni sahihi wakati sio kweli,”aliongeza.
“Wenzetu wa Baraza la Kiswahili wameona kuna haja ya kukaa na kujadiliana kuhusiana na tatizo la Kiswahili kuharibiwa kwenye nyimbo za wasanii. Tutakutana na wasanii tusikie wanachokisema na wananchi pia wasikie ili tupate michango mizuri zaidi,”alisisitiza.
Alipoulizwa kuhusu msimamo huo wa BASATA, Suma Lee alisema hawezi kuzungumza chochote kwa sasa kwa sababu baraza hilo halijawahi kumwita na kumueleza lolote.
“Nimekuwa nikisikia taarifa hizi kupitia kwenye vyombo vya habari, hivyo siwezi kuzungumza lolote hadi BASATA itakapowasiliana na mimi,”alisema.
Hata hivyo, Suma Lee alieleza kuridhishwa kwake na mapokezi ya mashabiki katika wimbo wake huo, ambao utakuwemo kwenye albamu yake mpya, aliyoipa jina la ‘Hesabu za Mapenzi’. Albamu hiyo itakuwa na nyimbo 15.

No comments:

Post a Comment