KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, November 17, 2011

Kili Stars kukata utepe na Amavubi

MABINGWA watetezi, timu ya soka ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars imepangwa kufungua dimba la michuano ya Kombe la Chalenji kwa kumenyana na Rwanda, Amavubi.
Ratiba ya michuano hiyo, iliyotolewa jana na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) inaonyesha kuwa, mechi hiyo itapigwa kuanzia saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
CECAFA imesema, mechi za michuano hiyo sasa zitachezwa kwenye uwanja mmoja pekee wa Taifa, baada ya mkoa wa Mwanza kushindwa kutimiza masharti ya kuwa mwenyeji wa mechi zingine.
Kwa mujibu wa CECAFA, kwa siku zitachezwa mechi mbili, isipokuwa siku ya uzinduzi, ambapo itachezwa mechi moja pekee.
Ratiba inaonyesha kuwa, Novemba 25 mwaka huu, Burundi itamenyana na Somalia kuanzia saa 8 mchana) kabla ya Uganda kukipiga na Zanzibar kuanzia saa 10 jioni.
Wakati huo huo, CECAFA imesema Eritrea imejitoa kwenye michuano ya mwaka huu, kufuatia wachezaji wake wengi kutoka wanapokwenda kucheza ugenini.
Mwaka jana, wachezaji zaidi ya 11 wa timu ya Red Sea ya Eritrea walitoroka kwenye kambi ya timu hiyo siku chache kabla ya kuondoka nchini na kuomba hifadhi ya ukimbizi.
Hata hivyo, maombi ya wachezaji hao yalikataliwa kutokana na kutokidhi vigezo vinavyotakuwa na kurejeshwa kwao.
Kufuatia kujitoa kwa Eritrea, CECAFA imesema, nafasi yake sasa imechukuliwa na Namibia, ambayo itacheza kama timu mwalikwa pamoja na Malawi.
Namibia sasa ipo kwenye kundi A pamoja na mabingwa watetezi, Kilimanjaro Stars, Rwanda na Djibouti.
Michuano ya mwaka huu imedhaminiwa tena na Kampuni ya Bia ya Serengeti.
Katika hatua nyingine, Kocha Mkuu wa Kilimanjaro Stars, Charles Boniface Mkwasa leo anatarajiwa kutangaza kikosi cha timu hiyo kitakachoshiriki kwenye michuano ya Kombe la Chalenji.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema jana kuwa, Mkwasa atatangaza kikosi hicho katika mkutano wake na waandishi wa habari utakaofanyika saa sita mchana kwenye ofisi za shirikisho hilo.

1 comment: