KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 30, 2011

Chondechonde mwacheni Vengu-Seki


UONGOZI wa kundi la Orijino Komedi umevitaka vyombo vya habari nchini kuacha kumfuatilia msanii wake, Joseph Shamba ‘Vengu’ aliyelazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam.
Mbali na kuviasa vyombo vya habari, kundi hilo pia limewaomba mashabiki wake kuacha kumsumbua msanii hiyo kwa kulazimisha kuingia kwenye chumba alimolazwa hospitalini hapo.
Kiongozi wa kundi hilo, Sekione David alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, madaktari wanaomtibu Vengu wameshauri asibughudhiwe na watu.
“Madaktari na familia yake hawataki jambo hili liwe wazi kwa kila mtu, ugonjwa ni siri ya mgonjwa na madaktari kwa manufaa ya hospitali,”alisema Sekione, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Seki.
Kiongozi huyo wa Orijino Komedi alisema, binafsi haruhusiwi kutoa taarifa zinazomhusu msanii huyo kutokana na kuzuiwa kufanya hivyo na madaktari.
“Hizi ni taratibu walizoweka madaktari na ndugu zake, hatuwezi kwenda kinyume ya hapo,”alisisitiza Seki.
Vengu amelazwa Muhimbili kwa zaidi ya miezi miwili huku ugonjwa wake ukifanywa kuwa siri kubwa. Kuna habari kuwa, msanii huyo anasumbuliwa na kichwa.
Kufuatia kulazwa hospitalini hapo kwa muda mrefu, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikitoa taarifa tofauti kuhusu ugonjwa unaomsumbua msanii huyo.
Katika kipindi cha Orijino Komedi wiki iliyopita, msanii maarufu kwa jina la Masanja alisikika akisema kwa masikitiko kwamba, hali ya Vengu bado haijatengemaa.
“Jamani jamani, Vengu anaumwa. Masikini jembe langu, linaumwa,”alisema.
Masanja alisema hayo, kufuatia mashabiki wengi wa kipindi hicho kuwapigia simu wakitaka kujua maendeleo ya afya ya msanii huyo.
Kutokana na kuthamini mchango wa msanii mwenzao, Masanja alisema wataendelea kutumia kazi zake zilizopita ili kuwaliwaza mashabiki wao.

1 comment: