KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 23, 2011

NEYMAR: Nataka kuweka historia duniani





RIO DE JANEIRO, Brazil
WAKATI alipokuwa akikatiza mitaani miaka kadhaa iliyopita,Neymar da Silva Santos Junior hakuwa mtu maarufu. Alionekana mtu wa kawaida, sawa na watoto wengine wa Kibrazil, nchi iliyobarikiwa kuwa na vijana wengi wenye vipaji vya kusakata kabumbu.
Lakini hali imekuwa tofauti miaka ya hivi karibuni, ambapo umaarufu wake kisoka umemfanya awe akizingirwa na kundi la watu kila anapopita mitaani, huku wengine wakimtaka atie saini vitabu vyao vya kumbukumbu na wengine kumuomba wapige naye picha ya pamoja.
Neymar (19) ni mchezaji mwenye kipaji cha aina yake kisoka, akiwa anafananishwa na Ronaldinho Gaucho, Robinho au Lionel Messi. Na kuna watu wanaobashiria kwamba, anaweza kuwa sawa na Pele kiuchezaji.
Chipukizi huyo amekuwa tegemeo kubwa la klabu yake ya Santos ya Brazil na pia timu ya taifa ya nchi hiyo. Uwezo wake kisoka ulizivutia klabu kadhaa kubwa za Ulaya kama vile Real Madrid ya Hispania na Chelsea ya England, lakini zote ziligonga mwamba kumsajili.
Kila anapokwenda, Neymar hufuatwa na kundi kubwa la wapiga picha. Iwe ni katika mji wa Santos, London na New York, hali huwa hivyo hivyo. Amekuwa shujaa kwa vijana wengi wa kiume na mvulana mwenye mvuto kwa wasichana, hasa kutokana na staili ya utengenezaji wa nywele zake.
Neymar anakumbuka miaka si mingi iliyopita, alipokuwa akitoka nyumbani kwenda kununua ice-cream, hakuwa akismamishwa na watu njiani. Lakini gharama za umaarufu zimeshayabadili maisha yake na kumfanya aonekane lulu machoni mwa mashabiki wa soka.
“Haya ndiyo maisha niliyoyachagua,”alisema Neymar alipohojiwa na mtandao wa FIFA hivi karibuni. “Sikuchagua niishi hivi, nilimuomba Mungu. Nilichokitaka ni kucheza soka na kuwa mwenye mafanikio na nipate umaarufu. Nimepata kila nilichokuwa nikikihitaji na nitakuwa mpumbavu kulalamikia chochote kwa sasa.”
“Siwezi kukaa mahali na kufikiria kwamba siwezi kutoka nje kwenda kununua ice-cream,”aliongeza. “Ninakwenda popote na kuishi maisha yangu ya kawaida, nasaini vitabu vya kumbukumbu vya mashabiki, napiga nao picha na hata kutolewa lugha za dhihaka kwa sababu hii ni sehemu ya maisha ya soka. Mwisho wa siku mimi ni binadamu wa kawaida.”
Licha ya kujifunza kuishi maisha hayo na ya matumaini tangu akiwa mdogo na pia kutawala kwenye vyombo vya habari mara kwa mara, ukweli unabaki palepale kwamba, Neymar bado ni kijana, aliyejawa na aibu na asiyeelewa maana ya mafanikio aliyoyafikia hivi sasa.
“Kusema ukweli, haya ni mambo mapya kwangu, kuwaona watu wote hawa wakishangilia kwa kutaja jina langu na kunitaka niseme ‘Hi’ ama kuwatolea tabasamu. Lakini tayari nimeshaanza kuzoea hali hii. Binafsi nilikuwa nikiwashabikia baadhi ya wachezaji nyota na kujawa na hofu wanapokatiza mbele yangu. Na sasa imekuwa zamu yangu na ninapata heshima kubwa kwa mashabiki,”alisema nyota huyo.
Neymar, ambaye mashabiki wa soka nchini Brazil wamempachika jina la Neymarzetes, amekuwa na wakati mgumu kwa mabeki wa timu pinzani, ambao wamekuwa wakifanya kila wanaloweza kumzuia uwanjani.
“Unamtoka mchezaji mmoja, hatua inayofuata unaangushwa chini. Unamtoka mchezaji mwingine, kinachofuatia unaangushwa tena chini. Na kigumu zaidi ni kwamba, kuna ukabaji wa mtu kwa mtu,”alisema.
Kupatiwa kwake nafasi ya kuichezea timu ya taifa ya Brazil kumemwezesha nyota huyo kujifunza mengi kuhusu mabeki kutoka sehemu mbalimbali duniani, elimu ambayo anakiri imemsaidia katika mambo mengi.
“Kucheza dhidi ya wachezaji waliopo Ulaya, kumenisaidia mambo mengi. Ukabaji wao ni mgumu, lakini ni tofauti,”alisema nyota huyo.
Neymar amemwelezea mshambuliaji wa kimataifa wa Argentina, Lionel Messi kuwa tayari ameshaweka historia na kupata mafanikio makubwa kisoka. Alisema binafsi ndio kwanza anaanza kuonyesha cheche zake na anakabiliwa na changamoto nyingi ili aweze kufikia mafanikio hayo.
Neymar, ambaye hivi karibuni alitia saini mkataba mpya wa kuichezea Santos hadi mwaka 2014, alisema anaamini michuano ya kuwania klabu bingwa ya dunia itakayofanyika mwezi ujao Japan, itamwongezea ujuzi zaidi kisoka.
Chipukizi huyu anavutiwa zaidi na klabu ya Barcelona ya Hispania. Anaielezea timu hii kuwa, inastahili tuzo zote ilizonyakua kwa vile soka yake ni ya kiwango cha juu na yenye mvuto wa aina yake.
Iwapo timu ya Santos na Barcelona zitakutana katika michuano hiyo, itakuwa ni burudani babu kubwa kwa mashabiki kwa vile itakuwa ni nafasi nzuri kwa Neymar na Messi kuonyesha uwezo wao.
Neymar na Messi ni miongoni mwa wachezaji 23 walioteuliwa kuwania tuzo ya mfungaji bora wa FIFA wa mwaka 2011.
“Siku zote nimekuwa nikisema kwamba, bado nina mambo mengi ya kujifunza. Messi ni mchezaji, ambaye tayari ameshaweka historia na atapata mafanikio mengi zaidi. Mimi ndio kwanza naanza na ninapaswa kufanya mengi ili niweze kufikia mafanikio yake,”alisema.
Neymar amesema amepania kujiweka fiti zaidi ili abaki kwenye kiwango cha juu na pia kuiwezesha nchi yake kufanya vizuri kimataifa.
“Nataka kuweka historia na Brazil mwaka 2014 na kuliweka jina langu kwenye kumbukumbu ya soka duniani,”alisema.
Neymar alijiunga na Santos mwaka 2003 na kuanza kupata namba kwenye kikosi cha kwanza miaka sita baadaye, akiwa na umri wa miaka 17.
Aprili 15, 2010 aliifungia Santos mabao sita katika ushindi wa mabao 8-1 dhidi ya Guarani katika mechi ya raundi ya pili ya michuano ya Kombe la Brazil. Aliifungia Santos mabao 16 katika mechi 19 za michuano hiyo na kuiwezesha kutwaa ubingwa.
Juni 2010, Santos ilikataa maombi ya kumuuza mshambuliaji huyo kwa klabu za West Ham, Manchester United, Chelsea, AC Milan, Inter Milan, Real Madrid na Juventus.
WASIFU

JINA: Neymar da Silva Santos Junior

ALIZALIWA: Februari 5, 1992

UMRI: Miaka 19

ALIKOZALIWA: Mogi das Cruzes, Sao Paulo, Brazil

UREFU: 1.74 m (futi 5 na inchi 9)

NAFASI: Mshambuliaji

KLABU: Santos

NAMBA YA JEZI: 11

TIMU ya TAIFA:

2009: Brazil U-17

2010: Brazil

2011: Brazil U-20

No comments:

Post a Comment