KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 30, 2011

Twenty Percent, Man Walter sasa ni chui na paka




HUWEZI kuamini. Pia unaweza kuita ni mchezo wa kuigiza ama filamu ya mauzauza. Ni kwa sababu kilichotokea, hakuna aliyekitarajia.
Ni kwamba mshindi wa tuzo tano za muziki za Kilimanjaro mwaka jana, Abbas Kinzasa 'Twenty Percent' na prodyuza wake, John Shariza, maarufu kwa jina la Man Walter hivi sasa hawaelewani. Ni sawa na chui na paka.
Unajua kisa ni nini?
Hakuna kingine zaidi ya mkwanja. Ndivyo inavyokuwa miaka yote utakaposikia msanii na prodyuza wake wamekorofishana. Sababu kubwa huwa ni kudhulumiana malipo.
Hivyo ndivyo ilivyotokea kwa Twenty Percent na Man Walter, ambao hivi karibuni walitoleana lugha kali, kila mmoja akimshutumu mwenzake kwamba ndiye chanzo cha kutokuelewana kwao.
Akihojiwa na kituo cha Radio One Stereo mwishoni mwa wiki iliyopita, Man Walter, ambaye ndiye mmiliki wa studio ya Combination Sound alisema, chanzo cha kutokuelewana huko ni ugomvi uliotokea kati yao kabla ya kuanza kwa onyesho lililofanyika mjini Morogoro.
Prodyuza huyo alisema, aliamua kuandaa onyesho hilo kwa ajili ya kumpongeza Twenty Percent na pia kuwashukuru mashabiki kwa kumpigia kura nyingi.
Alisema kabla ya kuanza kwa onyesho hilo, alifuatwa na Twenty Percent na kumtaka ampe malipo yake mapema. Alisema alipompa kwa mara ya kwanza, msanii huyo alikataa kupokea kiasi cha pesa alicholipwa kwa madai kuwa ni kidogo.
“Akaomba akabidhiwe malipo hayo mbele ya polisi, pia akakataa kupokea. Baadaye nikwamwita Afande Sele na kumkabidhi malipo hayo mbele yake, ndipo akakubali kupokea,”alisema Man Walter bila ya kufafanua kiwango hicho cha pesa.
Kwa mujibu wa Man Walter, licha ya kupokea malipo hayo, msanii huyo alitoa lugha kali kwake, akimshutumu na kumwita tapeli, aliyetumia kipaji chake kujinufaisha kimaisha.
Aliongeza kuwa, msanii huyo pia aliapa mbele za watu kwamba, hatorekodi tena nyimbo zake kwenye studio yake na wala asitarajie kufanyanaye kazi zingine.
“Kwa kweli maneno aliyoyatamka kwangu sikuyatarajia kabisa. Hata mashabiki waliofika ukumbini kushuhudia onyesho hilo walilalamika sana na kutoka nje,”alisema Man Walter.
Prodyuza huyo alisema, kilichomsikitisha zaidi ni kumsikia msanii huyo akiapa kwamba, atamfanyia kitu mbaya. Alisema alichokifanya si haki hata kidogo.
“Mimi ndiye niliyemtoa na kumpatia umaarufu kimuziki. Kutokana na makubaliano tuliyokuwa nayo, hakupaswa kurekodi nyimbo mpya kwa prodyuza mwingine. Alipaswa kunipa angalau nyimbo mbili,”alilalamika.
Kwa upande wake, Twenty Percent alisema si kweli kwamba haelewani na Man Walter, isipokuwa amerekodi nyimbo zake mpya kwenye studio zingine kwa lengo la kuzipa ladha tofauti.
“Sina ugomvi wowote na Man Walter, isipokuwa watu walipotuona tukibadilishana maneno makali, wakachukulia kwamba ugomvi wetu ni mkubwa,”alisema.
Msanii huyo alisema yeye na Man Walter ni marafiki wakubwa, iwe kikazi ama wanapokuwa mtaani wanapoishi na amekuwa akimchukulia kama kaka yake.
Alisema sababu kubwa iliyomfanya aamue kurekodi nyimbo zake mpya kwenye studio zingine ni kutokana na Man Walter kutingwa na kazi nyingi.
“Haya ni mabadiliko ya kawaida kimuziki. Nilichokifanya ni kubadili ladha ya muziki wangu ili nitoke kivingine badala ya vile nilivyozoeleka,”alisema.
“Man Walter ni kama kaka yangu. Tunapokuwa mtaani, yeye ndiye anayenipa mawazo mbalimbali kuhusu maisha, hatuna ugomvi, tupo pamoja,”alisisitiza.

No comments:

Post a Comment