KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, November 17, 2011

Malindi yashushwa rasmi daraja

TIMU ya soka ya Malindi imeshushwa kutoka daraja la kwanza hadi la pili katika Wilaya ya Mjini, kufuatia kushindwa kutekeleza masharti ya mahakama.
Malindi ilikuwa imefungua kesi kupinga kanuni iliyotumika kuiteremsha daraja, kufuatia matokeo ya ligi ndogo iliyochezwa kwa mkondo mmoja mwanzoni mwa mwaka huu.
Katika kusikiliza kesi hiyo, mahakama iliitaka Malindi kuifutaili irejeshwe daraja la kwanza, lakini kwa masharti ya kukamilisha taratibu zote za kuwemo katika ligi.
Msemaji wa Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA), Hafidh Ali Tahir alisema, Malindi imeshindwa kutimiza masharti iliyopewa, ambapo ilitakiwa kufanya hivyo ndani ya wiki moja.
Baadhi ya masharti iliyopewa ni kufanya usajili wa wachezaji, kulipa ada ya mashindano na pia kujisajili kwa mrajisi wa vyama vya michezo.
Awali, Miembeni United ilikubali kuuza nafasi yake ili kuishawishi Malindi iondoe kesi iliyokuwa imeifungua mahakamani.
Tahir alisema baada ya Malindi kuwasilisha shauri lake katika Mahakama ya mkoa ya Vuga, ambayo ilitoa amri ya kusitisha ligi kuu, uongozi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, ulikutana na uongozi wa Malindi na ZFA, kutafuta namna ya kuimaliza kadhia hiyo nje ya mahakama.
Kufuatia kikao hicho, ambacho pia kilimjumuisha Mkurugenzi wa Miembeni, Amani Ibrahim Makungu, kiongozi huyo alikubali kuipa Malindi nafasi ya kucheza ligi kuu na timu yake icheze daraja la kwanza, kwa lengo la kufuta aibu ya kuzipeleka kesi za soka mahakamani.
“Baada ya yote hayo, ikiwa ni pamoja na kupewa nafasi ya upendeleo, Malindi imeshindwa kutimiza masharti iliyopewa, kwa hiyo ZFA inatoa tamko kuwa, timu hiyo imeteremshwa daraja la pili wilaya ya Mjini”, alifafanua.
Katika hatua nyingine, Tahir amesema kwa sasa, ZFA inajipanga kuanza ligi kuu na kwamba, taratibu zote zitapangwa katika mkutano wa kamati ya utendaji unaotarajiwa kufanyika leo kisiwani Pemba.
Kuhusu udhamini, alisema kumejitokeza taasisi iliyojitolea kutoa sare za waamuzi, kuwasafirisha pamoja na mahitaji yao mengine. Hata hivyo, alisema ni mapema kuitaja kwa vile bado inaendelea kujipanga.
Hata hivyo, alisema licha ya kuharibika kwa meli ya Sea gull na kuzuiwa, bado chama chake hakijapokea barua ya kujiondoa kwa kampuni hiyo katika udhamini wake wa ligi kuu, na kwamba makubaliano yao yapo pale pale.

No comments:

Post a Comment