KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 23, 2011

Kambi ya Misri yaipa jeuri Zanzibar Heroes


TIMU ya soka ya Zanzibar, Zanzibar Heroes imerejea nchini juzi kutoka Misri, ilikokwenda kuweka kambi kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya Kombe la Chalenji.
Ofisa Habari wa Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA), Munir Zakaria alisema mjini hapa juzi kuwa, timu hiyo iliweka kambi Misri kwa wiki mbili.
Mbali ya kuweka kambi, Munir alisema timu hiyo ilicheza mechi tatu za kirafiki dhidi ya timu za Misri, ambapo ilishinda mechi moja na kufungwa mechi tatu.
Munir alisema timu hiyo ilipata ushindi wake wa pekee dhidi ya timu ya taifa ya vijana wa chini ya miaka 17 ya Misri. Katika mechi hiyo, Zanzibar Heroes ilishinda mabao 3-2.
Zanzibar Heroes ilikwenda Misri ikiwa chini ya Kocha Hemed Morocco, ambaye ndiye atakayeiongoza katika michuano ya Kombe la Chalenji, inayotarajiwa kuanza kesho.
Akizungumzia kambi hiyo, Munir alisema ilikwenda vizuri na kwamba mechi nne za kirafiki walizocheza, zimewaweka wachezaji katika hali nzuri kwa ajili ya Kombe la Chalenji.
Alisema kikosi hicho kwa sasa kipo fiti kwa ajili ya michuano hiyo na kuongeza kuwa, wachezaji wana ari kubwa ya kuibuka na ushindi.
Wakati huo huo, Munir amesema hatma ya Kocha John Stewart kutoka Uingereza kwa sasa ipo mikononi mwa ZFA.
Stewart, ambaye pia ni Kocha Mkuu wa Azam FC, alishindwa kujiunga na Zanzibar Heroes ilipokuwa Misri kwa madai kuwa, hati yake ya kusafiria ilikuwa imejaa.
Hata hivyo, utetezi wake huo umepingwa na baadhi ya viongozi wa chama hicho kwa madai kuwa, alifahamu mapema kuhusu safari hiyo.
Licha ya kuifundisha Azam, inayoshiriki michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara, Stewart pia ana mkataba wa kuifundisha Zanzibar Heroes wakati wa michuano mbalimbali.

No comments:

Post a Comment