KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 9, 2011

Taifa Stars kukipiga na Chad kesho

TIMU ya soka ya Taifa, Taifa Stars inashuka dimbani kesho mjini N’Djamena kumenyana na timu ya Taifa ya Chad katika mechi ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014.
Taifa Stars iliondoka nchini jana saa tisa alasiri kwa ndege ya Shirika la Kenya Airways, ikiwa na msafara wa watu 40, wakiongozwa na mjumbe wa kamati ya utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Eliud Mvella.
Msafara wa timu hiyo ulitarajiwa kuwasili N’Djamena saa 1.15 usiku kwa saa za Chad, sawa na saa 3.15 usiku kwa saa za Tanzania.
Katika msafara huo, wamo wachezaji 21 waliokuwepo kambini kwa ajili ya kujiandaa na pambano hilo, sita kutoka benchi la ufundi wakiongozwa na Kocha Jan Poulsen na wajumbe wawili kutoka Baraza la Michezo la Taifa (BMT).
Taifa Stars iliagwa juzi saa moja usiku kwa kukabidhiwa bendera ya Taifa na Mwenyekiti wa BMT, Dioniz Malinzi. Hafla hiyo ilifanyika kwenye hoteli ya New Africa, Dar es Salaam.
Katika hafla hiyo, Malinzi aliwataka wachezaji hao kucheza kufa na kupona ili waweze kushinda mchezo huo na kuahidi kuwalipia gharama za matibabu wale watakaoumia.
Akiwasilisha salamu zake kwa wachezaji hao kupitia njia ya video, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema ushindi ni muhimu ili kusherehekea vyema miaka 50 na uhuru.
Pinda aliwazawadia wachezaji hao sh. milioni 10 kwa aili ya kuwaongezea ari ili waweze kushinda pambano hilo.
Timu hiyo inaundwa na makipa Juma Kaseja (Simba) na Mwadini Ally (Azam). Mabeki ni Aggrey Morris (Azam), Juma Nyoso (Simba), Idrissa Rajab (Sofapaka, Kenya), Erasto Nyoni (Azam), Godfrey Taita (Yanga) na Juma Jabu (Simba). Viungo ni Henry Joseph (Kongsvinger IL, Norway), Nurdin Bakari (Yanga), Shabani Nditi (Mtibwa Sugar), Abdi Kassim (DT Long An, Vietnam), Ramadhan Chombo (Azam) na Shomari Kapombe (Simba). Washambuliaji ni Nizar Khalfan (Vancouver Whitecaps, Canada), Mrisho Ngassa (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Athuman Machupa (Vasalund IF, Sweden), Hussein Javu (Mtibwa Sugar) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC).
Taifa Stars inatarajiwa kurejea nchini Novemba 13 saa 7.25 mchana kwa ndege ya Shirika la Ethiopia na kwenda moja kwa moja kambini kujiandaa kwa mchezo wa marudiano utakaopigwa Novemba 15 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment