KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 30, 2011

JB: Tumeweza, tunasonga mbele



MSANII mkongwe wa fani ya filamu nchini, Jacob Steven amesema, maendeleo ya fani hiyo kwa sasa ni makubwa ikilinganishwa na miaka iliyopita.
Akihojiwa na kituo cha redio cha Clouds FM cha mjini Dar es Salaam wiki hii, Jacob alisema wakati fani hiyo ilipoanza, wasanii walikuwa wachache na walishindwa kunufaika nayo.
Msanii huyo, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la JB alisema, kadri miaka inavyosonga mbele, wasanii wamekuwa wakiongezeka na pia yamejitokeza mabadiliko makubwa katika utayarishaji wa filamu.
JB alisema hali hiyo imekuwa ikiwafanya wasanii nao waanze kunufaika na vipaji vyao kutokana na soko la filamu kuwa kubwa.
“Maendeleo wakati ule yalikuwa madogo kwa sababu ilikuwa ndio kwanza tunaanza. Wasanii wengi wa wakati ule hivi sasa hawapo,”alisema.
Aliwataja wasanii waanzilishi wa fani hiyo, iliyoanza kujipatia umaarufu miaka ya 1900 na ambao kwa sasa wamejiweka kando kuwa ni Bishanga, Aisha, Waridi na Mama Bishanga.
“Nina hakika katika miaka michache ijayo, ushindani katika fani ya filamu utakuwa mkubwa zaidi kwa sababu wasanii watazidi kuongezeka,”alisema.
Alisema katika miaka ya hivi karibuni, kumejitokeza wasanii wengi wa mitindo ya mavazi, urembo na wasomi wa kada mbalimbali, ambao wamezidi kuzinadhifisha filamu za kibongo na kuzifanya ziwe na mwonekano wa kimataifa.
“Kwa sasa tunao wasomi kutoka vyuo vikuu mbalimbali pamoja na Taasisi ya sanaa Bagamoyo. Kujitokeza kwao kwa wingi kunadhihirisha wazi kuwa, fani ya filamu hivi sasa inakubalika,”alisema.
Mbali na ongezeko la wasanii, JB alisema teknolojia inayotumika sasa katika kutengeneza filamu nayo ni ya juu zaidi na hivyo kuufanya ushindani uwe mkali.

1 comment: