KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 23, 2011

Simba yafanya kweli



WACHEZAJI Bukaba Bundara (kulia) wa Toto African na Abdalla Seseme wa Simba wakiwania mpira timu hizo zilipomenyana jana katika mechi ya nusu fainali ya michuano ya soka ya Kombe la Uhai kwa timu za vijana wa chini ya miaka 20 iliyochezwa kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam. Simba ilishinda mabao 4-1.


TIMU ya soka ya Simba jana ilifuzu kucheza fainali ya michuano ya Kombe la Uhai baada ya kuichapa Toto African mabao 4-1.
Katika mechi hiyo ya robo fainali, iliyochezwa kwenye uwanja wa Karume, Dar es Salaam, Simba ilikwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 3-0.
Kutokana na ushindi huo, Simba sasa itacheza fainali keshokutwa kwa kumenyana na mshindi wa mechi nyingine ya nusu fainali kati ya Azam na Serengeti Boys, iliyotarajiwa kuchezwa jana jioni.
Iliwachukua Simba dakika 25 kuhesabu bao la kwanza lililofungwa na mshambuliaji Edward Christopher baada ya kufanyika shambulizi kali kwenye goli la Toto.
Rama Singano aliifungia Simba bao la pili dakika ya 40 kabla ya Abdalla Seseme kuongeza la tatu dakika mbili zilizofuata.
Simba ilitawala zaidi kipindi cha kwanza cha mchezo huo, huku wachezaji wake wakipeana gonga safi na kuliweka lango la Toto kwenye msukosuko mkubwa.
Toto ilizinduka kipindi cha pili na kufanikiwa kupata bao la kujifariji dakika ya 51 lililofungwa na Iddi Mobi.
Matumaini ya Toto kusawazisha yalizimwa na Haroun Athumani, aliyeiongezea Simba bao la nne dakika ya 78 na kuamsha shamrashamra kutoka kwa mashabiki wa timu hiyo.
Bingwa wa michuano hiyo atazawadiwa kitita cha sh. milioni 1.5 wakati mshindi wa pili atapata sh. milioni moja na wa tatu sh. 500,000.
Mchezaji bora wa michuano hiyo atazawaduwa sh. 400,000, mfungaji bora sh. 300,000), kipa bora sh. 300,000 na timu yenye nidhamu sh. 300,000.

No comments:

Post a Comment