KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 30, 2011

Msondo, Sikinde uso kwa uso Krismas


BENDI kongwe za muziki wa dansi nchini, Msondo Ngoma na Mlimani Park Orchestra zimepanga kufanya onyesho la pamoja Desemba 25 mwaka huu kwenye viwanja vya klabu ya Sigara, Chang’ombe, Dar es Salaam.
Wakizungumza na Burudani kwa nyakati tofauti mjini Dar es Salaam juzi, viongozi wa bendi hizo walisema, onyesho hilo litadhaminiwa na Kampuni ya Konyagi.
Meneja wa Msondo Ngoma, Saidi Kibiriti alisema lengo la onyesho hilo ni kuimarisha umoja na ushirikiano kati ya wanamuziki wa bendi hizo kongwe nchini.
Kibiriti alisema bendi zote mbili zimekubaliana kuporomosha nyimbo mchanganyiko, zikiwemo za miaka 50 iliyopita na za sasa kwa lengo la kuwapa mashabiki burudani yenye vionjo na ladha tofauti.
“Hili si pambano la kutafuta nani mkali kati yetu, tunawaomba mashabiki waelewe hivyo, ni onyesho na kujenga na kuimarisha mshikamano kati ya wanamuziki wetu,”alisema.
Kwa upande wake, Katibu wa Mlimani Park, Hamisi Milambo alisema, maandalizi kwa ajili ya onyesho hilo yameshaanza na yanaendelea vizuri.
Milambo alisisitiza kuwa, lengo la bendi hizo si kupambana ili kumtafuta nani mkali kati yao, bali ni kuwapa mashabiki burudani kabambe ya muziki.
Hii itakuwa ni mara ya pili kwa Msondo na Mlimani Park kufanya onyesho la pamoja mwaka huu. Zilikutana kwa mara ya kwanza Juni mwaka huu katika onyesho lililofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
Onyesho hilo lilifanyika siku chache baada ya mwimbaji machachari nchini, Shabani Dede kuihama Mlimani Park na kujiunga na Msondo Ngoma.

1 comment: