KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 23, 2011

Ferej alalamikia ukiukwaji wa katiba ZFA


VURUGU zinazotokea mara kwa mara katika Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA) ni matokeo ya kukiukwa kwa katiba na kanuni za kuendesha mchezo huo.
Hayo yamesemwa na Rais wa ZFA, Ali Ferej Tamim wakati wa mkutano mkuu wa dharula wa chama hicho uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini hapa.
Mbali na kujadili masuala mbalimbali, mkutano huo uliitishwa kwa lengo la kufanya marekebisho ya katiba ya chama hicho.
Ferej alitoa kauli hiyo baada ya baadhi ya wajumbe wa kamati ya utendaji ya chama hicho kutoka Pemba, kulalamika kuwa, kimekuwa kikitoa maamuzi mengi bila ya kufuata katiba.
Wajumbe hao walilalamikia uamuzi wa ZFA wa kuirejesha Malindi katika ligi kuu bila kufuata taratibu ama kuishirikisha kamati ya utendaji ya chama hicho katika kutoa maamuzi.
Akijibu malalamiko hayo, Ferej alisema katika soka, hakuna kitu kinachoitwa makubaliano, kinachotakiwa ni kufuatwa kwa katiba na kanuni katika kutoa maamuzi.
Ferej alisema ni kweli kwamba yeye ni mwanachama wa klabu ya Malindi, lakini hawezi kutoa maamuzi kwa lengo la kuibeba.
Rais huyo wa ZFA alisema tatizo kubwa linaloikabili soka ya Zanzibar ni ukiukwaji wa kanuni na kusisitiza kuwa, iwapo halitapatiwa ufumbuzi, litakwamisha maendeleo ya mchezo huo.
Alisema yapo baadhi ya mambo, ambayo klabu zinaweza kukubaliana kama vile mfumo wa mgawo wa mapato, lakini si uendeshaji wa ligi.
“Katika hili, ni kweli kwamba kanuni zimevunjwa na timu zilizoshuka daraja, zimeonewa,”alisema rais huyo wa ZFA, ambaye ameichezea Malindi kwa miaka 11 na pia kuiongoza kwa kipindi kama hicho.

No comments:

Post a Comment