KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, December 8, 2010

NATAFUTA KAZI


MIMI NI MSICHANA MWENYE UMRI WA MIAKA 25, MKAZI WA ARUSHA, NATAFUTA KAZI YA NDANI KWENYE NYUMBA YOYOTE YA KIONGOZI WA SERIKALI AMA MFANYABIASHARA. KWA ALIYE TAYARI KUNIPATIA AJIRA, AWASILIANE NAMI KUPITIA NAMBA HII YA KAKA YANGU 0774-455808

Friday, December 3, 2010

Wacheza filamu wanaong'ara Bongo




STEVEN KANUMBA
Amedhihirisha kwamba ujuzi wa kuigiza haupatikani kwa kukaa kwenye darasa lenye kuta nne na kujifunza, bali ni kipaji cha kuzaliwa na ubunifu wa kila mara.
Ni msanii ghali ambaye 'hakodishiki' na watayarishaji filamu wa Bongo zaidi ya wafanyabiashara wenye asili ya kiasia, maarufu kama Wadosi. Kwa sasa, Kanumba ameamua kuwa mtayarishaji filamu na pia msanii kwa wakati mmoja na ni kipenzi cha mashabiki wengi wa fani hiyo katika nchi za Afrika Mashariki. Sura yake pekee inatosha kuuza filamu husika.

VICENT KIGOSI 'RAY'
Kwa mujibu wa watayarishaji wa filamu, Ray ndiye msanii ghali zaidi wa kiume nchini, ambaye anapendwa na mashabiki wengi ndiyo sababu katika filamu kumi bora nchini, huwa ameshiriki katika filamu saba. Ukizungumzia filamu za Tanzania kwa sasa, unamzungumzia Ray na kipaji chake kimempa thamani kubwa mbele ya jamii.

JACOB STEVEN 'JB'
Ni msanii mwenye vituko, ambaye ukimuona akiwa mtaani kwake Sinza jijini Dar es Salaam, huwezi kuamini kuwa ndiye staa unayemuona kwenye filamu kwa jinsi anavyojirahisisha.Amekamata sehemu kubwa ya soko na asilimia kubwa ya filamu alizocheza zinafanya vizuri sokoni. Hivi karibuni, JB aliwahi kutaka ajulikane kwa jina la Amitha Bachchan, mwigizaji nyota wa zamani wa Kihindo.
SINGLE MTAMBALIKE 'RICH'
Katika wasanii waliokaa miaka mingi kwenye tasnia hiyo, Rich ni mmojawapo kwani miaka ya nyuma aliwahi kutamba katika maigizo ya televisheni. Ni msanii mwenye staili ya aina yake, ambaye muda wowote ule unatamani kumuangalia kwenye filamu na maharamia wengi wamekuwa wakinufaika kwa kuuza kinyemela kazi zake na mastaa wengine.
MZEE CHILO
Babu ndiyo jina linalomtambulisha zaidi katika fani ya filamu. Anaweza akawa ndiye msanii mwenye umri mkubwa kuliko wote kwenye tasnia ya filamu nchini, lakini hakuwahi kuwaboa mashabiki. Amefiti kwenye sehemu nyingi alizoigiza na anathibitisha usemi kuwa 'Simba hazeeki maini' kwani amekuwa akifanya vitu, ambavyo hata vijana wa kisasa hawawezi kufanya wala kuiga.
MAHSEN AWADHI 'CHENI'
Hana haja ya kutambulishwa kwa mashabiki wa filamu nchini kwani ameifanya kazi hiyo miaka mingi na uzoefu wake unamsaidia kwani anafiti kila sehemu anayoigiza.
Anazo staili zake, ambazo zimekuwa zikisisimua mashabiki wake kila wanavyomuangalia kwenye runinga na ni ngumu kutamani filamu imalizike ndiyo maana soko lake litazidi kuwa juu siku zote.
TINO
Kwa mujibu wa watayarishaji wa filamu, msanii huyu ni miongoni mwa mastaa wa kiume wanaopendwa sana na mabinti ndiyo maana hupenda kumtumia zaidi kwenye filamu za mapenzi.
Kila anapocheza filamu, anatoka na staili mpya na unadhifu wake pamoja na utundu imeelezwa kuwa ni miongoni mwa vitu vinavyomfanya azidi kupendwa.
CLOUD
Si msanii ghali sana kwa mujibu wa watayarishaji wa filamu, lakini cha kushangaza ni kwamba, amefanya kazi nyingi kwa kiwango cha juu, ambacho wakati mwingine huwafunika hata waigizaji maarufu zaidi yake. Yumo miongoni mwa wasanii mahiri na wenye majina makubwa nchini kuanzia kwenye maigizo mpaka filamu.
CHUZI
Ana majukumu mengi katika tasnia hiyo kwani mbali na kuwa mwigizaji, anahusika kwa kiasi kikubwa katika kutengeneza filamu na tamthilia mbalimbali, ambazo zinafanya vizuri. Amejijenga vilivyo na anadhihirisha kipaji chake kwenye runinga.
HEMED NA MLELA YUSUF
Wanachosema baadhi ya watayarishaji wa filamu ni kwamba, wasanii hawa ni wepesi wa kuelewa ndio sababu wamekuwa wakipenda kufanyanao kazi katika filamu na kung'ara, ingawa hawako miaka mingi. Wanapewa nafasi kubwa ya kuzidi kung'ara kadri siku zinavyoendelea kwa vile wamepokelewa vizuri sokoni, ingawa imewahi kuvumishwa kuwa waligombana na baadaye wakasuluhishwa.
NURDIN MOHAMMED a.ka.Chekibudi
Hadhi yake kwa mashabiki imekuwa juu sana katika miezi ya hivi karibuni kutokana na kushiriki kucheza filamu nyingi, ambazo zimefanya vizuri na sura yake imetokea sana. Imefahamika rangi yake ndiyo inachengua mashabiki wa fani hiyo hasa wa kike.
BABA HAJI NA SAJUKI
Wana miaka kadhaa kwenye fani hiyo ya uigizaji na kila kukicha wamekuwa wakifanya mambo ambayo yamekuwa yakizidi kuwakuza na kuongeza thamani yao. Ingawa wanaweza wakawa si maarufu sana kwa mashabiki kama walivyo mastaa wengine, filamu nyingi walizoigiza zimefanya vizuri sokoni.
IRENE UWOYA
Hashikiki kwa gharama. Baadhi ya watayarishaji wa filamu wamemuelezea kuwa ni msanii wa kike anayependwa zaidi kwa sasa na ghali zaidi, ingawa yeye mwenyewe amekuwa mara kadhaa akikataa.Uzuri wake, umbo na kipaji ndivyo vitu vinavyombeba. Inadaiwa kuwa ni miongoni mwa wasanii, ambao hata akiigiza upuuzi, mashabiki lazima wanunue filamu yake bila kujali.
ROSE NDAUKA
Silaha yake kubwa ni ubunifu ingawa hata uzoefu umemsaidia na kwamba yupo katika orodha ya wasanii bora watano wa kike kwa sasa kwenye filamu za Tanzania.Hakuna anayemuangalia kwenye video akaacha kutabasamu. Anaigiza kwa hisia zinazoteka akili ya mtazamaji.
AUNT EZEKIEL
Uzuri wake pamoja na staili za mavazi vinambeba, lakini neno unaloweza kutumia kumuelezea ni kwamba ana kipaji cha ukweli. Utundu wake katika kuigiza umewatoa wengi machozi kama si kuwafanya wabadili staili ya maisha kutokana na funzo wanalopata. Imeelezwa kuwa hata kashfa zinazomuandama kila siku zimemjengea jina na kumuongezea mashabiki zaidi.
JACKLINE WOLPER
Ukweli unabaki palepale kwamba ni msanii, ambaye muda wowote utavutika kumuangalia yeye binafsi au filamu aliyoigiza kutokana na staili yake na urembo aliojaliwa. Awe anaigiza kama mpenzi au mke, anafanya vizuri kazi yake kuanzia mwanzo mpaka mwisho.
MONALISA
Tofauti yake na wenzake ni kwamba ana uzoefu mkubwa, ambao pengine katika wasanii wa umri wake wanaong'ara kwa sasa, hakuna wa kumfunika kwa hilo. Wadau wanadai kuwa ni mkali kwenye uigizaji mara mbili au tatu ya Uwoya na Aunt Ezekiel, lakini wao wamekuwa maarufu zaidi kutokana na haiba zao na kashfa za kila kukicha.
JOHARI
Zilipoanza kuvuma filamu, ndio alikuwa kama malkia na wasanii wengi wa kike wanaotamba kwa sasa wamejifunza mambo mengi kutoka kwake. Ni msanii mwenye mvuto, ambaye hawezi kufanana na wenzake kutokana na ubunifu wake na kufanya mambo kwa kiwango cha juu zaidi. Wadau wanadai alistahili kuwa tajiri mkubwa kwa sasa kutokana na kipaji chake.
RIHAMA ALLY
Ni msanii mwenye kipaji cha aina yake, ambacho hakuna mtayarishaji yeyote wa filamu anaweza kupuuzia au kuacha kukitumia. Sababu kubwa ya kutumika kwenye filamu nyingi ni kutokana na kuwapa mashabiki kile wanachohitaji na anajiamini mno ndio maana hakuwahi kufanya vibaya.
MAMA KAWELE
Ukiangalia filamu yake, hutabanduka kwenye kiti kwa jinsi alivyo na uwezo mkubwa wa kucheza na hisia zake na kukusisimua kwa kile atakachokuwa akiigiza.
FLORA MVUNGI
Hazuiliki ni mjanja balaa. Kuanzia watayarishaji wa filamu mpaka wasanii wenzake wanakubaliana na hilo bila ubishi, ndiyo maana amezidi kuwa juu siku zote. Kipaji chake kinafanya filamu ionekane kamili na ndio sababu kubwa ya kupendwa.
MAYA
Yamesemwa mengi, lakini hakuna anayeweza kuwa kama yeye wala kufanya anachokifanya kwenye filamu, ndio maana wasanii wakubwa kama Ray na Kanumba wanapenda kumtumia mara nyingi kwenye kazi zao. Anateka nyoyo za watazamaji na kuwaacha kwenye ulimwengu wa kufikirika.
THEA
Wanajaribu kumpambanisha na Rihama pamoja na Aunt Ezekiel, lakini mwisho wa siku anabaki kuwa juu na kuthibitisha kwamba uzoefu ni kitu muhimu katika kila jambo. Anajua anachokifanya na mashabiki wanamfanya thamani yake izidi kupanda.
LULU
Ni binti mdogo, ambaye amejipatia umaarufu wa haraka kwa muda mfupi kutokana na kipaji alichoonyesha kwenye filamu kadhaa alizofanya chini ya Ray, lakini hata mvuto wake unachanganya wengi. Alikumbwa na kashfa za hapa na pale katika miezi ya hivi karibuni ambazo ni kubwa kushinda umri wake na zimechangia kukuza jina lake na kufanya mashabiki wamfuatilie.
MAINDA
Ray amemkubali, ingawa imekuwa ikielezwa kuwa wana uhusiano wa kimapenzi, lakini msanii huyo wa kike ni kama ametekwa kabisa na Ray kwani katika filamu zake karibu zote yumo na amefanya vizuri na thamani yake ni kubwa.
JINI KABULA
Kabula, ambaye aliwahi kuwa na uhusiano na mwanamuziki Mr. Nice, kazi zake zimemfanya amekuwa maarufu na ni ngumu kumfunika. Ni msanii mwenye kipaji cha aina yake ambaye, orodha hii ya wasanii wanaotumika sana kwenye filamu haiwezi kutimia bila jina lake kuwepo.
NORA
Ukifanya tathmini ya haraka, unaweza kusema Nora na Johari wamefunikwa na vijana wanaowika kama Uwoya na Aunt Ezekiel, lakini kwa mujibu wa maelezo ya watayarishaji wa filamu, wasanii hao ni tofauti na kila mmoja ana thamani yake na bado anakubalika sokoni.

Thursday, December 2, 2010

Wacongo wa Yanga wakwama Dar

KLABU ya Yanga imesema, itawasajili wachezaji wake wapya, Itubu Imbem na Selenga Motitya kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wakati wa msimu wa ligi wa 2011/12.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, klabu hiyo imeshindwa kuwasajili wachezaji hao wakati wa usajili wa dirisha dogo kutokana na kushindwa kupata vibali vya uhamisho wa kimataifa kutoka klabu yao.
Wachezaji hao wawili wanatoka timu ya AFC Leopards ya Kenya, Itubu akiwa anacheza nafasi ya ushambuliaji wakati Selenga ni mchezaji wa kiungo.
Chanzo cha habari kutoka ndani ya Yanga kimeeleza kuwa, wachezaji hao wawili waliletwa nchini na Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Davis Mosha kwa ajili ya usajili wa dirisha dogo.
“Tatizo ni kwamba wachezaji hao walikuja wakati zikiwa zimebaki siku chache kabla ya usajili wa dirisha dogo kufungwa, hivyo haikuwa rahisi kufanya mazungumzo na klabu yao na kuwapatia uhamisho wa kimataifa,”kilisema chanzo hicho.
Kiliongeza kuwa, kufuatia usajili wao kukwama, uongozi umepanga kuwasajili katika ligi ya msimu wa 2011/12 iwapo benchi la ufundi litaridhishwa na viwango vyao vya soka.
Mtoa habari huyo alisema, timu hiyo inatarajiwa kuanza mazoezi kesho kwenye uwanja wa shule ya kimataifa ya Tanganyika, Dar es Salaam ikiwa chini ya Kocha Kostadin Papic.
“Lengo letu ni kuwabakisha ili tuwasajili katika ligi ya msimu ujao, lakini kabla ya kufanya hivyo, lazima tuwajaribu na kuridhishwa na viwango vyao,”alisema.
Katika usajili huo wa dirisha dogo, Yanga imefanikiwa kuwasajili mshambuliaji Davis Mwape kutoka Zambia na Juma Sefu kutoka JKT Ruvu ya mkoani Pwani.
Mwape amesajiliwa kwa ajili ya kuziba pengo la Kenneth Asamoah kutoka Ghana, ambaye klabu ya Yanga imeshindwa kupata uhamisho wake wa kimataifa kutoka katika klabu aliyokuwa akiichezea nchini Serbia.
Katika hatua nyingine, uongozi wa Yanga umeshindwa kufikia makubaliano na klabu ya African Lyon kuhusu usajili wa mkopo wa kipa Ivan Knezevic kutoka Serbia.
Yanga ilipanga kumuuza kipa huyo Lyon ili ipate nafasi ya kusajili mchezaji mwingine kutoka nje ya nchi kwa vile tayari imeshafikisha wachezaji watano wanaohitajika kwa mujibu wa kanuni.
Mmoja wa viongozi wa Yanga alithibitisha jana kuwa, viongozi wa Lyon wamegoma kumnunua kipa huyo kwa mkopo kwa madai kuwa, hawamuhitaji.

KUMBE JK MKALI WA KUPIGA GITA!


RAIS Jakaya Kikwete akipiga gita wakati alipowaongoza wanafamilia, kumpongeza mkewe, Mama Salma Kikwete wakati wa sherehe ya kutimiza miaka 47 iliyofanyika Ikulu mjini Dar es Salaam jana. (Picha ya Ikulu).

SAM WA UKWELI: Namshukuru Mungu, sasa nimetimiza malengo yangu


KWA kipindi cha takriban miezi mitatu sasa, kibao cha ‘Sina raha’ cha msanii Salum Mohamed Salum, maarufu kwa jina la ‘Sam wa Ukweli’, kimekuwa kikishika chati kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini.
Kushika chati kwa kibao hicho kumetokana na mambo mawili makubwa. Kwanza ni mpangilio wa ala za muziki na sauti mwanana ya mwimbaji na pili ni ujumbe uliomo kwenye kibao hicho.
Ni kibao kinachozungumzia masuala ya mapenzi, ambapo kijana Sam wa Ukweli anasikika akimlalamikia mwanadada fulani kwa kumtesa kimapenzi kiasi cha kumfanya asiwe na raha.
Akizungumza na Burudani wiki hii, Sam alikiri kuwa, kibao hicho kimempatia umaarufu mkubwa nchini kutokana na kukubalika kwa mashabiki wengi wa muziki wa kizazi kipya.
Kibao hicho ndicho kilichobeba jina la albamu yake ya kwanza yenye jumla ya vibao kumi. Mbali na ‘Sina raha’, vibao vingine vilivyomo kwenye albamu hiyo ni ‘Hata kwetu wapo’, ‘Usiniache mchumba’, ‘Lifti’, ‘Utamu ulokela’, ‘Lonely’, ‘Huwezijua’, ‘Penzi la kushare’, ‘Tunda la msimu’ na ‘Sina raha remix’.
“Kwa kweli kibao hiki kimefanya vizuri sana sokoni kuliko nilivyotarajia. Ni kibao kilichoniweka kwenye chati ya juu. Nashukuru kwamba mashabiki hivi sasa wananikubali sana,”alisema Sam.
“Nawashukuru mashabiki kwa kunisapoti. Kwa kweli hivi sasa ukitaja majina ya wasanii watatu wa muziki wa kizazi kipya hapa nchini, jina langu haliwezi kukosekana,”aliongeza msanii huyo, asiyekuwa na makeke.
Sam alisema albamu hiyo iliyoanza kuuzwa Oktoba mwaka huu na ambayo aliirekodi kwenye studio za Imotion Records za mjini Dar es Salaam, imemwezesha kutimiza mahitaji yake mengi muhimu ya kimaisha.
“Nashukuru kwamba hivi sasa napata pesa ya ugali, siwezi kufa njaa. Nina uwezo wa kununua kila ninachokihitaji kwa mahitaji muhimu ya kibinadamu,”alisema.
Sam alisema anashukuru kwamba, mafanikio ya albamu yake hiyo sokoni yametimiza malengo aliyokuwa amejiwekea baada ya safari ndefu ya kiusanii, iliyokuwa na vikwazo vya kila aina.
Alivitaja baadhi ya vikwazo alivyokuwa akikabiliana kuwa ni pamoja na kukosekana kwa studio za kurekodi nyimbo mahali alikokuwa akiishi, Kiwangwa mjini Bagamoyo mkoani Pwani.
“Kwa kweli, vikwazo nilivyowahi kukumbana navyo kimuziki ni vingi na vya kukatisha tamaa, lakini nilipiga moyo konde na kuamua kupambana navyo, nikiamini kwamba ipo siku Mungu atajibu dua zangu,”alisema.
Kufuatia mafanikio aliyoyapata, Sam alisema kwa sasa anajiandaa kurekodi wimbo mpya pamoja na video yake, akiwashirikisha wasanii chipukizi wawili, Miundombinu na Sal B kwa lengo la kuibua vipaji vyao.
Msanii huyo alisema kwa sasa, wapo wasanii wengi chipukizi wenye vipaji hapa nchini, lakini tatizo kubwa linalowakabili ni uwezo mdogo wa kifedha kwa ajili ya kurekodi nyimbo zao.
Alisema gharama za kurekodi nyimbo studio pamoja na kutengeneza kanda za video ni kubwa na kuongeza kuwa, kwa wasanii wengi chipukizi si rahisi kumudu gharama hizo.
Sam amewashukuru maprodyuza wa muziki, waandishi wa habari na watangazaji wa vituo vya radio kwa kumpa sapoti na kuzipa nafasi kazi zao kusikika na kutambulika kwa mashabiki.
Ametoa wito kwa wasanii chipukizi kufanyakazi kwa kujituma na pia kuipenda kazi yao ili iweze kuleta ushindani katika soko la muziki na kuwavutia mashabiki.
Sam, ambaye anavutiwa na wasanii Ambwene Yesaya ‘AY’ na Judith Wambura ‘Lady JayDee’, alianza kujihusisha na muziki mwaka 2005 kwa kuimba nyimbo za kuiga za wanamuziki mbalimbali wa zamani kama vile marehemu Marijani Rajabu na za bendi ya Msondo Ngoma.
Kutokana na umahiri wake wa kuiga nyimbo hizo, baadhi ya jamaa zake walimshauri ajitose kwenye fani hiyo kikamilifu kwa kutunga na kuimba nyimbo zake mwenyewe.
Hata hivyo, hakuweza kurekodi nyimbo hizo hadi mwaka 2007 baada ya kukutana na prodyuza Kisaka, ambaye alimshirikisha kwenye tamasha la kusaka vipaji lililofanyika kwenye ukumbi wa Moment Park, Kiwalani Dar es Salaam. Katika tamasha hilo, Sam aliibuka mshindi.
Baada ya kushinda tamasha hilo, Sam aliingia mkataba na Prodyuza Sam kwa ajili ya kurekodi nyimbo zake kupitia lebo ya kampuni yake na hadi sasa yupo chini ya kampuni hiyo.

Z'bar yajiweka pabaya Kombe la Chalenji


TIMU ya soka ya Zanzibar, Zanzibar Heroes jana ilikwaa kisiki katika michuano ya Kombe la Chalenji baada ya kupokea kichapo cha bao 1-0 kutoka kwa Ivory Coast katika mechi ya kundi B iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kipigo hicho kimeiweka Zanzibar Heroes kwenye nafasi ngumu ya kutinga robo fainali, ambapo sasa italazimika kushinda mechi yake ya mwisho dhidi ya Rwanda itakayochezwa kesho.
Pamoja na kupata kipigo hicho, Zanzibar Heroes inashika nafasi ya pili katika msimamo wa kundi hilo, ikiwa na pointi tatu sawa na Ivory Coast, lakini ipo mbele kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.
Mshambuliaji Kipre Bolou ndiye aliyepeleka kilio kwa Zanzibar baada ya kuifungia Ivory Coast bao hilo pekee na la ushindi dakika ya 61. Alifunga bao hilo kwa shuti kali la umbali wa mita 30.
Katika pambano hilo, Ivory Coast ilionyesha kiwango cha juu cha soka, hasa kipindi cha kwanza kabla ya Zanzibar kushtuka dakika za mwisho, lakini washambuliaji wake walipoteza nafasi kadhaa za kufunga mabao.
Katika mechi nyingine ya kundi hilo iliyochezwa jana, Rwanda na Sudan zilishindwa kutambiana baada ya kutoka suluhu.
Pambano hilo halikuwa na msisimko mkali kutokana na timu zote mbili kushindwa kuonyesha soka ya kuvutia.

SHIBOLI, mshambuliaji mpya wa Simba mwenye ndoto za kufika mbali kimuziki

MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya Zanzibar, Zanzibar Heroes, Ally Ahmed Shiboli ametamba kuwa, ataibuka mfungaji bora katika michuano ya mwaka huu ya Kombe la Chalenji inayoendelea kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam wiki hii, Shiboli alisema amedhamiria kuibuka mfungaji bora wa michuano hiyo ili aweze kutimiza malengo aliyojiwekea kisoka.
Majigambo hayo ya Shiboli yamekuja siku chache baada ya kuifungia Zanzibar mabao mawili, ilipoibwaga Sudan mabao 2-0 katika mechi ya kundi B iliyochezwa kwenye uwanja huo.
“Nimedhamiria kumaliza mashindano haya nikiwa mfungaji bora. Ndoto yangu imeanza kukamilika kwani nimeweza kufunga mabao mawili peke yangu katika mechi moja,”alisema.
Mshambuliaji huyo aliyesajiliwa na klabu ya Simba katika usajili wa dirisha dogo akitokea KMKM ya Zanzibar alisema, amepania kuifungia bao Zanzibar katika kila mechi atakayocheza.
“Nimedhamiria kucheza kwa kujituma na kuifungia timu yangu mabao mengi zaidi ili tumalize mechi za kundi letu tukiwa wa kwanza,”alisema.
Shiboli alisema Zanzibar imeanza vyema michuano ya mwaka huu kutokana na maandalizi mazuri waliyoyafanya ikiwa ni pamoja na wachezaji kufuata vyema mafunzo ya Kocha Stewart Hall kutoka Uingereza.
Zanzibar ilitarajiwa kutupa karata yake ya pili jana kwa kumenyana na Ivory Coast, ambayo katika mechi yake ya kwanza, ilichapwa mabao 2-1 na Rwanda.
Akizungumzia usajili wake Simba, Shiboli alisema alikuwa na ndoto za kuichezea timu hiyo kwa kipindi kirefu, lakini hakuwa akifahamu angewezaje kufika huko.
Alisema aliposikia kwamba viongozi wa Simba, Yanga na Azam, zote za Dar es Salaam wanamtafuta, alifarijika kwa kutambua kwamba kiwango chake kimewakuna.
Shiboli aliwavutia viongozi wa klabu hizo tatu baada ya kuonyesha soka ya kiwango cha juu wakati Zanzibar Heroes ilipomenyana na Dar es Salaam All Stars katika mechi za kirafiki zilizochezwa Dar es Salaam na Zanzibar.
Awali, Mwenyekiti wa klabu ya Yanga, Llyord Nchunga aliwaambia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam wiki iliyopita kuwa, walikuwa katika hatua za mwisho za kumsajili mchezaji huyo na kwamba mazungumzo kati yao yalikuwa yakienda vizuri.
Lakini siku chache baadaye, Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ alitoa taarifa kuwa, klabu hiyo imefanikiwa kumsajili Shiboli kwa mkataba wa miaka mitatu.
Shiboli anatarajiwa kuanza kuichezea Simba katika mzunguko wa pili wa ligi kuu ya Tanzania Bara, unaotarajiwa kuanza Januari 15 mwakani. Simba inaongoza ligi hiyo kwa tofauti ya pointi mbili kati yao na watani wao wa jadi Yanga.
Alipoulizwa kuhusu matarajio yake kwa Simba, Shiboli alisema hawezi kuwaahidi mengi mashabiki wa timu hiyo, lakini alisisitiza kuwa, atacheza kwa kujituma ili kuisaidia ifanye vizuri katika ligi hiyo.
“Ni vigumu kwa sasa kusema nitafanya nini Simba kwa sababu mimi ni mgeni na ligi kuu ya Tanzania Bara, lakini kwa vile lengo langu ni kupata mafanikio zaidi kisoka, nitafanya kila ninaloweza kuisaidia timu yangu mpya,”alisema.
Wakizungumzia usajili wa mchezaji huyo, baadhi ya wachezaji nyota wa Simba, akiwemo kipa Juma Kaseja walikiri kuwa, timu yao imepata mshambuliaji hatari na mwenye uwezo wa kuiletea mafanikio zaidi.
Kaseja alisema Shiboli ni mshambuliaji mwenye uwezo wa kufanya lolote kila anapofika karibu na lango la upinzani na pia ana uwezo mkubwa wa kufunga mabao kwa mashuti ya mbali.