KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, November 30, 2013

SALAM ZA MALINZI KWA JK

 
SALAMU ZA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA KWENYE HAFLA YA KUPOKEA KOMBE HALISI LA DUNIA TANZANIA
 
Mheshimiwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete- Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
 
Mheshimiwa Dk. Fennela Mukangara- Waziri wa
Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo
 
Ndugu Dioniz Malinzi- Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT)
 
Mkuu wa msafara wa FIFA/Coca-Cola
 
Bw Yebeltal Getachew- Meneja Mkazi wa Coca-Cola
 
Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF
 
Wageni waalikwa
 
Mabibi na mabwana
 
Mheshimiwa Rais, nianze kwa kukushukuru kwa heshima uliyoupatia mpira wa Tanzania kwa kukubali kuwa mgeni rasmi katika hafla yetu hii ya kupokea Kombe halisi la Dunia.
 
Hii ni mara ya tatu kwa Tanzania kupewa heshima hii na FIFA na washirika wake kampuni ya vinywaji ya Coca-Cola.
 
Coca-Cola ni washirika wetu wa karibu na wamekuwa wakidhamini mashindano ya kitaifa ya vijana tangu
mwaka 2007, mashindano ambayo kwa kiasi kikubwa yamesaidia kuibua vipaji vingi ambapo baadhi yao wameweza kuchezea timu zetu za Taifa na klabu za Ligi Kuu na Daraja la Kwanza.
 
Tunawashukuru sana Coca-Cola na tunaahidi  kuendelea kuwapa ushirikiano katika jitihada zao za kuendeleza soka ya vijana.
 
Mheshimiwa Rais, tarehe 19 Novemba, 2009 wakati unapokea kombe hili hili hapa Tanzania ulitoa changamoto kadhaa kwa uongozi wa mpira wa Tanzania.
 
Ulitushauri tuimarishe uongozi na utendaji wetu kuanzia ngazi ya Taifa, Mikoa, Wilaya hadi klabu, ulitushauri tupate walimu wenye uzoefu wa kutosha kufundisha timu zetu za mpira na pia ulitushauri tuwekeze katika kuibua na kuendeleza vipaji vya wachezaji toka wakiwa na umri mdogo.
 
Mheshimiwa Rais ushauri wako kwetu tuliuzingatia na tulifanya jitihada za kuufanyia kazi. Hali ya utulivu katika uendeshaji mpira wetu imeimarishwa na pale palipoonyesha dalili za migogoro tulikemea na ikibidi tulichukua hatua madhubuti kutatua migogoro.
 
Tumefanya kozi mbalimbali za kuwaendeleza walimu wetu wa mpira, waamuzi, madaktari na viongozi wetu wa ngazi mbalimbali na matokeo yake yanaonekana katika kuinuka kwa viwango vyao vya ufundishaji na utoaji uamuzi uwanjani.
 
Mheshimiwa Rais kama ulivyotuelekeza mwaka 2009 maendeleo ya soka ya vijana ndio ufunguo wa maendeleo ya mpira kwa Taifa letu. Uongozi mpya wa TFF ulioingia madarakani alfajiri ya tarehe 28, Oktoba 2013 tayari unalifanyia kazi jambo hili kwa umakini mkubwa.
 
Uongozi wetu umeamua kuwa ufunguo wa mpango endelevu wa soka ya vijana utakuwa ni Tanzania kuwa mwenyeji wa fainali za Afrika za vijana chini ya umri wa miaka 17 mwaka 2019.
 
Fainali hizi uhusisha mataifa manane yanayogawanywa katika makundi mawili ya awali akiwemo mwenyeji ambaye anaingia moja kwa moja kwenye hatua ya makundi ya fainali hizi. Aidha timu mbili zinazoongoza makundi haya mawili moja kwa moja huwa zinacheza fainali za dunia za vijana chini ya umri wa miaka
17.
 
Fainali hizi ndizo ziliwaibua akina Luis Figo, Ronaldino, Nwankwo Kanu, Michael Essien, Nii Lamptey, Celestine Babayaro na wengine kadhaa.
 
Ili tupate timu nzuri ya vijana umri chini ya miaka 17 mwaka 2019 itabidi mwaka kesho 2014 tufanye mashindano ya kitaifa ya vijana chini ya umri wa chini wa miaka 12 ili tupate kikosi cha kwanza cha Taifa U-12, kikosi ambacho kitakuwa pamoja kuelekea 2019.
 
Katika kuboresha kikosi hiki mwaka 2015 tutafanya mashindano ya kitaifa ya umri chini ya miaka 13, 2016 yatakuwa ya umri chini ya miaka 14, 2017 yatakuwa ya umri chini ya miaka 15 na 2018 yatakuwa ya umri chini ya miaka 16 na ambayo yatatupatia kikosi cha mwisho cha kuingia nacho fainali za vijana mwaka 2019.
 
Tunaamini timu nzuri za Taifa U-17 ya mwaka 2019 itatuzalishia kikosi imara kitakachoshiriki Olimpiki za 2020, kucheza CHAN na AFCON zitakazofuata na hatimae kufaulu fainali za dunia 2026 ambayo ni miaka kumi na tatu kuanzia sasa.
 
Ninashukuru tarehe 21 Novemba 2013, Shirikisho la mpira barani Afrika (CAF) liliniteua kuwa Mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya michuano ya Afrika umri
chini ya miaka 17 (CAF U-17 Organizing Committee), tunaamini kuwepo kwangu katika kamati hii muhimu ya CAF kutasaidia Tanzania ipate wenyeji huu mwaka 2019.
 
Mheshimiwa Rais kwa mujibu wa kanuni za CAF nchi inayoomba uenyeji wa fainali za michuano ya Afrika haina budi ionyeshe barua ya kuungwa mkono na nchi yake(Letter of support from Government).
 
Wiki ijayo tutawasilisha barua kwenye Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ya kuomba kuungwa mkono na Serikali katika azma yetu hii, tunaomba Serikali ituunge mkono katika jambo hili.
 
Mheshimiwa Rais nimalizie kwa kukushukuru tena kwa uwepo wako katika shughuli hii muhimu, ninaishukuru Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwa ushirikiano wanaotupa katika shughuli zetu za kila siku, FIFA nawashukuru sana kwa kutuwezesha kuwa moja ya nchi 88 duniani zilizopokea kombe hili, Coca-Cola asanteni sana tuzidi kuwa karibu.
 
Watanzania wenzangu ninaomba tuje kwa wingi kesho Jumamosi kutembelea Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuliona Kombe hili na kupiga nalo picha. Imani yangu ni kuwa ipo siku Kapteni wa Timu yetu ya Taifa atamkabidhi Rais wa Tanzania kombe hili.
 
Asante

WAMBURA AUKUBALI UTEUZI WA RAGE, ASEMA HANA LENGO LA KUMBEBA MTU


"Hivi karibuni niliteuliwa na Mwenyekiti wa Klabu ya Simba Mhe Ismail Aden Rage  kuwa mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba.Wanachama na wapenzi wengi wa Simba kutoka sehemu mbali  nje na ndani ya nchi walinipiga simu, wengine wakinitaka nikatee uteuzi na wengine wakinitaka nikubali uteuzi, kila mmoja  akiwa na sababu zake,  Wakati napokea uteuzi huu na kutafakari ilibidi nijiridhishe  katika mambo mbalimbali  yakiwemo yafuatayo:

1. Uhalali wa uteuzi huu kisheria na  hasa  kwa kuzingatia hali halisi  ya sasa ya siasa za Klabu.
2. Nini mantiki ya  kuteuliwa kwangu  wakati huu wa mgogoro na nini hasa nafasi yangu.
3. Nini utakuwa mchango wangu katika kamati ya Utendaji katika wakati huu na baadaye.
4. Wajibu wangu ni nini kama mwanachama wa Simba.
5. Nini chanzo cha mgogoro huu wa Simba na ulazima wa wanachama wa Simba Kuingia Katika Mgogoro huu.
6. Utayari wa pande mbili zinazopingana kurudi katika meza ya Mazungumzo
7. Athari za muda mfupi na Mrefu kwa Klabu ya Simba  kwa kurejea migogoro mbali mbali iliyo wahi  kutokea  katika siku za Nyuma.
8. Kina nani hasa watakaofaidika zaidi na mgogoro huu (viongozi wa Simba, Wanachama wa Simba, Klabu ya Simba  au wapinzani na maadui wa Simba).
9. Nini Nafasi ya TFF katika kutatua na Kupatia ufumbuzi wa mgogoro huu.

Baada ya kujiuliza na kutafakari nilitambua na kujiridhisha kama ifuatavyo:

1. MAMALAKA YA MWENYEKITI KUTEUA WAJUMBE WAWILI WA KAMATI YA UTENDAJI YA SIMBA
Kwa mujibu wa Katiba ya Simba Ibara ya 28(1)(d) mwenyekiti anaweza kuteua wajumbe wawili kuingia kwenye Kamati ya Utendaji ya Simba , bila kutoa  nafasi ya Wateuliwa kuuliza wameteuliwa kutoka katika kundi lipi kati ya Wajumbe wawili. Kwa mantiki hiyo mwenyekiti anapewa  nguvu za kikatiba kuteua wajumbe wawili ambao anaona wanaweza kumsaidia katika shughuli  mbalimbali za kuendesha klabu na sio zawadi au shukurani kama ambavyo wengi wamekuwa wakitafsiri,nadhani jambo muhimu la kuhoji ni wanaoteuliwa wanakwenda kufanya nini kwenye kamati ya Utendaji kwa maana ya uwezo wao kuisaidia Simba na sio nani ateuliwe na nani asiteuliwe kwani hilo liko katika mamalaka ya  mteuzi alimradi tu anayeteuliwa ni mwanachma wa Simba na ataongeza tija kwa klabu.
2. NINI MANTIKI YA KUTEULIWA  KWANGU   KATIKA WAKATI HUU WA MGOGORO  NA NINI HASA NAFASI YANGU
Wanachama na wapenzi wengi wa Simba walitafsiri uteuzi huu umefanyika kwa nia ya kumsaidia mwenyekiti ili aendelee kukaa madarakani, watu wenye mawazo hayo pamaoja na wengine waliokuwa na mawazo  tofauti na hayo hawakuangalia na kuzingatia  kwa upana sababu za uteuzi huu, Ukweli ni kwamba wajumbe wote wa kamati ya Utendaji ya Simba akiwemo mwenyekiti walikuwa ni sehemu ya mgogoro huu hivyo isingekuwa rahisi  pande zinazopingana  kutafuta suluhu kama itahitajika, hivyo ni wazi ni mtu  mwingine mwenye uzoefu na  uwezo wa kutatua mgogoro huu na  ambaye hakuwa na upande wowote katika mgogoro huo alihitajika , aidha ninamini kuwa  Uzoefu wangu katika uongozi wa mpira wa miguu na Elimu  yangu Ulifaa  kuingia katika Kamati ya Utendaji ya Simba ili pamoja na mambo mengine niweze kutafuta na kurejusha amani katika Simba , ninapenda ieleweke kuwa katika mgogoro huu mimi sikuwa na sina pande wowote katika pande  mbili zinazopingana , jambo lililonifanya  kujiuliza ikiwa nitakubali uteuzi  huu Simba Itafaidika na nini na kama nikikataa uteuzi  Smba itapata hasara kiasi gani, niligundua kukataa kuna athari kubwa zaidi kwa Simba aidha ingekua pia ni udhaifu na kukosa ukomavu katika uongozi ambao kwa kiasi kikubwa uamuzi huo ungetafsiriwa ni kuweka mbele ubinafsi badala ya maslahi ya walio wengi na klabu, watu wengi walijiuliza inakuwaje Rage  kumteua Wambura  na mimi kukubali kufanya kazi nae  hasa ukizingatia mahusiano yao katika siku za nyuma katika utawala wa mpira wa miguu, Jibu langu ni kuwa SIMBA KWANZA  MAHUSIANO YA MTU NA MTU BAADAYE.

 3. NINI UTAKUWA MCHANGO WANGU WA SASA NA SIKU ZA BAADAYE  KWA SIMBA.

Baada ya kutafakari kwa  kina mchango wangu kama mjumbe wa kamati ya Utendaji ya Simba kwa siku za usoni, niligundua ya kuwa sitakuwa na msaada wowote kwa klabu yangu kama mgogoro huu hautakwisha na viongozi kurudi katika meza moja na kufanya kazi ambayo wanachama wa Simba walitegemea wafanye wakati wanawachagua,  hivyo niliona ni vyema nikachukua jukumu la kuingilia kati mgogoro huu ili niweze  kujua nini hasa kiini cha mgogoro huu katika Uongozi wa Simba. Nilipata nafasi ya kuongea na Mwenyekiti wa Simba na  kisha kuongea na mjumbe mmoja moja waliochaguliwa  wa Kamati ya Utendaji na Kisha kukutana nao kwa pamoja katika siku tofauti tofauti, ili kujua kiini na sababu za sintofahamu iliyokuwa inaendelea ndani ya Uongozi wa Simba, Kwanza nina penda kuwashukuru wajumbe  wote wa kamati ya Utendaji ya Simba Kwa Ushirikano mkubwa na mzuri walionipa, ufahamu wao  na uelewa wao wa masuala ya Simba umeonyesha  ukomavu mkubwa na weledi  katika uongozi wa Simba, tumefanya mazungumzo marefu , makubwa na ya Kina juu ya mstakabali wa Klabu yetu,  wajumbe walikuwa na masikitiko na manung’uniko mbalimbali ya msingi ambayo kimsingi mwenyekiti atakaporejea atakutana na kamati yake ili mamabo ya msingi yaliyozungumzwa yafanyiwe kazi na kupanga utekelezaji  wake. Mwenyekiti ameisha taarifiwa juu ya auamuzi huu.  Msingi wa mazungumzo yetu uliegemea zaidi athari ambazo Klabu yetu ingeezipata katika kipindi hiki kuelekea ligi Mzunguko wa pili na mchezo kati yetu na Mahasimu wetu YANGA katikati ya mwezi wa December pamoja na  athari  nyingine ambazo klabu yetu ingepata kimapato kupitia wadhamini  na wafadhili mbali mbali walio na mikata na wasio nayo, aidha wapenzi na wanachama wengi wasiopenda migogoro  wameamu kukaa mbali na Timu yetu viwanjani na nje ya uwanja, aidha wapenzi wengi wa Simba wamepoteza ujasiri wa kuizungumzia na kuitetea Klabu yao mitaani popote walipo kwa kuwa hawajui siku inayofuata kutatokea  jambo gani litakalo wakarahisha, kwa kuzingatia hayo yote ndio maana wajumbe wakaridhia mazungumzo ya kutafuta amani na umoja katika klabu yaendelee na sasa anasubiriwa mwenyekiti ili nae atumie busara zake kumaliza mvutano huu ambao kwa sasa umeisha fikia tamati kati ya 85%-90%.
Kwa mujibu wa Katiba ya Simba Ibara 28(1)MUUNDO WA KAMATI YA UTENDAJI “Kamati ya Utendaji inaundwa na Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti na wajumbe waliochaguliwa  na Mkutano Mkuu pamaoja na wajumbe walioteuliwa”aidha ibara hiyo inasomeka pamoja na ibara ya 33(1)&33(3)a,b,c,d,e,f,g,h. Kwa mantiki hiyo bila Mwenyekiti hakuna Kamati ya Utendaji na Mwenyekiti bila wajumbe hakuna Kamati ya utendaji jambo ambalo lingepelekea Simba kusimsmisha shughuli zote kwani shughuli zote za Simba muhimu zitafanyawa na kuidhinishwa na kamati ya Utendaji kwa mujibu wa katiba ya Simba ibara ya 30(1)a,b,c,d,e,f,g,h,i,j,k,l,m.

Aidha katika kuendeleza nia ya kuifanya Simba Moja nitajitahidi katika siku za hivi karibuni nikitane na wanachama wa  Matawi ambayo yanaonekana au kuhisiwa  kutokuwa na uhusiano mzuri na uongozi wa Simba kama (Mpira Pesa, Vuvuzela na mengine) ili kujua sababu za kutokuwa na mahusiano Mazuri na uongozi ili kutafuta suluhisho la kudumu na hatimae washirki katika shughuli za klabu na  kuifanya Simba Moja isiyokuwa na wanachama wenye matabaka kwa sabau yoyote ile.
4. NINI WAJIBU WANGU KAMA MWANACHAMA WA SIMBA

Wajibu wangu wa uwanachama kama walivyo wanachama wengine  ni wa hiari kwani kila mmoja wetu alichagua kuipenda Simba kwa hiari yake bila Shuruti lolote na bila kujali atapata nini kibinafsi aidha kimaslahi au kiuongozi zaidi ya furaha na maendeleo ya Simba, hivyo  kila mwanachama anawajibu kikatiba na kikanuni kuilinda , kuitumikia na kuiteteta klabu ili ifikie malengo bila kuvunja taratibu na misingi tuliojiwekea, inasikitisha kuona siku hizi kuna baadhi ya watu wako hiari kuona na kusababisha timu ifungwe eti tu kwa kuwa hampendi kiongozi Fulani aliyeko madarakani, hiyo haikubaliki na ninawaomba wanachama na wapenzi wa Simba ikiwa watambaini mtu wa aina hiyo Katika klabu yetu ashughulikiwe mara moja , kwani kuna watanzania wengi  na wapenzi mbali mbali wa Simba nje na ndani  ya Dar-es-salaam(MARA , MTWARA,MANYARA, SONGEA nk) ambao hawajui nini kinachoendelea hapa ila wanaumia sana timu inapofanya vibaya katika michezo mbalimbali. Kuhujumu klabu sio tu kwa kufungisha timu bali hatu kununua na kuuza  vifaa bandia vya michezo vinavyojitambulisha na klabu huku ukijua wazi  klabu haipati  mapato yoyote  wote hawa wanastahili adhabu sawa na stahiki, kutokana na matukio mbalimbali ya kujaribu kuondoa viongozi kabla ya muda wao wa uongozi  kuisha na bila mafanikio inapashwa kuwa somo tosha kwa wanachama kuwa makini wakati wa uchaguzi kuchagua viongozi wanaowafahamu uwezo wao bila kurubuniwa kwa zawadi na pesa ndogo ndogo, kwani katika mfumo wa dunia ya leo sio tu kwenye Siasa hata katika mpira kuanzi FIFA,CAF,TFF mapinduzi yamefutwa na hayakubaliki tena kwa sababu yoyote ambayo iko nje ya utaratibu wa kikatiba.
 Mwanachama unamchagua kiongozi awe madarakani kwa miaka 4 ambayo ni sawa na siku 1460, ukifanikiwa kuuza kura yako kwa Shs 50,000 wakati wa uchaguzi  ni sawa na kuuza na kulipwa shilling  34.24 kwa siku  ambayo haikutoshi hata nauli ya kuja mjini huko ni kuhujumu klabu  kama wengine, nawaomba wanachama wenzangu tuamke tutoke kwenye usingizi huo usioleta tija wala maendeleo na mwisho ni migogoro isiyokwisha katika klabu.
5. NINI CHANZO CHA MGOGORO HUU  WA SIMBA NA ULAZIMA WA WANACHAMA  WA SIMBA KUINGIA KATIKA MGOGORO HUU.

 Baada ya kuongea na pande zote mbili katika mgogoro huu nimebaini sababu kubwa za mgogoro ni:
(i) Mawasiliano(communication) hafifu ndani ya kamati ya utendaji jambo linalosababisha baadhi ya wajumbe kutokujua baadhi ya mambo
(ii) Kukosekana kwa  Dira na mwelekeo (Vision) jambo linalofanya kamati ya utendaji wote au mmoja mmoja kukosa mwongozo wa kujua wapi klabu inaelekea.
(iii) Kukosekana kwa uamuzi wa pamoja na uwazi (collective Decissions and Transparence)  katika baadhi ya  mambo katika uendeshaji wa klabu.
(iv) Kukosa kuaminiana (Trust) miongoni mwa wajumbe wa kamati ya utendaji
(v) Kukosekana kwa Kanuni (regulations) mbalimbali za uongozi na Utawala, usimamizi wa  Fedha, nk.
(vi) Kukosekana kwa mafuzo, warsha , semina na kozi mbali mbali za utawala kwa kamati ya utendaji ili kila mmoja ajue wajibu na mipaka ya madaraka  yake katika Klabu.
Baada ya kubaini  mapungufu hayo, niliona  hizi ni kasoro ambazo zinaweza kurekebishika ndani ya kamati ya utendaji yenyewe ikiwa pande zote zinaweza kukiri mapungufu haya na kutenga wasaa na rasilimali ili kuondoa kasoro  hizo.
Kuhusu wanachama kuingilia mgogoro huu nina amini wanachama wana nafasi yao katika kuleta na kutatua migogoro mbalimbali, lakini katika mgogoro huu wa sasa ulikuwa kati ya mwenyekiti na Wajumbe wake wa Kamati ya Utendaji, hivyo ilikuwa mapema mno kwa wanachama kuingilia mgogoro huu kwa sababu bado ulikuwa ndani ya uwezo wa kamati ya utendaji ya Utendaji ya  Simba.

6. UTAYARI WA PANDE MBILI ZINAZOPINGANA KURUDI KATIKA MEZA YA MAZUNGUMZO

Baada yakuwasiliana na kukutana na pande zote mbili za mgogoro huu, ninapenda kuzishukuru kwa kukubali kukutana ili kumaliza tofauti zao, ni wazi kwenye usuluhishi ni lazima pande zote zitapata na kupoteza kiasi cha matarajio yake sio rahisi upande mmoja ukapata ilichohitaji yenyewe kwa 100% hivyo ni wazi pande zote  kwa kuzingatia umuhimu wa mapatano kwa mustakabali wa Simba Watakaa na kukubaliana kuondoa tofauti zao na kisha kila pande utafuata na kuheshimu  katiba na kanuni kama muongozo katika kufanikisha malengo ya Simba, mwisho wa usuluhishi hakuna upande utakao kuwa umeshinda au kushindwa isipokua Simba  ndio itashinda, ni imani yangu watatambua nje ya Simba hakuna aliyemaarufu miongoni mwao, na pia nana penda kuwashauri wapambe wa pande zote kujiepusha na kutoa  maneno ya kuudhi na kejeli kwa upande mwingine ili kujenga umoja katika Simba.

7. ATHARI ZA MUDA MFUPI NA MREFU KWA KLABU YA SIMBA  KWA KUREJEA MIGOGORO MBALI MBALI ILIYO WAHI  KUTOKE KATIKA SIKU ZA NYUMA.

Mgogoro wowote una matokeo Chanya au Hasi (+ve or –ve results) wakati mwingine migogoro imesaidia kuwakumbusha watawala umuhimu wa kuwatawala watawaliwa  kama walivyo kubaliana kupitia Katiba lakini wakati mwingi migogoro inaishia kuboma kama ilivyo kuwa kwa Yanga kuzaliwa Pan Africa na kwa Simba Kuzaliwa Red Star, hivyo ni jukumu la wahusika kupima kabla ya kuingia katika mgogoro juu ya matokeo yake ya mwisho, kumbukumbu zangu zinanionsha hakuna kiongozi aliyewahi kupita Simba bila migogoro kutokea na hakuna hata mgogoro mmoja uliowahi kuleta matokeo chanya zaidi ya kurudisha nyuma maendeleo ya simba, baadhi ya migogoro ilipelekea hadi  baadhi ya viongozi kupoteza maisha(marehemu Mzee Juma Salum na mhasibu wa Simba)  wakiwa safarini wakijaribu kumaliza mgogoro, baadhi ya viongozi wa Simba waliokutana na  migogoro ni  pamoja na Mzee Hassan Brashi,Marehemu Ngonya, Marehemu mzee  Bamchawi,Mzee Hazali,Mzee Chamshama, Mzee Dalali na wengine wengi ambapo migogoro yote hiyo haikuisaidia  wala kuleta tija kwa Simba, kuna wakati Simba ilikaa karibu  ya miaka mitatu bila ya kuwa na uongozi wa kuchaguliwa Kisheria. Hivyo ni wajubu wa wana Simba tupime na tuamue kama mgogoro huu una tija hasa ukizingatia muda wa uongozi huu inaishia mwezi wa 5(may) 2014 na uchaguzi kufanyika, rai yangu kwa wanasimba kufikiria, kumpima na kutafakari ni kiongozi gani tuna muhitaji kutaongoza kwa miaka 4 ijayo kuanzia 2014 badala ya kusinzia na kuamka wakati wa uchaguzi na kuchagua mtu asiye sahihi na baada kujaribu  kumng’oa kwa kupitia mlango wa nyuma, “mke mzuri hupewa na mwenyezi Mungu ila kiongozi mbovu humchagua wewe mwenyewe na mungu hukubariki ukae nae kwani umemchagua mwenyewe kwa hiari yako”.

8. KINA NANI HASA WATAKAOFAIDIKA ZAIDI NA MGOGORO HUU (VIONGOZI WA SIMBA, WANACHAMA WA SIMBA, KLABU YA SIMBA  AU WAPINZANI WA SIMBA)

Kimsingi wanaoipenda na kuitakia mema Simba hawawezi kwa njia moja au nyingine kufurahia migogoro ya Simba kwani inatia maudhi na kukatisha tamaa ninaamini hata wanachama wengi binafsi hawapendi  hali hii, ila kuna baadhi ya watu wachache hawasemi ila wanafaidika binafsi  kimapato na hali ilivyo sasa na wakati mwingine wa migogoro, viongozi wa Simba hawana faida na migogoro hii kwani inawafanya washindwe kufanya kazi waliyowaahidi wapiga kura wao wakti wa uchaguzi.
Wanaofaidika kwa kiwango kikubwa na mgogogro wetu ni mahasimu na wapinzani  wetu kwani wana hakika bila umoja, mshikamano na upendo hatuwezi kuwa na timu ya Ushindani, hivi sasa timu yetu iko nafasi ya 4 mgogoro huu ukiendelea unaweza kutupeleka pabaya zaidi hata kufika kushuka daraja, wanaokumbuka historia ya Simba  wakati wa Marehemu J.D.Ngonya, tuliwahi kuponea kushuka daraja mechi ya mwisho ya ligi sababu ya migogoro, na wakati ule upinzani haukuwa mkali kiuchumi na kimiundombinu ya mpira  kama wakati huu,  hivyo wana Simba tusitumiwe na kutumia mikono yetu wenyewe kuivunja klabu yetu, tupambane na adui wa nje halafu ndio tuulizane wenyewe tukiwa ndani hakuna haja ya kuchochewa na maadui zetu na kisha



 kuyatangaza matatizo yetu hadharini halafu tunaona ujiko, sifa na ufahari, hii ni hatari kwa Klabu hasa katika biashara kwa maana ya uwekezaji na udhamini kwani  hakuna mfanyabiashara anayependa kuwekeza mahali kwenye fujo na kusiko na utulivu.

9. NAFASI YA TFF KATIKA KUTATUA NA KUPATIA UFUMBUZI WA MGOGORO HUU.                                                                                                                        Simba ni mwanachama wa TFF ambapo TFF ni mwanachama wa FIFA, kimsingi  chombo kikuu kinachosimamia Mpira wa Miguu hapa nchini ni TFF hivyo katika mfumo wa uongozi na uendeshaji wa mpira duniani kila nchi ina chombo kinacho tambuliwa na FIFA katika kusimamia mpira wa miguu katika nchi mwanachama hivyo kwa Tanzania ni  TFF , kwa mantiki hiyo kupingana na TFF kunaweza kuleta hatari na madhara makubwa zaidi kwa Simba, kwani TFF haiwezi kuifutia Simba usajili wake ila inaweza kuisimamisha au kuifukuza uanachama  pale inapoona inapingana na maamuzi yake, mfano  ulitokea kwa Tanzania kufungiwa na FIFA 2000 baada ya kukataa maagizo ya FIFA japo wakati huo FAT ilikuwa na katiba yake, mwaka 2004 Fifa ilifupisha kipindi cha uongozi wa FAT kutoka miaka 4 hadi 3 kwani uchaguzi ulikuwa ufanyike 2005 kama katiba ya FAT/TFF ilivyo kuwa inaelekeza, hivyo sio busara kwa Simba ambaye ni mwanachama wa TFF kupingana nayo,Katiba ya Simba Ibara ya 11(1)f  inazungumzia Wajibu wa Mwanachama “Asiwe na uhusiano wowote wa kimichezo na wanachama waliosimamishwa au kufukuzwa” na hata katiba ya  TFF  inacho kifungu hicho hivyo Simba inaweza kujikuta katika kisiwa ikiwa itatengwa na TFF.                                                                                                         Kwa kuwa suluhisho linaelekea kupatika ni matarajio yangu kuishirikisha TFF katika kufikia makubaliano na kusimamia utekelezaji wa makubaliano ya suluhu .                   Ni matumaini yangu wahusika watanielewa kwani huu ni mtazamo wangu binafsi bila kushauriwa na upande wowote na  ambao hauna lengo la kuusaidia upande wowote wa mgogogoro huu zaidi ya kuzingatia maslahi na mustakabali wa Simba Sports Club kwa Sasa na kwa siku zijazo, ni matumaini yangu Viongozi na Wanachama wa Simba watachukulia maoni haya kama changamoto na sio vinginevyo, na kwa wale ambao wengependa kuhukumu basi vyema kwanza kuzingatia yafuatayo i): Laws(sheria zilizopo),ii) Evidence(Ushahidi uliopo) na  Iii) Facts of the matter(Uhalisia wa jambo).  
MUNGU IBARIKI SIMBA, MUNGU IBARIKI TANZANIA. AHSANTENI
Michael Richard Wambura.                                                                             
Nakala:                                                                                                                   :Mwenyekiti Simba Sports club                                                                                              
:Rais- TFF                                                                                                                                                   :Wajumbe Kamati ya Utendaji SIMBA

Friday, November 29, 2013

KOMBE LA DUNIA LATUA DAR

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, akilifunua Kombe la Dunia la FIFA katika Uwanja wa michezo wa CCM Kirumba mjini Mwanza jana jioni baada ya kulipokea Kombe hilo lililotua nchini kwa mara ya pili, ambapo leo wananchi watapata fursa ya kupiga nalo picha.
 

Rais Kikwete, akilinyanyua Kombe hilo kwa furaha baada ya kuzindua rasmi shambra shambra za ujio wake nchini katika uwanja wa Kirumba jijini Mwanza jana jioni.
 
Rais Kikwete, akifurahia hukua kiwa ameliinua Kombe hilo juu kuwaonyesha wananchi waliojitokeza kwenye Uwanja wa Kirumba kulipokea. Wananchi wa Jiji la Dar es Salaam, leo watapata fursa ya kupiga picha na kombe hilo katika Uwanja wa Taifa.

TFF YATOA AGIZO KWA WANACHAMA WAKE


Wanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wanatakiwa kufanyia marekebisho katika katiba zao kwa kuingiza ibara ya Kamati za Maadili.

Maagizo hayo yanatokana na kikao cha Kamati ya Utendaji ya TFF iliyoketi Novemba 23 mwaka huu jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jamal Malinzi ambapo pamoja na mambo mengine ilijadili umuhimu wa wanachama wake kuunda kamati hizo.

Wanachama wa TFF ambao muda wao wa uchaguzi umekaribia, wanatakiwa kufanya marekebisho hayo kwanza kabla ya kuingia kwenye mchakato wa uchaguzi.

TFF ina aina tatu za wanachama. Wanachama hao ni vyama vya mpira wa miguu vya mikoa, vyama shiriki na Klabu za ligi Kuu.

FAINALI YA KOMBE LA UHAI CHAMAZI
Mechi ya Fainali ya michuano ya Kombe la Uhai inayoshirikisha timu za umri chini ya miaka 20 za klabu za Ligi Kuu itachezwa keshokutwa (Jumapili) kwenye Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

Coastal Union ndiyo itakayocheza fainali hiyo kuanzia saa 9.30 alasiri dhidi ya mshindi wa mechi ya nusu fainali ya pili kati ya Yanga na Mtibwa Sugar inayotarajia kuchezwa baadaye leo.

Mechi ya fainali itatanguliwa na ile ya kutafuta mshindi wa tatu kati ya Azam na timu itakayoshindwa katika mechi ya pili ya nusu fainali ya michuano ya mwaka huu iliyoanza katika viwanja vya Karume na DUCE kabla ya kuhamia Chamazi.

Thursday, November 28, 2013

SIOGOPI KUTIMULIWA-KESHI


LAGOS, Nigeria
KOCHA Mkuu wa timu ya taifa ya Nigeria, Stephen Keshi, amesisitiza kuwa, hana wasiwasi wa kutimuliwa kabla ya kuanza kwa fainali za Kombe la Dunia za 2014 zitakazofanyika Brazil.
Ikiwa chini ya Keshi, Nigeria ilifanikiwa kufuzu kucheza fainali za kombe hilo baada ya kupata ushindi wa jumla wa mabao 4-1 dhidi ya Ethiopia katika mechi za hatua ya mtoano.
Keshi, ambaye alikuwa nahodha wa Nigeria miaka 1980, aliwahi kuzikosa fainali za michuano hiyo mara mbili baada ya kuiwezesha nchi hiyo kufuzu kucheza kombe hilo.
Mwaka 2002, Keshi alikuwa msaidizi wa Shuaibu Amodu wakati Nigeria ilipofuzu kucheza fainali za kombe hilo, lakini makocha hao wawili walitimuliwa na nafasi yao ilichukuliwa na Adegboye Onigbinde. Fainali za mwaka huo ziliandaliwa kwa pamoja na Korea Kusini na Japan.
Miaka minne baadaye, Keshi alipatwa na mkasa mwingine unaofanana na huo baada ya Chama cha Soka cha Togo kumtimua, licha ya kuiwezesha nchi hiyo kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2006 zilizofanyika Ujerumani.
Keshi (51) ameelezea msimamo wake huo siku chache baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Shirikisho la Soka la Nigeria (NFF), kinafanya mipango ya kuajiri kocha mzungu kwa ajili ya fainali za Brazil.
"Kazi hii ni ya kuajiriwa na kutimuliwa,"amesema Keshi. "Wakati nilipotimuliwa 2002, nilipatwa na mshtuko, lakini ndivyo maisha yalivyo. Sote tunaendelea na maisha kwa sababu huwezi kuendelea kuishi kwa hasira na kukata tamaa."
"Tunazungumzia Nigeria hapa, hivyo huwezi kujua nini kinaweza kutokea. Lakini jambo la muhimu kwa sasa ni kwamba, tumeelekeza nguvu na akili zetu katika kile kilicho mbele yetu, ambacho ni kuwaandaa wachezaji, si kingine,"alisema kocha huyo.
Keshi alisema si jambo zuri kwa mtu kuisumbua akili yake juu ya kile kinachoweza kutokea. Alisema anashukuru amefanikisha kufanya kile, ambacho wengi hawakuwa na matarajio nacho na kwamba kazi hiyo inaendelea.
"Siwezi kuishi kwa woga wa kutimuliwa. Kiukweli, ni kupoteza nguvu,"alisisitiza.
Keshi amekuwa na uhusiano mbovu na waajiri wake,NFF, tangu alipokiongoza kikosi cha Nigeria, kilichokuwa kikiundwa na vijana wengi wapya, kutwaa ubingwa wa Afrika mapema mwaka huu nchini Afrika Kusini.
Kocha huyo na wasaidizi wake, wanadai mishahara ya miezi saba na Keshi amelipwa mishahara ya miezi miwili tu tangu alipoiongoza Nigeria kutwaa kombe hilo, ikiwa ni mara ya kwanza tangu 1994.
 Mwanasoka huyo mkongwe ameielezea hali hiyo kuwa, inakatisha tamaa na haikubaliki na ameishutumu NFF kwa kushindwa kumlipa malimbikizo ya mishahara yake.
Waziri wa Michezo wa Nigeria, Bolaji Abdullahi amemshutumu Keshi kwa kulizungumza suala hilo kwenye vyombo vya habari.
Pamoja na kutolipwa mishahara yake, Keshi amesisitiza kuwa, ataendelea na kibarua chake cha kuinoa Nigeria na kujenga timu itakayofanya maajabu Brazil.
Amesema amestushwa na taarifa za maofisa wa NFF kutaka kuajiri kocha wa kigeni kwa ajili ya kumsaidia wakati wa fainali za Kombe la Dunia.
"Sihitaji msaada wa kocha wa kigeni, kuiongoza Nigeria kufanya vizuri katika fainali za Kombe la Dunia, hivyo kama kuna mtu anataka iwe hivyo, nitakataa ofa hiyo kwa sababu tayari ninao wasaidizi ninaofanyakazi nao,"amesema Keshi.

NYOTA 10 WAONGEZWA MIKATABA YANGA

KLABU ya Yanga imewaongezea mikataba ya muda mrefu, wachezaji wake nyota 10 na sasa wataendelea kuitumikia timu hiyo hadi mwaka 2016.
Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kaziguto alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, uamuzi wa kuwaongezea mikataba wachezaji hao, umetokana na mapendekezo ya benchi la ufundi.
Wachezaji walioongezewa mikataba ni Kelvin Yondani (2014-2016), Nadir Haroub 'Cannavaro' (2014-2016), Athumani Iddi 'Chuji' (2014-2016), Simon Msuva (2014-2016) na Jerry Tegete (2014-2016).
Wengine ni Saidi Bahanuzi, Salum Telela, David Luhende, Oscar Joshua na Didier Kavumbagu, ambao nao wameongezewa mikataba ya miaka miwili hadi 2016.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Abdalla Bin Kleb amesema, wachezaji hao ni baadhi ya waliomaliza taratibu zote za kutia saini mikataba mipya, itakayowafanya waendelee kuitumikia klabu hiyo kwa miaka miwili zaidi.
"Tupo katika mazungumzo ya mwisho na wachezaji wetu wengine na mazungumzo yanaendelea vizuri. Tunaamini muda si mrefu, nao tutakuwa tumeshamalizana nao ili waweze kuendelea kuitumika Yanga tena kwa muda mrefu, "alisema Bin Kleb.
Uamuzi wa Yanga kuwaongezea mikataba wachezaji hao, umekuja baada ya kuwepo na taarifa kwamba, baadhi ya klabu, ikiwemo Simba, zilianza kuwanyemelea baada ya kubaini kwamba mikataba yao inakaribia kumalizika.
Wakati huo huo, kikosi cha Yanga kinaendelea na mazoezi kwenye uwanja wa Bora ulioko Mabatini-Kijitonyama kwa ajili ya maandalizi ya mechi yao ya kuwania Ngao ya Hisani dhidi ya Simba.
Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kaziguto alisema jana kuwa, kikosi hicho kinafanya mazoezi kikiwa chini ya kocha wake, Ernie Brandts.
Baraka alisema pia kuwa, uongozi wa Yanga umemtumia salamu za pongezi, beki Kelvin Yondani kwa kuteuliwa kuwa nahodha mpya wa kikosi cha Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, kinachoshiriki michuano ya Kombe la Chalenji, iliyoanza jana nchini Kenya.

USAJILI DIRISHA DOGO KUFUNGWA DESEMBA 15


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limesema usajili wa dirisha dogo, ulioanza mapema mwezi huu, unatarajiwa kufungwa Desemba 15 mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa na TFF kwa vyombo vya habari juzi, imezitaka klabu zote zinazoshiriki michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara, kuheshimu kanuni na kuzingatia muda uliowekwa.
"Pia tunapenda kuzikumbusha klabu kuwa, kupeleka mchezaji kwa mkopo katika klabu nyingine, hakutoi nafasi ya kusajili mchezaji mpya. Kama klabu ilisaji wachezaji 30, maana yake ni kwamba, haina nafasi ya kuongeza wachezaji," imesema taarifa hiyo.
 TFF imesema, kwa upande wa wachezaji wa kigeni (foreign players), kuanzia msimu ujao wa 2014/2015, watakuwa watatu tu badala ya watano wa sasa.
Imesema pia kuwa, kuhusu usajili wa wachezaji kutoka nje, mpaka sasa hakuna hata klabu moja iliyoingia kwenye TMS kuomba uhamisho.
"Itakapofika Desemba 15, utaratibu huo wa TMS utafungwa," imesema taarifa hiyo.
Wakati huo huo, TFF imesema, imepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha mwamuzi wa zamani wa FIFA, Andrew Kiloyi kilichotokea mjini Iringa.
Mwenyekiti wa Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Mkoa wa Iringa, Ramadhan Mahano, alisema juzi kuwa, Kiloyi alifariki dunia Novemba 24 mwaka huu kutokana na ugonjwa wa fangasi ya ubongo.
Kwa mujibu wa Mahano, mwili wa marehemu Kiloyi umesafirishwa kwenda kwao Kigoma kwa ajili ya mazishi.
Kiloyi alizaliwa Mei 5, 1968. Alijiunga na uamuzi wa mpira wa miguu mwaka 1988, ambapo alipata beji ya FIFA mwaka 2001, akiwa mwamuzi msaidizi. Alistaafu uamuzi mwaka 2009 na hadi anafariki, alikuwa mjumbe wa Kamati ya Waamuzi ya Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Iringa (IREFA).

YANGA YAITESA ASHANTI KOMBE LA UHAI



TIMU ya soka ya vijana wa chini ya umri wa miaka 20 ya Yanga, jana ilitoa kichapo cha mabao 2-1 kwa Ashanti United, katika mechi ya michuano ya Kombe la Uhai.
Katika mechi hiyo ya robo fainali, iliyochezwa kwenye uwanja wa Azam Complex, Mbagala, Dar es Salaam, timu zote mbili zilionyesha kandanda ya kuvutia na kuwapa burudani murua mashabiki.
Iliwachukua Ashanti dakika 32 kuhesabu bao la kwanza, lililofungwa na Juma Ally, baada ya kuwachambua mabeki wa Ashanti na kubaki ana kwa ana na kipa wa timu hiyo.
Baada ya kufungwa bao hilo, Yanga ilichachamaa na kusukuma mashambulizi mfululizo kwenye lango la Ashanti. Mashambulizi hayo yalizaa matunda dakika ya 42 baada ya Haruna Rashid kuisawazishia.
Timu zote mbili, zilikianza kipindi cha pili kwa kasi kila moja ikipania kuongeza bao la pili. Juhudi hizo zilizaa matunda kwa Yanga, iliyopata bao la pili dakika ya 75 kupitia kwa Baraka Ally.
Baada ya kufunga bao hilo, Yanga ilianza kucheza mchezo wa kujihami huku Ashanti ikihaha kusaka bao la kusawazisha, lakini milango ilikuwa migumu.
Katika mechi nyingine ya robo fainali iliyochezwa jana, Azam iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Prisons.

CANNAVARO AMPA TANO KASEJA


NAHODHA wa timu ya soka ya Yanga, Nadir Haroub 'Cannavaro' amesema, amefurahia kusajiliwa kwa kipa nyota nchini, Juma Kaseja, aliyeachwa na klabu ya Simba.
Cannavaro amesema, ujio wa Kaseja utakuwa na msaada mkubwa kwa Yanga kwa sababu ni kipa mwenye uzoefu wa michuano ya ligi na kimataifa.
Kaseja alijiunga na Yanga hivi karibuni, akiwa mchezaji huru baada ya kulipwa kitita cha sh. milioni 40.
Kipa huyo wa zamani wa Simba, alitarajiwa kuanza mazoezi na Yanga juzi, lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu.
Kwa mujibu wa Cannavaro, Kaseja ataleta changamoto kubwa kwa timu hiyo, yenye makipa wengine wawili nyota, Ally Mustapha 'Bartez' na Deogratius Munishi 'Dida'.
"Nampenda sana Kaseja kwa sababu ni kipa mzuri na anayependa mazoezi. Naamini uzoefu wake utatusaidia sana katika ligi na michuano ya kimataifa,"alisisitiza beki huyo.
Aliitaja sifa nyingine ya Kaseja ni kuwa kiongozi mzuri wa wachezaji wenzake, kwa kuwaeleza jinsi ya kujipanga na pia kuwakumbusha majukumu yao wanapokuwa uwanjani.
"Nimeshawahi kucheza naye nikiwa Yanga na timu ya Taifa, hivyo namjua vizuri na ninavutiwa na uwezo wake,"alisema Cannavaro.

COASTAL UNION YAIWEKEA NGUMU YANGA



UONGOZI wa klabu ya Coastal Union ya Tanga, umesema hauna mpango wa kumuuza mchezaji wao nyota, Abdul Banda.
Akizungumza kwa njia ya simu jana kutoka Tanga, Mwenyekiti wa Coastal Union, Ahmed Aurora hawako tayari kumuuza mchezaji huyo kwa gharama yoyote.
Aurora alisema hayo baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Banda amejiunga na mabingwa wa Tanzania Bara, Yanga.
"Hatuwezi kumuuza mchezaji wetu yeyote kwa sababu hatuko kwenye nafasi nzuri kwenye msimamo wa ligi na bado tunapigana kuhakikisha tunafanya vizuri katika mzunguko wa pili,"alisema.
Aurora alisema taarifa za Banda kusajiliwa na Yanga, zimeleta mtafaruku kubwa kwa mashabiki wa Coastal Union na kuwaweka kwenye wakati mgumu viongozi wa klabu hiyo.
"Mashabiki wetu wamekuwa wakitusumbua kupiga simu kuulizia hatma ya Banda. Ninachoweza kuwahakikishia ni kwamba, Banda hauzwi na wasubiri watamuona tena katika mechi za mzunguko wa pili,"alisema.
Banda ameibuka kuwa mmoja wa wachezaji nyota wa Yanga, kutokana na staili yake ya uchezaji na pia kupanda mbele kusaidia mashambulizi na kurudi nyuma kuongeza nguvu kwenye ulinzi.
Beki huyo kisiki, amesajiliwa na Coastal Union msimu huu baada ya kupandishwa daraja kutoka kikosi cha pili cha timu hiyo.

Sunday, November 24, 2013

RAGE AITUNISHIA MISULI TFF, ASEMA HAITISHI MKUTANO NG'O


Zifuatazo ni kauli za Ismail Aden Rage ambazo nimemnukuu akiongea na Waandishi kutokana na stori zilizochukua headlines kwa siku kadhaa kuhusu Kamati kumsimamisha kama Mwenyekiti wa Simba.


1. ‘Kwanza napenda kuipongeza kamati ya utendaji ya TFF kwa kuafiki mimi Ismail Aden Rage ndio Mwenyekiti halali wa Club hii ya Simba na nimepata barua yao jana ileile, katika katiba ya Simba kuna kitu wengi hawajui maana ya Kamati ya utendaji wanadhani ni wale watu saba… hapana!!! kamati ya Utendaji ni Mwenyekiti, Makamu wa Mwenyekiti… hamna kaimu hapo, kuna Wajumbe 7 waliochaguliwa katika mkutano halali… , Wajumbe saba wa kuchaguliwa mmoja wapo akiwa ni Mwanamke na wengine wawili wa kuteuliwa na Mwenyekiti, leo nitateua mwingine mmoja.. nimetoa mmoja’

2. ‘Kwa bahati mbaya Club ya Simba haina Makamu Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti alishajiuzulu ila ina Kaimu Mwenyekiti tu ila huku kwenye katiba hatajwi, kwenye katiba ya Simba Makamu Mwenyekiti ana kazi mbili, moja kwa kuelekezwa na Mwenyekiti na pili Makamu Mwenyekiti anafanya kazi wakati Mwenyekiti hayupo’ – Aden Rage

3. ‘Joseph Itangire ni Kaimu Mwenyekiti tu niliemteua lakini hajapata uhalali wa kikatiba kwa hiyo katiba hii inaendelea kusema, mwenye mamlaka ya kuitisha kamati ya Utendaji mara nne kwa mwaka ni Mwenyekiti, nimekua muungwana tumefanya mara 12 mwaka huu.. kama Mwenyekiti hayupo, katiba inasema anakaimu hana mamlaka ya kuitisha kikao chochote kwa mujibu wa katiba kwa hiyo kikao kile kilichofanyika hakina tofauti na kikao cha harusi’

4. ‘Maamuzi yangu kama Mwenyekiti wa Simba sasa, kwa kuwa mkutano ule ulikua ni batili… jana niliandika barua kwa TFF kwamba viongozi hawa wamevunja katiba za TFF, Simba, CAF na FIFA… ukitaka kulalamika ni lazima uwe na ushahidi wa aina mbili unaokubalika ambao ni document na video casette iliyo na sura za watu na maneno yao waliyosema, wana document ambayo kwenye barua ya Malinzi amekiri anayo na imesainiwa na Makamu Mwenyekiti wa Simba Joseph Itangire’

5. ‘Nimesikitika sana na maagizo ya TFF ya kunitaka niitishe mkutano na Wanachama wa Simba ndani ya siku 14, sijui wameitoa wapi kwenye katiba ya TFF na Simba, wamekwenda mbali na kuninyang’anya madaraka… wamenipa alafu wameninyang’anya alafu wamenipa na Ajenda ya mkutano, sasa wamenirudishia madaraka ya nini? mimi kama Mwenyekiti wa Simba… siitishi mkutano, nalindwa na katiba kwa hilo’

6. ‘Unaponipa amri unaninyang’anya madaraka yangu, katiba inasema kama naona itafaa nitaitisha… tuheshimu katiba, nilitegemea taarifa ya kwanza ya TFF mpya ingelaani mapinduzi ya kipuuzi yanayotokea’

7. Heshima yangu mimi ni Mbunge taifa linaelewa hivyo, nimekuta ofisi hii hakuna umeme miaka 18 pamoja na pazia za magunia, nimekuta uhuni mtupu.. wachezaji wameuzwa, Henry Joseph, Matole na wengine uliza wanachama wa Simba ilipata shilingi ngapi? leo imani inawatoka kusikia nimeuza Wachezaji wawili tu Congo DRC milioni 320 na nikaweka wazi hadharani sio kuwaambia Mke wangu na watoto wangu..

8. Leo nimetumiwa msg kutishia kuuwawa na tayari nimesharipoti Polisi, leo hii msg nimepata mtu kaniambia ‘Nisipotoka Simba ataniua’ alivyokua mpumbavu hajui hizi simu zinasajiliwa, nimecheki jina lake mpaka mtaa anaokaa pengine sasa yuko Lupango… why??? mpira ni burudani!! kuna mtu alikua Simba sasa yuko TFF anataka kuleta vurumai ndani ya TFF na Simba, kwa nini? kwa nini ununue watu? waandishi wa habari hebu tuache kuchochea, wewe Mwandishi ni nani ununuliwe? kuna Mwanamke Mwaandishi mmoja kalipwa milioni 2 ili anichafue, sijali.. ‘

9 Nimefanya Demokrasia sana na ndio inanitokea puani, nimeteua kamati… ziko kamati nyingi sana lakini sijaona Mwandishi hata mmoja anakwenda kuuliza kamati ya ufundi, Usajili ila kila mmoja ananishambulia mimi, leo sitaki maswali ya Waandishi wa habari, sasa mna hiari… kuandika au kuacha wala hamnipi tabu nyie, kuchafuliwa nimezoea’

10. Ukitaka kuwa kiongozi teka Ikulu kwanza, hapa ndio ikulu.

KILI STAARS KUAGWA KESHO



Kikosi cha Kilimanjaro Stars kinaagwa kesho (Novemba 25 mwaka huu) tayari kwa safari ya Nairobi, Kenya kushiriki michuano ya Kombe la Chalenji inayoanza kutimua vumbi Novemba 27 mwaka huu.

Hafla ya kuiaga timu hiyo itafanyika saa 5 asubuhi kambini kwao katika hoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam. Msafara wa Kilimanjaro Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager utaongozwa na Ahmed Idd Mgoyi. Timu itaondoka saa 10 alasiri kwa ndege ya RwandAir.

Wachezaji waliomo katika msafara huo ni makipa Deogratius Munishi (Yanga), Ivo Mapunda (Gor Mahia, Kenya) na Aishi Manula (Azam). Mabeki ni Erasto Nyoni (Azam), Himid Mao (Azam), Ismail Gambo (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Michael Pius (Ruvu Shooting) na Said Moradi (Azam).

Viungo ni Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruna Chanongo (Simba), Hassan Dilunga (Ruvu Shooting), Ramadhan Singano (Simba) na Salum Abubakar (Azam).

Safu ya ushambuliaji inaundwa na Elias Maguli (Ruvu Shooting), Faridi Musa (Azam), Joseph Kimwaga (Azam), Juma Liuzio (Mtibwa Sugar), Mbwana Samata (TP Mazembe, DRC), Mrisho Ngasa (Yanga) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, DRC).

Hata hivyo, washambuliaji Samata na Ulimwengu watajiunga na timu hiyo jijini Nairobi, Desemba Mosi mwaka huu wakitokea Lubumbashi ambapo Novemba 30 mwaka huu TP Mazembe itacheza fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Benchi la Ufundi la timu hiyo linawajumuisha Kim Poulsen (Kocha Mkuu), Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi), Juma Pondamali (Kocha wa Makipa), Leopold Tasso (Meneja wa Timu), Dk Mwanandi Mwankemwa (Daktari wa Timu), Frank Mhonda (mtaalamu wa tibamaungo) na Alfred Chimela (Mtunza Vifaa).

Kilimanjaro Stars ambayo ipo kundi B katika michuano hiyo itacheza mechi yake ya kwanza Novemba 28 mwaka dhidi ya Zambia kwenye Uwanja wa Machakos.

Boniface Wambura Mgoyo
Kaimu Katibu Mkuu
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

TFF YATOA AGIZO KWA RAGE


Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage ameagizwa kuitisha Mkutano Mkuu wa Dharura wa klabu ndani ya siku 14 kuanzia sasa.


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetoa agizo hilo baada ya kubaini kuwa mgogoro katika klabu baada ya kupokea barua mbili; moja kutoka Kamati ya Utendaji ikielezea kumsimamisha uongozi Rage, na nyingine kutoka kwa Mwenyekiti huyo ikielezea kutotambua kusimamishwa huko.

Uamuzi wa TFF umefanywa kwa kuzingatia Ibara ya 1(6) ya Katiba ya Simba inayosema: “Simba Sports Club ni mwanachama wa TFF, itaheshimu Katiba, kanuni, maagizo na uamuzi wa TFF na FIFA, na kuhakikisha kuwa zinaheshimiwa na wanachama wake.”

TFF itatuma wawakilishi wake katika mkutano huo, na kumuagiza Mwenyekiti wa Simba kuhakikisha wanachama wote wenye hoja wanapata fursa ya kusikilizwa.

Boniface Wambura Mgoyo
Kaimu Katibu Mkuu
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

TFF YAUNDA KAMATI NDOGO NDOGO



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ametangaza wajumbe wa kamati ndogongo (standing committees) wakati zile za haki (judicial organs) na uchaguzi zitaundwa baadaye.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji kilichofanyika leo (Novemba 23 mwaka huu) jijini Dar es Salaam, Rais Malinzi alisema kamati hizo zimeundwa kwa mujibu wa katiba ili kuisaidia Kamati ya Utendaji.

Pia ametangaza wajumbe wanne wa Kamati ya Utendaji aliowateua. Wajumbe hao ni Richard Sinamtwa na Ramadhan Nassib, wakati wengine wanaoingia moja kwa moja kwenye Kamati ya Utendaji kutokana na kamati wanazoziongoza ni Dk. Paul Marealle na Saloum Umande Chama.

Kamati ya Fedha na Mipango inaongozwa na Makamu wa Rais wa TFF, Wallace Karia wakati wajumbe ni Francis Ndulane (Makamu Mwenyekiti), Omari Walii, Eliud Mvella, Said Muhammed, Geofrey Nyange, Kidao Wilfred, Ayoub Nyenzi, Lina Kessy na Cyprian Kuhyava.

Geofrey Nyange anaongoza Kamati ya Mashindano wakati wajumbe ni Clement Sanga (Makamu Mwenyekiti), Msafiri Mgoyi, James Mhagama, Mohamed Nassoro, Moses Katabaro, Seif Ahmed, Gerald ambi, Davis Mosha, Said George na Nassoro Idrissa.

Kinara wa Kamati ya Ufundi ni Kidao Wilfred wakati wajumbe ni Athumani Kambi (Makamu Mwenyekiti), Vedstus Lufano, Blassy Kiondo, Rahim Kangezi, Patrick Kahemele, Daud Yassin, Nicholas Mihayo na Dk. Cyprian Maro.

Kamati ya Mpira wa Miguu wa Vijana inaongozwa na Ayoub Nyenzi, Khalid Abdallah (Makamu Mwenyekiti), Ali Mayay, Mulamu Ng’hambi, Apollo Kayungi, Said Tully, Luteni Kanali Charles Mbuge, Lameck Nyambaya na Ibrahim Masoud.

Lina Kessy anaongoza Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake wakati wajumbe ni Shyrose Bhanji (Makamu Mwenyekiti), Zena Chande, Amima Karuma, Dk. Cecilia Makafu, Zafarani Damoder, Beatrice Mgaya, Sofia Tigalyoma, Martin Mung’ong’o na Engrid Kimaro.

Kamati ya Waamuzi inaongozwa na Saloum Umande Chama, Nassoro Said (Makamu Mwenyekiti), Charles Ndagala (Katibu), Riziki Majala, Kanali Isaro Chacha, Paschal Chiganga, Victor Mwandike, Soud Abdi na Zahra Mohamed.

Hamad Yahya Juma ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi anaongoza Kamati ya Habari na Masoko wakati wajumbe ni Naibu Waziri January Makamba (Makamu Mwenyekiti), Tido Mhando, Yusuf Manji, Yusuf Bakhresa, Samwel Nyalla, Jack Gotham, Fredrick Mwakalebela na Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA).

Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji inaongozwa na Richard Sinaitwa, Moses Karuwa (Makamu Mwenyekiti), Zacharia Hanspoppe, Hussein Mwamba, Philemon Ntahilaja, Abdul Sauko na Imani Madega.

Kiongozi wa Kamati ya Ukaguzi wa Fedha ni Ramadhan Nassib wakati wajumbe ni Zitto Kabwe (Makamu Mwenyekiti), Nicholas Magarinza, Jackson Songora, Epaphra Swai, Kalilo Samson, Goodluck Moshi, Golden Sanga na Elias Mwanjala.

Dk. Paul Marealle anaongoza Kamati ya Tiba wakati wajumbe ni Dk. Fred Limbanga (Makamu Mwenyekiti), Dk. Mwanandi Mwankemwa, Dk. Nassoro Matuzya, Dk. Eliezer Ndelema na Asha Sadiki

Thursday, November 21, 2013

RAGE MWANAUME WA SHOKA, KAMATI YA UTENDAJI YAMRUDISHA MADARAKANI, KUREJEA NCHINI KESHO



HATIMAYE kamati ya utendaji ya klabu ya Simba imebatilisha uamuzi wake wa kumsimamisha uongozi, mwenyekiti wake, Ismail Aden Rage.

Uamuzi huo umetangazwa mchana huu na Kaimu Makamu Mwenyekiti wa Simba, Joseph Itang'are 'Kinesi' alipokutana na waandishi wa habari Kinondoni, Dar es Salaam.

Awali, Kinesi alipanga kukutana na waandishi hao makao makuu ya klabu hiyo, mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam, lakini akaamua kuhamishia kikao hicho nyumbani kwa mdhamini wa klabu, Hamisi Kilomoni.

Kinesi amesema, wamefikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha kwamba, kikao walichokiitisha na kutangaza kumsimamisha Rage, hakikuwa halali.

Kwa maana hiyo, hata uamuzi wa kumuondoa Kocha, Abdalla Kibadeni na msaidizi wake, Jamhuri Kihwelo 'Julio' nao pia haukuwa sahihi.

Kamati ya Utendaji ya Simba ilitangaza kumsimamisha Rage kwa madai ya kutokuwa na imani na uongozi wake. Tuhuma zingine zilikuwa kufanya maamuzi binafsi bila kuishirikisha kamati ya utendaji na klabu kutonufaika na mauzo ya mchezaji Emmanuel Okwi.

Hata hivyo, Rage alipinga mapinduzi hayo kwa madai kuwa hayakuwa halali, kutokana na kamati ya utendaji kutompa nafasi ya kujitetea kutokana na tuhuma zilizokuwa zikimkabili.

Rage, ambaye wakati wa mapinduzi hayo alikuwepo safarini nchini Sudan, anatarajiwa kurejea nchini leo na amepanga kuitisha mkutano wa dharula wa wanachama Jumapili.

BABU SEYA, PAPII KOCHA WAENDELEA KUSOTA JELA



JOPO la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, limeridhia hukumu ya kifungo cha maisha jela iliyotolewa kwa mwanamuziki Nguza Vicking 'Babu Seya' na mwanawe, Johnson Nguza 'Papii Kocha'.

Uamuzi wa jopo hilo la majaji, ulifikiwa leo kwenye mahakama hiyo baada ya kufanya mapitio ya hukumu hiyo.

Majaji watatu wakiongozwa na Nathalia Kimaro, Mbarouk Mbarouk na Salum Massati, walisoma  hukumu hiyo, ambayo ilikuwa ikisubiriwa kwa hamu kubwa na ndugu, jamaa na marafiki wa Babu Seya na Papii Kocha.

Babu Seya na mwanawe, waliwasilisha maombi ya mapitio hayo juu ya hukumu iliyotolewa Februari, mwaka 2010,  na Jopo hilo la majaji, ambalo liliwatia hatiani kwa makosa ya ulawiti na ubakaji na kuwapa adhabu ya kifungo cha maisha.

Jopo hilo liliwaachia huru watoto wengine wa Babu Seya, Nguza Mbangu na Francis Nguza.
Oktoba 30, mwaka huu, wakati liliposikiliza hoja za kisheria kuhusu maombi ya mapitio zilizowasilishwa na wakili wa Babu Seya, Mabere Marando.

Mara baada ya uamuzi huo wa Mahakama ya Rufani,  Babu Seya aliwaeleza waandishi wa habari kuwa, ameamua kumuachia Mungu suala lao kwa sababu kwa Mungu hakuna makosa.

Kwa upande wake, Papii Kocha alisema kwa sasa wanategemea huruma ya Rais Jakaya Kikwete kwa vile mahakamani wamekwama.

Wakili Gabriel Nyela, aliyemwakilisha Marando alisema: "Hatua hii ni ya mwisho, hatuwezi kukata rufani sehemu nyingine."

Baada ya uamuzi huo wa mahakama, vilio vilisikika kutoka katika kila pembe, hasa vya akina mama, waliokuwa wakiwaonea huruma wanamuziki hao wawili.

Babu Seya na mwanawe wote wenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), walikuwa wanakabiliwa na mashitaka ya kubaka na kuwalawiti watoto 10, kesi iliyosikilizwa kwa mara ya kwanza na kuhumumiwa kifungo cha maisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, Juni 25, 2004.

Awali, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,  iliwatia hatiani Babu Seya na wanawe watatu kwa jumla ya makosa 23 ya ubakaji na ulawiti walioshitakiwa nayo. Mashitaka 18 yalifutwa na uamuzi wa jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani.  Washitakiwa walidaiwa kutenda makosa hayo, kati ya Aprili na Oktoba, 2003.

MALINZI AIAHIDI ZFA UANACHAMA WA FIFA



Na Salum Vuai, Zanzibar

WIKI tatu tangu Jamal Malinzi achaguliwe kuwa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), jana aliwasili Zanzibar na kufanya mazungunmzo na uongozi wa Chama cha Soka (ZFA), na kuahidi kulivalia njuga suala la kuipatia Zanzibar uanachama wa Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA).

Katika mazungumzo hayo Malinzi alizungumzia suala la Zanzibar kupata uanachama wa FIFA  na CAF ambapo, alisema kuwa katika uongozi wake atahakikisha kuwa analishughulikia suala hilo, ili kuona kwa jinsi gani ataweza kulimaliza kwa Zanzibar kupata uanachama.
Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa VIP uwanja wa Amaan, Malinzi alisema katika kipindi chake cha uongozi TFF, atahakikisha  Zanzibar inapata uanachama wa FIFA  pamoja na ule wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
Kwa sasa, Zanzibar ni mwanachama shirikishi wa CAF, ambapo klabu zake zinazotwaa ubingwa wa ligi kuu na nafasi ya pili, huiwakilisha kwenye ligi ya mabingwa na Kombe la Shirikisho.
"Kwa kushirikiana na wenzangu TFF na ZFA, tutalishughulikia suala hilo ili kuona jinsi tunavyoweza kulimaliza kwa Zanzibar kupata uanachama wake FIFA na CAF," alieleza Rais huyo.
Malinzi alisema umefika wakati sasa ZFA ikawa na mwakilishi wake ndani ya Kamati Tendaji ya TFF, na kueleza kuwa, akisema atapeleka pendekezo katika kamati hiyo, ili kuifanyia marekebisho katiba ya shirikisho katika mkutano mkuu ujao.
Alifahamisha kuwa, marekebisho hayo yatafanyika kwa lengo la kuingiza kifungu kitakachoipa Zanzibar nafasi hiyo katika Kamati Tendaji ya TFF.
Kuhusu muundo wa timu za Taifa za Tanzania kwa wachezaji walio katika umri tafauti, Malinzi alisema hivi karibuni, kutafanyika kikao maalumu cha jopo la walimu wa michezo hapa Zanzibar, kwa lengo la kupanga mikakati ya kuimarisha timu hizo.
Kwa upande wa ligi ya Muungano ambayo imekufa kwa miaka mingi baada ya Zanzibar kupata nafasi ya kushiriki yenyewe  katika michuano ya CAF, alisema atahakikisha ligi hiyo inarudi tena japo kwa misingi mipya badala ya ile ya zamani.
Katika hatua nyengine, Rais huyo aliyerithi nafasi ya Leodgar Tenga aliyemaliza muda wake, alisema TFF hivi sasa iko katika mipango ya kuutumia utalii katika kuinua michezo, kwa kuwalika magwiji wa soka wa zamani pamoja na klabu maarufu duniani.
Itakumbukwa kuwa, miaka miwili iliyopita, aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo Ali Juma Shamuhuna, aliongoza ujumbe mzito jijini Geneva, Uswisi kuiombea Zanzibar uanachama wa FIFA, lakini ombi hilo liligonga mwamba ikielezwa kuwa nchi hiyo haitambuliwi kimataifa kwa kuwa inabebwa na Tanzania kupitia TFF.
Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi wote wa juu na wengine wa ZFA akiwemo Rais wake Ravia Idarous Faina.

YANGA B HOI KWA AZAM B



AZAM FC imeendeleza wimbi la ushindi katika michuano ya Kombe la Uhai baada ya kuilaza Yanga mabao 2-0 katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Mabao ya Azam yalifungwa na Adam Omar dakika ya saba na Gadiel Michael dakika ya 39.

Katika mchezo mwingine uliofanyika Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam, Mtibwa Sugar iliichapa Rhino Rangers ya Tabora bao 1-0.

Bao hilo la pekee na la ushindi la Mtibwa lilifungwa na Patrick Mdidi dakika ya 38.

Katika mechi zilizochezwa asubuhi, Ashanti United iliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya JKT Oljoro ya Arusha kwenye uwanja wa Azam Complex.

Mabao yote mawili ya Ashanti yalifungwa na mtoto wa beki wa zamani wa kimataifa wa Tanzania na klabu ya Yanga, Salum Kabunda ‘Ninja Msudan’ (marehemu), aitwaye Ally Salum Kabunda anayecheza na mdogo wake, Hassan Salum Kabunda.

Katika mechi nyingine, Kagera Sugar iliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Prisons ya Mbeya.
Mabao ya Kagera yalifungwa na Mohammed Mohammed na Hassan Rajab.

Kwenye uwanja wa DUCE, Mbeya City iliifunga JKT Ruvu bao 1-0 wakati Ruvu Shooting ikatoka sare ya 1-1 na Mgambo JKT.

23 KUIWAKILISHA BARA KOMBE LA CHALENJI, STARS, ZIMBABWE ZAINGIZA MIL 50/-

 
Kocha Mkuu wa Kilimanjaro Stars, Kim Poulsen ametaja kikosi cha wachezaji 23 watakaoshiriki michuano ya Kombe la Chalenji inayofanyika nchini Kenya kuanzia Novemba 27 mwaka huu.
 
Kilimanjaro Stars iliyotwaa kombe hilo mara ya mwisho mwaka 2010 chini ya Kocha Jan Poulsen, na ambayo imepangwa kundi B katika michuano ya mwaka huu, itacheza mechi yake ya kwanza Novemba 28 mwaka dhidi ya Zambia kwenye Uwanja wa Machakos.
 
Wachezaji wanaounda kikosi hicho cha Tanzania Bara ni makipa Deogratius Munishi (Yanga), Ivo Mapunda (Gor Mahia, Kenya) na Aishi Manula (Azam). Mabeki ni Erasto Nyoni (Azam), Himid Mao (Azam), Ismail Gambo (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Michael Pius (Ruvu Shooting) na Said Moradi (Azam).
 
Viungo ni Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruna Chanongo (Simba), Hassan Dilunga (Ruvu Shooting), Ramadhan Singano (Simba) na Salum Abubakar (Azam).
 
Safu ya ushambuliaji inaundwa na Elias Maguli (Ruvu Shooting), Faridi Musa (Azam), Joseph Kimwaga (Azam), Juma Liuzio (Mtibwa Sugar), Mbwana Samata (TP Mazembe, DRC), Mrisho Ngasa (Yanga) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, DRC).
 
Kilimanjaro Stars inatarajia kuondoka Jumatatu (Novemba 25 mwaka huu) kwenda Nairobi kushiriki michuano hiyo itakayoanza Novemba 27 mwaka huu na kumalizika Desemba 13 mwaka huu.   
 
 STARS, ZIMBABWE YAINGIZA MIL 50/-
Mechi ya kirafiki ya kimataifa ya FIFA Date kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Zimbabwe (The Warriors) iliyochezwa juzi (Novemba 19 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 50,980,000 kutokana na watazamaji 7,952.
 
Tiketi za kushuhudia mechi hiyo ziliuzwa kwa sh. 5,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.
 
Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 7,776,610.17 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh. 3,682,560.
 
Asilimia 15 ya uwanja sh. 5,928,124, asilimia 20 ya gharama za mechi sh. 7,904,166 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 1,976,041.
 
Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 17,784,373 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 889,219 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF

KIGOGO YANGA ASUSA



WAJUMBE wawili kati ya watatu walioteuliwa kuunda Bodi ya Yanga, wameamua kujiweka pembeni kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wa klabu hiyo.

Uchunguzi uliofanywa na Burudani umebaini kuwa, wajumbe hao hawajalipwa mishahara yao tangu walipoteuliwa kushika nyadhifa hizo miezi mitatu iliyopita.

Wajumbe hao, Patrick Naggi kutoka Kenya na Peter Simba, wamekaririwa wakisema kuwa, wameona ni vigumu kwao kuendelea kufanyakazi Yanga wakiwa katika mazingira magumu.

Kwa mujibu wa uchunguzi huo, tayari Naggi amesharejea kwao Kenya wakati Simba ameamua kufanya shughuli zingine nje ya zile za Yanga.

Mmoja wa watu wa karibu na Naggi, aliieleza Burudani wiki hii kuwa, Mkenya huyo alikuwa akiishi hotelini kwa muda wote aliokuwepo nchini na pia kutumia gari la kukodi.

"Kilichomshtua ni kuona kuwa, huduma zote hizo hadi sasa hazijalipwa na uongozi wa Yanga na hivyo kujikuta akiwa kwenye matatizo,"kilisema chanzo cha habari.

Kiliongeza kuwa, Naggi alirejea kwao Kenya baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara na alilazimika kukopa fedha za nauli.

Mkenya huyo aliletwa nchini kwa ajili ya kuchukua nafasi ya Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako.

Chanzo chetu cha habari kieleza kuwa, kuondoka kwa Naggi ni ishara kwamba, hatarajii kurudi tena nchini na ameshaanza kutafuta kazi sehemu nyingine.

Katika hatua nyingine, imebainika kuwa watendaji kadhaa wa klabu ya Yanga hawana mikataba na wamekuwa wakifanyakazi kienyeji.

Uchunguzi wa Burudani umebaini kuwa, miongoni mwa wasiokuwa na mikataba ni pamoja na Kocha Msaidizi, Fred Felix Minziro na maofisa wenzake wa benchi la ufundi, akiwemo daktari.

Kwa mujibu wa uchunguzi huo, Minziro amekuwa akipigwa danadana kila anapoomba kupatiwa mkataba na hali hiyo imewafanya yeye na wenzake kuwa na hofu ya kupoteza haki zao iwapo utakuja uongozi mpya.

Alipoulizwa kuhusu madai hayo jana, Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kaziguto alisema hawezi kuyatolea majibu kwa vile hajapata taarifa hizo kutoka kwa viongozi.