KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 9, 2011

TZ Bara kundi moja na Rwanda, Ethiopia

Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Michezo Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholas Musonye (kulia) akitangaza timu zitakazoshiriki katika michuano ya mwaka huu ya Kombe la Chalenji, alipozungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana. Wa pili kulia ni Rais wa baraza hilo, Leodegar Tenga, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL), Teddy Mapunda na Meneja wa bia ya Tusker, Ritha Chaki. (Na mpiga picha wetu)


MALAWI ndio timu pekee kutoka nje ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, iliyoalikwa kushiriki katika michuano ya mwaka huu ya Kombe la Chalenji.
Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholas Musonye alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, timu 12 zinatarajiwa kushiriki katika michuano hiyo.
Musonye alisema michuano hiyo imepangwa kuanza Novemba 25 na kumalizika Desemba 10 mwaka huu katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.
“Tumeialika timu hii makusudi kwa lengo la kusisimua maendeleo ya soka katika ukanda huu. Ni matumaini yetu kuwa, timu hii italeta changamoto katika michuano hii na kuifanya iwe na ushindani mkubwa,”alisema.
Kwa mujibu wa Musonye, timu hizo 12 zimepangwa katika makundi matatu yenye timu nne kila moja. Aliyataja makundi hayo kuwa ni A litakalokuwa na timu za Tanzania Bara, Rwanda, Ethiopia na Djibouti.
Kundi B litakuwa na timu za Uganda, Burundi, Somalia na Zanzibar wakati kundi C litakuwa na timu za Sudan, Kenya, Malawi na Eritrea.
Katibu Mkuu huyo wa CECAFA alisema, ratiba kamili ya michuano hiyo itatangazwa keshokutwa.
Musonye alisema lengo la CECAFA ni kuona kiwango cha soka katika nchi za ukanda huu kinapanda na mojawapo ya timu zake, inafuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014.
Michuano ya mwaka huu imedhaminiwa na Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) kupitia bia yake ya Tusker. Kampuni hiyo itatumia sh. milioni 823 kudhamini michuano hiyo.
Naye Meneja wa bia ya Tusker, Rita Mlaki aliwataka watanzania kujitokeza kwa wingi wakati wa michuano hiyo kuishangilia Tanzania Bara na Zanzibar ili ziweze kufanya vizuri.

No comments:

Post a Comment