KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 5, 2012

Simba chali kwa Jamhuri


MABINGWA watetezi wa Kombe la Mapinduzi, Simba juzi walianza vibaya kutetea kombe hilo baada ya kuchapwa mabao 2-1 na Jamhuri ya Pemba katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Amaan mjini hapa.
Kipigo hicho kwa Simba kimekuja siku chache baada ya watani wao wa jadi Yanga, nao kuchapwa bao 1-0 na Mafunzo katika mechi nyingine ya michuani hiyo iliyochezwa kwenye uwanja huo.
Katika pambano hilo lililochezwa kuanzia saa mbili usiku, Simba ilipata nafasi nyingi za kufunga mabao kipindi cha kwanza, lakini zilipotezwa na washambuliaji wake.
Nafasi ya kwanza ilipatikana dakika ya 28 wakati Ramadhani Singano aliposhindwa kuunganisha wavuni krosi ya Gervas Kago kabla ya mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Jamhuri ya Afrika ya Kati naye kupotesa nafasi dakika ya 36.
Edward Christopher naye alishindwa kuifungia bao Simba dakika ya 45 wakati alipopewa pasi akiwa ndani ya 18, lakini shuti lake lilitoka nje. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa suluhu.
Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote mbili kuongeza kasi ya mchezo na kufanya mashambulizi mengi zaidi. Mashambulizi hayo yalizaa matunda kwa Jamhuri dakika ya 55 baada ya kupata bao la kuongoza kupitia kwa Ali Othman Mmanga.
Bao hilo liliiongezea nguvu Jamhuri, ambayo ilifanikiwa kuongeza bao la pili dakika ya 66 lililofungwa na Bakari Khamis baada ya kutokea kizaazaa kwenye lango la Simba.
Simba ilizinduka dakika ya 74 na kupata bao la kujifariji kupitia kwa Shomari Kapombe baada ya mabeki wa Jamhuri kuzembea kuokoa hatari kwenye lango lao.
Kocha Mkuu wa Simba, Milovan Cirkovic alisema baada ya mchezo huo kuwa, licha ya kufungwa, timu yake ilicheza vizuri, isipokuwa mabeki wake walimwangusha. “Mabeki wangu leo wameniangusha sana, hasa Nyoso (Juma). Sikutegemea kabisa kuwa ataweza kuachia goli ambalo tumefungwa dakika moja tu baada ya yeye kuingia uwanjani,”alisema.
Kocha Mkuu wa Jamhuri, Renatus Mayunga alisema kufanya vizuri kwa timu yake katika mechi hiyo kumewapa moyo wa kutwaa kombe hilo mwaka huu.

No comments:

Post a Comment