KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, January 9, 2012

KWADWO: Tumepania kufanya maajabu CAN 2012


ROME, Italia
KWADWO Asamoah ni mmoja wa wachezaji wa kimataifa wa Ghana wanaotamba kisoka barani Ulaya kutokana na uwezo mkubwa alionao katika kusakata kabumbu.
Kiungo huyo anayekipiga katika klabu ya Udinese ya Italia, alianza kung’ara mwaka 2010 alipoichezea Ghana katika fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika nchini Afrika Kusini.
Katika mwaka huo, Asamoah aliichezea Ghana katika mechi zote za Kombe la Mataifa ya Afrika na kufuzu kucheza fainali na pia katika mechi za Kombe la Dunia, ambapo Ghana iliweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kutoka Afrika kufuzu kucheza robo fainali.
Kwadwo (23) ni mchezaji mwenye kasi, nguvu na mbinu za aina yake za kuwatoka mabeki wa timu pinzani. Hivi karibuni, alishinda tuzo ya mchezaji bora mwenye kipaji anayechipukia barani Afrika.
Chipukizi huyo wa Ghana alikuwa miongoni mwa wachezaji walioiwezesha Udinese kumaliza msimu wa ligi ya Serie A ya Italia mwaka 2011 ikiwa ya tatu. Mekeke yake uwanjani yalizifanya klabu nyingi za Ulaya kuanza kumkodolea macho, ikiwemo Manchester United ya England.
Kwadwo ni mmoja wa wachezaji waliomo kwenye kikosi cha Ghana, kinachotarajiwa kushiriki katika fainali za mwaka huu za Kombe la Mataifa ya Afrika zinazotarajiwa kufanyika Equatorial Guinea na Gabon.
Ghana ni miongoni mwa nchi zinazopewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri kwenye fainali hizo huku Kwadwo akitarajiwa kung’ara na hivyo kuzivutia zaidi klabu za Ulaya.
Akihojiwa na mtandao wa FIFA hivi karibuni, mwanasoka huyo amekiri kuwa, licha ya Udinese kuuza wachezaji wake nyota kadhaa msimu huu, lakini imeweza kuanza vyema katika ligi ya Serie A na ligi ya Ulaya.
Alisema msimu uliopita, walicheza vizuri na kupambana na timu ngumu, ambazo ziliwasaidia kuwafanya wachezaji wajiamini na hivyo kupata matokeo mazuri.
Kwadwo alisema mafanikio ya Udinese yamechangiwa na timu hiyo kuundwa na wachezaji wengi vijana na wenye kiu ya kupata mafanikio makubwa zaidi kisoka.
‘Timu yetu ni mojawapo yenye wachezaji wenye umri mdogo katika ligi ya Serie A. Tunasaidiana kwa hali na mali uwanjani na tuna umoja wa aina yake. Mwelekeo wetu ni kama ilivyokuwa mwaka jana, japokuwa wamekuja wachezaji kadhaa wapya, ‘ alisema.
Kwadwo amekiri kuwepo kwa tofauti kiuchezaji katika klabu ya Udinese na timu ya taifa. Akiwa Udinese anacheza nafasi ya kiungo mkabaji wakati akiwa kikosi cha Ghana, anacheza nafasi ya kiungo mshambuliaji.
‘Nikiwa Ghana nacheza nyuma ya mshambuliaji wa kati, Asamoah Gyan wakati nikiwa Udinese, nimejifunza kucheza kama kiungo mkabaji nafasi ya kushoto na kusaidia sehemu zote za uwanja. Wakati mwingine hutokea nikacheza nafasi ya ulinzi, ‘alisema.
Kwadwo alitamba kuwa, Ghana ina matumaini makubwa ya kufanya vizuri katika fainali za Afrika kwa vile timu yao ni nzuri, inaundwa na wachezaji wenye kiwango cha juu kisoka na haina matatizo.
Alisema kama watacheza kwa ari na kujituma, kama ambavyo Kocha Goran Stevanovic amekuwa akiwasisitizia, watakuwa tishio kwa timu yoyote watakayocheza nayo.
Kiungo huyo alikiri kuwa, kutokuwepo kwa timu ngumu kama vile Misri, Cameroon na Nigeria katika fainali hizo, kutapunguza ladha ya ushindani, lakini alisisitiza kuwa, kutwaa ubingwa ni kazi ngumu.
‘Siku zote zimekuwa zikijitokeza timu mpya, ambazo hutoa ushindani mkali kwa timu yoyote. Timu zote zilizofuzu kucheza fainali hizi zilistahili,’ alisema.
Kwadwo hakuwa tayari kutabiri timu inayoweza kutwaa ubingwa. Alisema timu zote zitaanza fainali hizo zikiwa katika kiwango sawa, lakini alikiri kuwa huenda yakajitokeza matokeo ya kushangaza.
Akizungumzia michuano ya kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014, Kwadwo alisema Zambia ndiyo timu pekee ya kuihofia katika kundi lao. Timu zingine zilizopangwa kundi hilo ni Sudan na Lesotho.
Kwadwo alisema hakushangazwa Ghana ilipotolewa hatua ya robo katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 2010 kwa sababu hivyo ndivyo mchezo wa soka ulivyo.
“Ndivyo soka ilivyo. Kuna wakati mbaya na vipigo visivyotarajiwa. Jambo zuri ni kwamba siku zote unakuwa na nafasi ya kujirekebisha,”alisema.
“Tulikaribia kufuzu kucheza nusu fainali, lakini dakika za mwisho tulikosa penalti, ambayo ingetuwezesha kuweka historia, lakini inaweza kutokea. Tuna matumaini ya kujirekebisha katika fainali zijazo. Ningependa kupata nafasi hiyo,” aliongeza.
Kwadwo alisema anafurahia maisha nchini Italia, ikiwa ni pamoja na kuichezea Udinese, ambayo alijiunga nayo miaka minne iliyopita.
Pamoja na kuwepo Italia kwa miaka minne, Kwadwo alisema hafikirii kubadili uraia kwa sababu anafurahia asili yake. Lakini alisisitiza kuwa, anafurahia kuishi Italia.
Kiungo huyo alisema pia kuwa, anafurahia chakula cha kiitaliano, lakini anafurahia zaidi kula pasta na ubwabwa, japokuwa wakati mwingine hukikumbuka chakula chao cha asili cha fufu.

No comments:

Post a Comment