KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, August 6, 2012

SIMBA, YANGA, AZAM ZAFANYIANA UMAFIA, MSIMBAZI WAMSAJILI REDONDO KWA MIL 30/-

Klabu za Simba, Yanga na Azam sasa zimeamua kufanyiana vurugu kwa kuchukuliana wachezaji bila kufuata na kuheshimu taratibu za usajili.


Vurugu hizo zilianza jana baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Simba imeamua kumsajili kiungo Ramadhani Chombo Redondo kutoka Azam wakati mchezaji huyo bado ana mkataba na klabu yake.


Habari kutoka ndani ya Simba zimeeleza kuwa, wameamua kumsajili Redondo baada ya mchezaji huyo kuwaeleza kuwa, mkataba wake na Azam umemalizika.

Redondo, ambaye aliondoka Simba takribani miaka 3 iliyopita, amesaini Simba kwa ada ya millioni 30. Kiungo huyo amepewa shilingi millioni 20, na millioni 10 zilizobaki atamaliziwa baadae.

Hata hivyo, kiongozi mmoja wa Azam amesema leo kuwa, mkataba wa Redondo kuichezea Azam unatarajiwa kumalizika Juni mwakani, hivyo Simba imecheza pata potea kumsajili mchezaji huyo.

Wakati Simba ikimsajili Redondo, watani wao wa jadi Yanga walibisha hodi katika Jiji la Kampala nchini Uganda wakisaka saini ya mshambuliaji Emmanuel Okwi wa wekundu hao wa Msimbazi.

Okwi alirejea Uganda wiki iliyopita akitokea Austria alikokwenda kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa na imeelezwa kwamba ameshafuzu majaribio hayo.

Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Uganda alirejea kwao kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya ugonjwa wa malaria alioupata Austria.

Habari za uhakika kutoka Yanga zimeeleza kuwa, mjumbe wake wa kamati ya utendaji, Abdala bin Kleb ndiye aliyetumwa nchini humo kushughulikia usajili wa Okwi.

Yanga imeamua kumuwinda Okwi baada ya kuzidiwa kete na Simba katika usajili wa beki Mbuyi Twite kutoka APR ya Rwanda. Yanga imesema lazima ilipe kisasi Simba kwa kumnyakua Okwi.

Mbali na Yanga, kuna habari pia kuwa, Azam nayo imetinga mjini Kampala, lengo lao kuu likiwa ni kumuwinda Okwi baada ya kupata taarifa kwamba, Simba imemsajili Redondo.

Je, nini utakuwa mwisho wa vurugu hizi? Tusubiri tuone.

No comments:

Post a Comment