KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

CHIDI BENZI AMCHANACHANA AFANDE SELE

MSANII mkongwe wa muziki wa kizazi kipya nchini, Rashid Abdalla 'Chidi Benz' amemponda msanii mwenzake, Selemani Msindi 'Afande Sele' kwa madai kuwa, amepitwa na wakati.
Chidi amesema msanii huyo mwenye maskani yake mkoani Morogoro anapaswa kuchunga kauli zake kwa sababu baadhi ya matamshi yake yanaonyesha kuwa, upeo wake kiusanii ni mdogo.
Chidi alisema hayo wiki hii mjini Dar es Salaam, kufuatia Afande Sele kuuponda uamuzi wa msanii wake wa zamani, Dogo Dito kujiunga na kundi la La Familia.
Afande Sele ameufananisha uamuzi huo wa Dogo Dito kuwa ni sawa na mchezaji kuihama klabu ya Manchestern United na kujiunga na Wolves. La Familia ni kundi linaloongozwa na Chidi Benz.
"Mimi namshangaa sana Afande Sele kwa sababu ni mtu ninayemuheshimu na sikutarajia angeweza kusema maneno kama hayo," alisema.
"Kuifananisha La Familia na Wolves ni makosa makubwa sana kwa sababu kundi langu lipo mjini sio kama Watu Pori (kundi la Afande Sele), ambalo lipo Morogoro, kwa hiyo unapotoa mifano ya aina hii, unapaswa kuwa makini,"aliongeza.
Chidi alisema asingependa kuwa na malumbano na Afande Sele kwa sababu ameamua kubadilika kimaisha na hapendi kuendelea kuwa mtu wa vurugu kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Alisema kwa sasa Dogo Dito yupo kundi la THT hivyo Afande Sele amefanya makosa kulilalamikia kundi lake na kuongeza kuwa, msanii anapotoka kundi moja kwenda lingine hapaswi kulaumiwa kwa sababu anatafuta maslahi mazuri zaidi.

No comments:

Post a Comment