KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 22, 2012

Sitta mgeni rasmi bonanza la TASWA

WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki na mbunge wa Urambo Mashariki, Samuel Sitta anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika bonanza la vyombo vya habari.
Bonanza hilo limepangwa kufanyika keshokutwa kwenye ufukwe wa klabu ya Msasani, Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini (TASWA), Juma Pinto alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, pamoja na mambo mengine, Sitta atakabidhi zawadi ya vikombe na medali kwa washindi.
Mbali na kukabidhi zawadi, Pinto alisema Waziri Sitta atapata fursa ya kuzungumza na washiriki wa bonanza hilo.
Kwa mujibu wa Pinto, bonanza hilo, ambalo huandaliwa kila mwaka na TASWA, litawashirikisha waandishi wa habari 1,500 kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini.
Pinto alisema lengo la bonanza hilo ni kuwaweka pamoja waandishi wote wa habari bila kujali ni wa siasa, michezo, uchumi, afya na mambo mengine pamoja na wafanyakazi wa idara zingine kwa ajili ya kubadilishana mawazo na kufurahi pamoja.
Alisema maandalizi ya bonanza hilo yapo hatua za mwisho, ambapo bendi ya FM Academia ‘Wazee wa Ngwasuma’ watatoa burudani kwa washiriki. Alisema bonanza hilo limepangwa kuanza saa tatu asubuhi hadi saa mbili usiku.
Pinto alisema burudani nyingine zitatolewa na wasanii wa muziki wa kizazi kipya, ambao watatangazwa leo, lengo likiwa kuwa na bonanza tofauti na miaka ya nyuma.
Amevitaka vyombo vya habari, ambavyo havijathibitisha ushiriki wake kwa njia ya maandishi, vifanye hivyo kama vilivyoagizwa kwenye barua zao za mialiko, vinginevyo ushiriki wao hautathaminika.

No comments:

Post a Comment