KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 20, 2011

Salha amuasili mtoto yatima Dar






MREMBO wa Tanzania wa mwaka 2011, Salha Israel ameamua kumuasili mtoto mchanga mwenye umri wa mwezi mmoja, aliyelazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam.
Salha alitangaza uamuzi wake huo mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya kuelezwa mazingira yaliyosababisha mtoto huyo alazwe kwenye hospitali hiyo.
Mrembo huyo wa Tanzania, alifanya ziara kwenye hospitali hiyo, akiwa amefuatana na waandaaji wa kipindi cha Njia Panda, kinachorushwa hewani na kituo cha Radio cha Clouds FM.
Mtoto huyo, ambaye Salha ameamua kumpa jina lake, alikutwa ametupwa vichakani na kuokotwa na wasamaria wema, ambao ndio waliomfikisha Muhimbili.
Salha aliwaeleza wauguzi wa hospitali hiyo kwamba, atahakikisha anamlea mtoto huyo katika maisha yake yote.Mtoto huyo yatima, amelazwa wodi namba 36, ambayo ni maalumu kwa watoto wachanga.
Mlimbwende huyo amesema, katika kipindi chote atakachokuwa akilitumikia taji lake, atajikita zaidi katika harakati za kutetea haki za watoto wachanga.
"Watoto hawa wamekuwa wakisahauliwa kwa kiasi kikubwa. Watu wanakumbuka kuwasaidia watoto kuanzia miaka mitano na kuendelea na kukimbilia kutoa vyandarua na vitu vingine, lakini ukweli ni kwamba kundi la watoto hawa limesahaulika mno, “alisema mrembo huyo.
Mbali na kumuasili mtoto huyo, Salha aliitumia ziara yake katika hospitali hiyo kutoa misaada mbalimbali kwa watoto waliolazwa kwenye wodi hiyo. Misaada iliyotolewa na mrembo huyo ni sabuni za kufulia, maji na mashuka.
“Huu ni mwanzo tu wa kampeni hii, nitakaporudi kwenye mashindano ya dunia, mimi pamoja na wadau wengine wa urembo, tutahakikisha tunafanya kampeni kubwa ya kuihamasisha na kuielimisha jamii katika suala zima la kuwasaidia watoto hawa, ambao baadhi yao hutelekezwa na wazazi wao kutokana na kuwa na matatizo mbalimbali wangali wachanga,” alisema.
Naye Mkuu wa Itifaki wa Kamati ya Miss Tanzania,Albert Makoye aliushukuru uongozi wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuwapa sapoti ya kutosha katika kutekeleza mpango wa kuwasaidia watoto waliolazwa kwenye hospitali hiyo.
Makoye alisema watoto wanaotupwa na wazazi wao kutokana na matatizo mbalimbali, wanastahili kusaidiwa kwa vile wanazo haki zote za kuishi kama watoto wengine.
Wakati huo huo, Salha anatarajiwa kuondoka nchini leo kwenda London, Uingereza kwa ajili ya kushiriki katika fainali za kumsaka mrembo wa dunia. Shindano hilo limepangwa kufanyika Novemba 8 mwaka huu.
Salha aliagwa rasmi juzi na Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi, Athumani Mfutakamba, ambaye alimtaka mrembo huyo kuyatumia mashindano hayo kutangaza vivutio vya nchi. Salha alikabidhiwa fedha taslim sh. milioni tisa kutoka kwa wafanyakazi wa wizara hiyo na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).

No comments:

Post a Comment