KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, April 16, 2014

MAELFU YA MASHABIKI WAILAKI AZAM



MASHABIKI wa Azam FC wamejitokeza kwa wingi jioni ya leo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam kuilaki timu yao, ikitokea Mbeya ambako jana iliifunga Mbeya City na kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.


Msafara wa wa Azam uliwasili kwa ndege ya Fats Jet Saa 12:00 jioni hii na kupokewa na mamia ya wapenzi wake kabla ya kupanda basi lao la kisasa kuelekea makao yao makuu, Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Ilikuwa hoi hoi, nderemo na vifijo katika mapokezi ya timu hiyo ya Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na familia yake katika mapokezi yake baada ya mabingwa hao wapya wa Bara kutua JNIA.

Azam ilitwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jana, baada ya kuifunga Mbeya City mabao 2-1 Uwanja wa Sokoine mjini hapa, huku waliokuwa wapinzani wao katika mbio za taji hilo, Yanga SC wakishinda 2-1 dhidi ya JKT Oljoro mjini Arusha jana pia.

Azam imefikisha pointi 59 ikiwa na mchezo mmoja mkononi ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote baada ya mechi za mwisho Aprili 19, mwaka huu. Yanga SC yenye pointi 55 sasa ikiifunga Simba SC wiki ijayo itafikisha 58.

Mabao ya Azam jana yalifungwa na Gaudence Mwaikimba na John Bocco, wakati la Mbeya City lilifungwa na Mwagane Yeya.

Licha ya kuwa timu ya kwanza kuifunga Mbeya City kwenye Uwanja wake jana, Azam FC pia inakuwa timu ya kwanza nje ya Simba na Yanga kutwaa ubingwa wa Bara tangu mwaka 2000 Mtibwa Sugar ilipofanya hivyo

Azam inakuwa timu ya saba nje ya Simba SC kutwaa taji la Ligi Kuu, baada ya Cosmo mwaka 1967, Mseto mwaka 1975, Pan Africans mwaka 1982, Tukuyu Stars mwaka 1986, Coastal Union 1988 na Mtibwa Sugar mara mbili mfululizo 1999 na 2000.

No comments:

Post a Comment