KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

VUMILIA: Nina mtoto, ndoa bado kidogo


MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Vumilia amekiri kuwa ni kweli kwamba anaye mtoto, aliyezaa na mpenzi wake, lakini bado hawajafunga ndoa.
Vumilia alibainisha hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Friday Nite Live kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha East Africa.
Alisema mtoto wake huyo anaitwa Mariam, lakini haishi pamoja na baba yake na kusisitiza kuwa, mipango ya ndoa bado haijatimia.
Vumilia, ambaye ni mmoja wa waasisi wa kundi la Tanzania House of Talent (THT), amekuwa akitamba kwa kibao chake kipya kinachojulikana kwa jina la ‘Tatizo ni umaskini’.
Alisema alikitunga kibao hicho yeye mwenyewe kutokana na wazo la kubuni na kukanusha madai kuwa, ni tukio lililowahi kumtokea katika maisha yake.
“Unajua watu wengi wamekuwa wakitunga nyimbo za kuelezea matukio mbalimbali, lakini hakuna aliyewahi kuzungumzia jambo hili,”alisema.
“Hivyo kuna siku nilikaa nyumbani na kuwaza sana kuhusu sababu zinazowafanya wazazi kuwakatalia watoto wao wasioe ama kuolewa na watu wanaowapenda ndipo nikapata wimbo huu,” aliongeza.
Vumilia amesema amekuwa akipata nguvu ya kimuziki kutokana na binti yake, ambaye kila anapomuona ameamka salama, hujisikia vizuri. Alimzaa mtoto huyo mwaka juzi.
Mwanadada huyo mwenye sura na umbo la kuvutia alisema, alimzaa mtoto wake huyo kwa kukusudia na si kwa bahati mbaya kama baadhi ya watu walivyokuwa wakimvumishia.
“Wenzangu walidhani nisingeweza tena kuendelea na muziki baada ya kujifungua. Walidhani ningefilisika. Jambo hilo lilinihuzunisha sana. Lakini Mungu alikuwa upande wangu na nikafanikiwa zaidi,”alisema.
Vumilia alisema kwa sasa anafanyakazi ya muziki kwa mafanikio zaidi na anaishi vizuri na baba wa mtoto wake, japokuwa hawaishi pamoja, lakini wanaheshimiana kama mtu na mzazi mwenzake. Mwadada huyo amewataka wasanii wenzake wa kike wanapopata uja uzito, wawe wamedhamiria kwa dhati kuwa na watoto na kufanya hivyo si kosa la jinai.
Mwanadada huyo amesema hadi sasa hajawahi kupata tatizo lolote kimuziki kwa sababu mashabiki wamekuwa wakimpokea vizuri na humshangilia kila anapopanda na kushuka stejini.
Vumilia alijiunga na kundi la THT mwaka 2006 akiwa mmoja wa waanzilishi wake. Wakati akijiunga na kundi hilo, alikuwa na kipaji cha kuimba, lakini alilazimika kujifunza upya.
Akizungumzia wimbo wake wa 'Utanikumbuka', Vumilia alisema umemwezesha kupata mafanikio zaidi kifedha na kimaisha na pia ameweza kuisaidia familia yake.
Alisema alitunga wimbo huo kutokana na matatizo aliyowahi kuyapata dada yake kutoka kwa mume wake, ambapo kila alipokuwa akienda kumtembelea, alimkuta akiwa na majonzi.
Kutokana na kukithiri kwa mates ohayo, Vumilia alisema dada yake alilazimika kuondoka kwa mumewe na kurejea kwa wazazi wake huku akimuapiza mumewe kwamba ipo siku atamkumbuka.
Vumilia alisema anachoshukuru ni kuona kwamba, kibao hicho kimemsaidia dada yake kurejea kwa mumewe kutokana na ukweli kwamba, alianza kumkumbuka kimapenzi.
Mwanadada huyo alisema wapo wasichana wengi wanaopenda kujitosa kwenye fani ya muziki, lakini wanakatishwa tamaa kutokana na kutojitokeza watu wa kuwaunga mkono.
Alisema baadhi yao baada ya kujitokeza, wamekuwa wakikumbwa na tamaa za kimapenzi kwa mapromota, madj na mameneja wao na kusahau majukumu yao.
Kwa sasa, Vumilia ameamua kujifunza upigaji wa vyombo vya muziki likiwemo gita na anatarajia kuzindua albamu yake mpya yenye nyimbo kumi hivi karibuni.
Baadhi ya nyimbo zinazotarajiwa kuwemo kwenye albamu hiyo ni pamoja na ‘Utanikumbuka’, 'Tatizo Umaskini', 'Nenda', 'Akupe Raha', 'Penzi la Kinafiki' na 'Telephone'.
Mbali na kupiga muziki, Vumilia anapendelea kusoma vitabu, kukutana na watu tofauti ili kujua maisha yao na shida zao kwa lengo la kupata matukio ama visa vya kuvitungia nyimbo.
Anavutiwa na uimbaji wa mwanamuziki Pauline Zongo, Juliana wa Rwanda na Nyota Ndogo wa Kenya. Kwa wanamuziki wa kimataifa, anavutiwa na Monica Seka.
Anamshukuru mwalimu mkuu wa kundi la THT, Richard Mangustino kuwa ndiye aliyemfundisha muziki na kumwezesha kufika alipo sasa.

No comments:

Post a Comment