KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 20, 2010

CHUJI: Nitachezea timu yoyote, ninachozingatia maslahi


MSHAMBULIAJI Athumani Iddi ‘Chuji’ wa Yanga hivi karibuni alikaririwa akisema kuwa, huenda akarejea katika klabu yake ya zamani ya Simba baada ya viongozi wa timu hiyo kuonyesha nia ya kumsajili. Katika makala hii ya ana kwa ana, Chuji anaelezea mambo mbalimbali kuhusu maisha yake kisoka na mipango yake ya baadaye.

SWALI: Hivi karibuni ulikaririwa na gazeti hili ukisema kuwa, upo katika mazungumzo na viongozi wa klabu ya Simba kwa ajili ya usajili wa msimu ujao wa ligi. Je, mazungumzo yako na viongozi wa Simba yamefikia wapi hadi sasa?
JIBU: Ni kweli nilikutana na viongozi wa Simba hivi karibuni na katika mazungumzo yetu, walionyesha nia ya kutaka kunirejesha katika klabu hiyo msimu ujao, lakini bado hatujafikia mwafaka, tunaendelea na mazungumzo.
SWALI: Kwa nini hujafikia mwafaka na Simba wakati umeonyesha wazi kwamba hutaki kuendelea kuichezea Yanga msimu ujao kutokana na sababu mbalimbali?
JIBU:Ni kweli, awali niliwahi kusema hivyo, lakini tofauti kati yangu na Simba zimemalika na ndio maana hata mama yangu mzazi alipokuwa anaumwa, walinisaidia sana, kwa kweli nawashukuru kwa jambo hilo.
SWALI: Huoni kama utakuwa umekula matapishi yako na pengine wapenzi wa soka watashindwa kukuelewa?
JIBU: Soka ni sehemu ya maisha yangu ya kila siku, napenda kutengeneza maisha yangu ya baadae kupitia soka,hivyo ninaangalia zaidi maslahi bora kwanza na mapenzi ya klabu baadae.
SWALI: Una mpango wowote wa kuongeza mkataba wa kuichezea Yanga msimu ujao?
JIBU: Nilishafanya mazungumzo na uongozi wa Yanga kuhusu jambo hilo, lakini mfadhili wetu Yusuf Manji alitoa pesa kidogo kwa wachezaji wote. Hadi sasa bado sijakaa chini na viongozi wa Yanga kuzungumzia suala la mkataba.
SWALI: Huoni kama kuna hatari ya wewe kuingia kwenye matatizo iwapo utatia saini fomu za usajili za klabu mbili?
JIBU: Siwezi kufanya hivyo kwa sababu najua sheria zinavyosema kuhusu jambo hilo. Nipo makini kukwepa matatizo ya aina hiyo. Nikifungiwa, maana yake ni kwamba ninahatarisha ajira yangu, ambayo ni kucheza soka.
SWALI: Iwapo klabu ya Yanga itakupa pesa kwa ajili ya kuongeza mkataba, utakuwa tayari kufanya hivyo? Na ni kiasi gani cha pesa, ambacho utataka ulipwe ili kumwaga wino Yanga?
JIBU: Kwa kweli siwezi kutaja kiwango cha fedha ninachotaka kulipwa na klabu yoyote, sio Yanga tu. Hiyo ni siri yangu. Lakini nitakuwa tayari kuendelea kuichezea Yanga iwapo watanilipa fedha ninazozihitaji, si vinginevyo.
SWALI: Kwa muda mrefu sasa umeondolewa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa tuhuma za utovu wa nidhamu. Umejifunza nini kutokana na tatizo hilo?
JIBU: Nimejifunza mambo mengi na kujua jinsi watu walivyo. Lakini jambo la msingi ni kwamba, bado nahitaji kulitumikia taifa langu muda wowote nitakapotakiwa kujiunga na timu hiyo.
SWALI: Una maoni gani kuhusu kumalizika kwa mkataba wa Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Marcio Maximo?
JIBU: Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Japokuwa sikuwa nikielewana na Maximo, lakini ametupa mafanikio makubwa, licha ya kuwepo kwa kasoro ndogo ndogo, ambazo mimi binafsi naziona ni za kibinadamu.
SWALI: Je, kuondoka kwa Maximo kunaweza kufungua milango kwako kurejea kwenye kikosi cha Taifa Stars?
JIBU: Hilo siwezi kulijibu kwa sababu mwamuzi wa kurejea kwangu kwenye kikosi hicho ni kocha mpya, aliyetangazwa hivi karibuni na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
SWALI: Je, una mipango yoyote ya kwenda kucheza soka ya kulipwa nje ya Tanzania?
JIBU: Ni kweli ni nina mpango wa kwenda Sweden. Nimepata timu huko, lakini bado kuna mambo madogo ninayaweka sawa, ikiwa ni pamoja na usajili na kujua hali ya wazazi wangu kwanza. Pia natarajia kukutana na Manji ili kujua hatma yangu msimu ujao.

No comments:

Post a Comment