KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

Huyu ndiye kocha mpya Taifa Stars


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limemtangaza Jan Borge Poulsen kuwa kocha mkuu mpya wa timu ya Taifa, Taifa Stars.
Poulsen (64) anatarajiwa kuanza kibarua hicho Agosti Mosi mwaka huu, akichukua nafasi ya kocha wa sasa, Marcio Maximo anayemaliza mkataba wake Julai 31 mwaka huu.
Katibu Mkuu wa TFF, Fredrick Mwakalebela aliwaambia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, Poulsen anatarajiwa kutia saini mkataba wa miaka miwili wa kuifundisha timu hiyo.
Uamuzi wa kumteua Poulsen kuwa kocha mkuu wa Taifa Stars ulifikiwa katika kikao cha kamati ya utendaji ya TFF kilichofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita.
Poulsen, ambaye ni kocha mkuu wa zamani wa timu ya taifa ya Denmark, aliwabwaga makocha wengine wanne kutoka nchi za Bulgaria, Poland, Serbia na Ureno.
Awali, jumla ya makocha 59 kutoka nchi mbalimbali duniani, wakiwemo wanne kutoka Tanzania, walituma maombi ya kazi hiyo kabla ya kuchujwa na kubaki watano.
Mwakalebela alimwelezea Poulsen kuwa ni kocha mwenye kiwango cha juu na pia mkufunzi wa makocha, anayetambuliwa na Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA).
Poulsen alizaliwa Machi 23, 1964. Alianza kucheza soka katika klabu ya vijana ya Store Heddinge BK kabla ya kujiunga na Ronne IK. Alianza kucheza soka ya wakubwa katika klabu ya Boldklubben Frem.
Mwanzoni mwa miaka ya 1980, aliteuliwa kuwa kocha wa klabu ya Boldklubben Frem na baadaye Koge Boldklub kabla ya kuteuliwa kuwa kocha msaidizi wa timu ya taifa ya Denmark, ambayo ilitwaa ubingwa wa Ulaya mwaka 1992.
Baada ya kushinda taji la Ulaya, aliteuliwa kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya vijana wa chini ya miaka 21. Aliifanyakazi hiyo hadi mwaka 1999, alipoteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Michezo wa timu ya taifa ya Singapore.
Wakati kocha Vincent Subramaniam wa Singapore alipotimuliwa mwaka 2001 kutokana na matokeo mabaya, Poulsen aliteuliwa kushika nafasi yake.
Hata hivyo, hakuweza kuiletea Singapore mafanikio yoyote. Naye alitimuliwa mwaka uliofuata na kurejea Denmark, ambako na kuendelea na kazi hiyo katika klabu mbalimbali.
Mwaka 2006, alifikia makubaliano na klabu ya Greve Fodbold ya kuwa kocha mpya wa timu hiyo, lakini wakati huo huo, akapata ofa ya kuwa kocha wa timu ya vijana wa chini ya miaka 20 na Jordan. Aliikubali ofa ya Jordam.
Januari mwaka 2008, Poulsen aliteuliwa kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Armenia. Machi 30 mwaka jana, alitemeshwa kibarua hicho na Shirikisho la Soka la Armenia.

No comments:

Post a Comment