KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 10, 2010

Narudi Simba-Chuji


KIUNGO Athumani Idd wa klabu ya Yanga amesema huenda akarejea katika klabu yake ya zamani ya Simba iwapo viongozi wake watashindwa kumalizana naye haraka.
Akizungumza na Burudani kwa njia ya simu jana, Chuji alisema amekuwa akifanya mawasiliano mara kwa mara na viongozi wa Simba ili arejee klabu hiyo msimu ujao wa ligi.
Chuji alisema amefikia uamuzi huo baada ya kumaliza mkataba wake wa miaka miwili wa kuichezea Yanga na kwamba kwa sasa yupo huru.
"Soka ndiyo ajira yangu, naona Yanga wapo kimya hadi sasa kuhusu mkataba mpya, lakini Simba wananisumbua mara kwa mara, kama watanipa dau kubwa, nitarudi,"alisema kiungo huyo wa zamani wa timu ya taifa, Taifa Stars.
Wakati Chuji akielezea msimamo wake huo, Mfadhili mkuu wa Yanga, Yusuf Manji mwishoni mwa wiki iliyopita alitoa orodha ya wachezaji wenye mkataba na klabu hiyo. Wachezaji hao ni Nurdin Bakari, Athumani Idd, Shamte Ally, Jerson Tegete, Idd Mbaga na Ally Msigwa.
Manji alikaririwa akisema kuwa, ametenga kitita cha sh. milioni 108 kwa ajili ya kuwalipa wachezaji wa ndani na nje ili waweze kuichezea timu hiyo msimu ujao.
Wachezaji, ambao mfadhili huyo atalazimika kuwalipa fedha zingine ili waendelee kuichezea timu hiyo ni kipa Yaw Berko kutoka Ghana, Fred Mbuna, Steven Marashi na beki Wisdom Ndhlovu kutoka Malawi.
Wengine ni Bakari Mbegu, Shadrack Nsajigwa, Godfrey Bonny, Kigi Makasi, John Njoroge, Nadir 'Cannavaro' Haroub na Abdi Kassim.
Wakati huo huo, Chuji amesema kipigo ilichokipata Taifa Stars katika mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya Brazil kilichangiwa na wachezaji kuchoka.
Chuji alisema kutokana na kukabiliwa na mechi mbili ndani ya saa 24, wachezaji wengi walichoka na kushindwa kucheza katika kiwango chao cha kawaida.
“Timu yoyote, ambayo ingekutana na Brazil katika mazingira kama hayo, lazima ingekumbana na kipigo kama hicho,”alisema mchezaji huyo aliyetemwa kwenye kikosi hicho na Kocha Marcio Maximo kwa tuhuma za utovu wa nidhamu.
Kabla ya kucheza na Brazil, Stars ilipambana na Rwanda na kufungwa bao 1-0 katika mechi ya marudiano ya raundi ya pili ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN).

No comments:

Post a Comment