KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 25, 2017

MO FLAVOUR, MSANII ALIYEPANIA KUITANGAZA TANZANIA KIMATAIFA



Na Mwandishi Wetu
KWA umri, msanii Mohamed Ngwenje, maarufu kwa jina la Mo Flavour, bado ni mdogo. Ndio kwanza amefikisha umri  wa miaka 19, ikiwa ni miaka michache baada ya kumaliza elimu ya sekondari katika shule ya Uwanja wa Taifa, iliyoko mkoani Morogoro.
Pamoja na umri wake huo mdogo na pia kuwa na miaka michache tangu alipojitosa katika fani ya muziki wa kizazi kipya, msanii huyo ameshafanya mambo makubwa mawili.
Kwanza amesharekodi nyimbo mbili, Usibeti aliouimba peke yake na Kusudi, ambao ameuimba kwa kushirikiana na wanamuziki nyota wawili nchini, Jose Mara na Khalid Chuma ‘Chokoraa’.
Wimbo wake wa Usibeti ndio uliomtambulisha katika anga za muziki huo wa kizazi kipya na ndio uliomwezesha kukutana na Jose Mara na Chokoraa na hatimaye kukubali kurekodi naye wimbo wa Kusudi.
Tayari Mo Flavour ameshaurekodi wimbo wa Usibeti kwenye video na audio na kwa sasa anafanya mipango ya kurekodi video ya wimbo wa Kusudi, baada ya kukamilisha kazi ya kurekodi audio.
Mo Flavour amerekodi nyimbo hizo kwenye studio za Moro Town Records ya Morogoro na Amoroso Sound ya Dar es Salaam, ambayo ilitumika kuchanganya ala za muziki kitaalamu zaidi.
Kwa mujibu wa msanii huyo chipukizi, alifanikiwa kurekodi nyimbo hizo kwa udhamini wa baba yake mzazi, Ngwenje Mohamed, ambaye pia amekuwa akimtumia kama meneja wake.
“Kwa sasa baba ndiye kila kitu kwangu katika masuala ya muziki, lakini lengo langu kubwa huko mbele ni kuwa na meneja wa uhakika kwa ajili ya kusimamia kazi zangu,”alisema Mo Flavour, alipozungumza na Uhuru, hivi karibuni mjini Dar es Salaam.
Msanii huyo, ambaye kwa sasa anachukua masomo ya kompyuta katika Chuo cha Royal, kilichoko Ubungo, Dar es Salaam, alisema anamshukuru Mungu kwamba, nyimbo zake zote mbili zimepokelewa vizuri na mashabiki wa muziki wa kizazi kipya.
Alisema kupokelewa vizuri kwa nyimbo hizo, kulijidhihiridha wakati wa utambulisho wa kibao chake cha kwanza cha Usibeti, alioufanya mwaka jana, kwenye ukumbi wa Jahazi Garden, mjini Morogoro.
Kwa mujibu wa Mo Flavour, alifanya onyesho hilo la uzinduzi kwa udhamini wa baba yake na kuongeza kuwa, lilihudhuriwa na mashabiki lukuki.
“Hata mapato niliyoyapata yalikuwa mazuri na ndiyo yaliyoniwezesha kupata fedha za kurekodi wimbo wangu uliofuata wa Kusudi,”alisema Mo Flavour.
Mbali na mafanikio hayo, alisema amekuwa akipata mialiko mingi ya kufanya maonyesho mbalimbali ya muziki huo kwa kushirikiana na baadhi ya wasanii maarufu nchini.
“Jambo la kufurahisha ni kwamba, nimeanza kupokea mialiko kutoka hata katika nchi jirani za Uganda na Kenya. Hii inadhihirisha kwamba, kazi zangu zinakubalika,”alisema.
Akizungumzia hali ya muziki huo nchini, Mo Flavour alisema ni nzuri na ya kuridhisha kutokana na mafanikio yaliyofikiwa na wasanii wengi wa fani hiyo.
Hata hivyo, alikiri kuwa kikwazo kikubwa kwa wasanii wanaochipukia ni kukosa promosheni kwa vile mapromota wanapenda zaidi kuwasaidia wasanii waliokwishapata umaarufu, badala ya wale wanaochipukia.
“Unaweza kutunga nyimbo nzuri na kali, ikapendwa na mashabiki, lakini ikakosa mtu wa kuitangaza. Hali hii imekuwa ikisababisha wasanii wengi wanaochipukia kukata tamaa mapema,”alisema.
Msanii huyo amesema anamshukuru Mungu kwa kupata uungwaji mkono wa kiwango kikubwa kila alipotembelea vituo mbalimbali vya redio na televisheni nchini. Alisema hali hiyo imekuwa ikimtia moyo na kumfanya ajitume zaidi.
“Japokuwa kumekuwa na malalamiko ya watangazaji wa redio na televisheni kubania kazi za wasanii, kwangu mimi hali ni tofauti. Kila ninapopeleka kazi zangu kwenye vituo vya redio na televisheni, zimekuwa zikikubalika. Sikuwahi kuombwa rushwa,”alisema.
Msanii huyo pia amesema anaunga mkono uwepo wa sheria ya hatimiliki nchini, ambayo inamwezesha msanii kulipwa kila kazi yake inapotumika kwenye vituo vya redio na televisheni.
Amesema kazi ya muziki ni biashara, vivyo hivyo vituo vya redio na televisheni navyo vimekuwa vikifanya biashara, hivyo vinapotumia kazi za wasanii, havina budi kuwalipa.
Mo Flavour amesema binafsi anavutiwa na wasanii wote wa kizazi kipya nchini kwa kuwa kila mmoja anajitahidi kufanya vizuri ili aweze kupata mafanikio.
Ameyataja malengo yake katika siku zijazo kuwa ni pamoja na kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia muziki huo na pia kuwa mwanamuziki wa kimataifa.
Amewataka wasanii wa muziki huo wawe makini katika kazi yao, hasa wanapobahatika kupata udhamini kutoka kwenye kampuni na watu binafsi.
“Nawashauri wasanii wenzangu unapopata msaada wa udhamini, jitume. Huwezi kuendelea kusaidiwa kama hufanyi jambo la maana,”alisema.
Pia, aliwataka wasanii wa muziki huo kuacha tabia ya kujikweza na kujiona wapo matawi ya juu pale wanapoanza kupata mafanikio. Alisema kufanya hivyo kunawakera mashabiki na kutasababisha waporomoke mapema kimuziki.
0000000


















No comments:

Post a Comment