KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, October 21, 2012

SERENGETI BOYS YAINGIA KAMBINI



KIKOSI cha wachezaji 25 wa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys kimeingia kambini leo mjini Dar es Salaam kujiandaa kwa mechi ya raundi ya mwisho ya michuano ya Afrika kwa vijana.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura amesema leo kuwa, Serengeti Boys ambayo iko chini ya Kocha Mdenmark, Jakob Michelsen, itacheza mechi hiyo ya raundi ya tatu na mshindi kati ya Congo Brazzaville na Zimbabwe ambapo tayari Congo Brazzaville imefanikiwa kupata ushindi wa ugenini wa mabao 2-1. Mechi ya marudiano itachezwa jijini Brazzaville kati ya Oktoba 26-28 mwaka huu.
Katika mechi hiyo ya raundi ya tatu, Serengeti Boys itaanzia nyumbani katika mchezo utakaofanyika Novemba 17, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, wakati mechi ya marudiano itachezwa wiki mbili baadaye.
Wambura amesema TFF ipo katika mikakati ya kuhakikisha Serengeti Boys inapata mechi mbili za kirafiki za kimataifa kabla ya kumvaa mshindi kati ya Congo Brazzaville na Zimbabwe. Fainali za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 zitafanyika Machi mwakani nchini Morocco.
Tanzania imefuzu bila jasho hadi kufika hatua hiyo, baada ya wapinzani wake wa awali, Kenya na Misri kujitoa katika Raundi ya Kwanza na ya Pili.Kama Tanzania itafuzu kushiriki Fainali hizo za mwakani, itapoza machungu ya mwaka 2005 walipofuzu kucheza Fainali za Vijana wa umri huo kwa kuzitoa Rwanda, Zambia na Zimbabwe, lakini baadaye kwa sababu ya ‘kufoji’ umri wa Nurdin Bakari, ikaondolewa mashindanoni.
Zaidi ya Fainali za Mataifa ya Afrika 1980 na CHAN 2009, katika soka ya wanaume, Tanzania haijashiriki fainali nyingine zozote za Afrika tangu iingie kwenye soka ya kimataifa.

No comments:

Post a Comment