KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, May 11, 2015

WANAMUZIKI WA TANZANIA WANAKOSA UBUNIFU-BELLA




MWIMBAJI nyota wa muziki wa dansi nchini na kiongozi wa bendi ya  Malaika, Christian Bella, amesema sababu kubwa inayowafanya wanamuziki wa Tanzania kushindwa kupata mafanikio kimataifa ni kukosa ubunifu.
Bella amesema wanamuziki wa Tanzania wanashindwa kwenda na wakati na kwa miaka mingi sasa wamekuwa wakipiga muziki uleule, bila kuubadili na kuweka vionjo vipya.
“Wanamuziki wa Tanzania hawataki kwenda na wakati, wanakosa ubunifu. Wanataka kupiga muziki ule ule wa miaka ya 80,”amesema.
Bella, ambaye nyimbo zake nyingi zimetokea kugusa hisia za mashabiki wa muziki nchini, alisema hayo wiki hii, alipokuwa akizungumzia maendeleo yake kimuziki na hali ya muziki nchini.
Amesema licha ya kumiliki bendi ya Malaika, amekuwa akirekodi nyimbo zake binafsi kwa lengo la kujitangaza na kukuza kipaji chake.
“Bendi ni yangu, lakini haiwezi kuimarika bila mimi kujitangaza,”amesema mwanamuziki huyo mwenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).
Amesema uamuzi wake huo hauna maana kwamba anaidharau bendi hiyo au kuitelekeza, bali amepania kula sahani moja na wakali wa muziki wa bongo fleva kama Ali Kiba na Naseeb Abdul ‘Diamond.
Amesema nyimbo zake zimekuwa zikipendwa na mashabiki wengi wa muziki nchini kutokana na kuwa na mashairi yenye mvuto na pia kuweka vionjo vipya mara kwa mara.
“Naimba na kupiga nyimbo zangu kwa kuchanganya aina tofauti ya muziki. Nachanganya bongo fleva, dansi na pia naangalia wenzangu wanafanya nini,”amesema Bella, ambaye aliwahi kuwa kiongozi wa bendi ya Akudo Impact.
“Hakuna kipya katika muziki, aina zote za muziki zinazopigwa sasa, zilishawahi kupigwa miaka ya nyuma.
“Hata Koffi Olomide na Fally Ipupa wanaiga vionjo vya muziki vya Kitanzania. Katika muziki, hakuna kitu kinachoitwa kuiga muziki wa bendi au mwanamuziki fulani,”amesema mwanamuziki huyo, ambaye amekuwa na ushirikiano mkubwa na wasanii wa bongo fleva.
Bella amekiri kuwa binafsi anavutiwa na muziki wa kizazi kipya kutokana na ukweli kwamba wasanii wake ni wabunifu na amekuwa akipata vitu vingi kutoka kwao.
Mwimbaji huyo mwenye sauti yenye mvuto, inayopanda na kushuka mithili ya mawimbi baharini, amesema baadhi ya wanamuziki wa Tanzania hawapendi maendeleo ya wenzao na wamekuwa wakipenda kufuatilia maisha na kazi za wenzao.
“Wapo wanaoweza kukufuatilia kila siku kutaka kujua umefanya nini. Hata ukifanya kitu kizuri, utaona wanakukosoa, lakini ukiwaambia waingie studio kurekodi, hawawezi,”amesema.
Bella amesema wakati alipoanzisha bendi ya Malaika, baadhi ya wanamuziki walimponda na kumtabiria kwamba haiwezi kufika mbali, lakini alijipa moyo.
“Ningekuwa na moyo dhaifu, ningekata tamaa mapema, lakini nilijipa moyo kwamba nitafanikiwa, na kweli nimefanikiwa kwani bendi ipo juu kuliko zile zilizoanzishwa miaka mingi,”amesema.
Amekanusha madai kuwa, amekuwa akiwabania wanamuziki wenzake katika bendi ili wasipate umaarufu. Lakini amekiri kuwa msimamo wake ni kwamba haiwezekani bendi ikawa na mastaa kibao. Amesisitiza kuwa staa katika bendi huwa ni mmoja.
“Kila mtu anataka kuwa staa, hilo haliwezekani. Mwanamuziki anaweza kuwa na nyimbo alfu moja kwenye kabati, lakini hakuna hata moja iliyowahi kushika chati. Lazima wanamuziki watofautiane,”amesisitiza.
“Kama ni kweli nimekuwa nikiwabania wanamuziki wenzangu, mbona baada ya kuondoka Akudo Impact, bendi imeshindwa kuendelea. Kwa nini wale waliobaki wameshindwa kuiendeleza na kutumia nafasi ya kuondoka kwangu kuonyesha vipaji vyao?” Alihoji.
Bella amesema katika bendi yake ya Malaika, hatoi ruhusa kwa kila mwanamuziki kurekodi nyimbo zake binafsi kwa vile kufanya hivyo kutaidhoofisha bendi.
Amesema kama suala ni kutaka kupata umaarufu, amekuwa akiwaachia wanamuziki wake saa tatu kila wanapofanya maonyesho, kupiga nyimbo za utangulizi ili kuonyesha makali yao kabla ya yeye kupanda stejini.
“Huwa tunaanza maonyesho yetu saa tatu usiku. Nawaacha wanaimba kwa saa tatu, mimi naimba kuanzia saa sita usiku,” amesema.
“Umaarufu unaanzia kwenye maonyesho, sio kwenye TV. Wale mashabiki wanaoingia ukumbini tangu saa mbili usiku ndio wanaokupa umaarufu,”amesema.
Bella amesema kwa sasa anajiandaa kwa safari ya kwenda Ufaransa kwa ajili ya kuingia mkataba na promota mmoja maarufu wa wanamuziki kutoka DRC ili kurekodi nyimbo zake katika sura ya kimataifa na kujitangaza zaidi duniani.
Hata hivyo, hakuwa tayari kutaja jina la promota huyo na pia kueleza lini anatarajia kwenda safari hiyo.

No comments:

Post a Comment