KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 13, 2013

DIAMOND, WEMA WAKUTANISHWA KWENYE FILAMU


Waandaaji wavunja benki kuwalipa washiriki
Diamond akiri itakuwa kazi ngumu kuliko muziki

LICHA ya kuvunjika kwa uhusiano wao wa kimapenzi, msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Naseeb Abdul 'Diamond' na msanii nyota wa filamu, Wema Sepetu watakutanishwa katika filamu.

Wapenzi hao wawili, ambao wamekuwa wakirudiana na kuachana mara kwa mara, wanatarajiwa kucheza filamu mpya itakayoanza kurekodiwa hivi karibuni.

Akihojiwa katika kipindi cha Take One Action kilichorushwa hewani hivi karibuni na kituo cha televisheni cha Clouds, Diamond alisema amelipwa pesa nyingi kwa ajili ya kucheza filamu hiyo.

Diamond alisema hakuna msanii wa filamu aliyewahi kulipwa kiwango hicho cha pesa na kwamba hata yeye hajawahi kulipwa pesa kama hizo katika kazi yake ya muziki.

Hata hivyo, Diamond hakuwa tayari kutaja kiwango hicho cha pesa kwa madai kuwa, taarifa zaidi zitatolewa na waandaaji wa filamu hiyo hivi karibuni.

"Taarifa kuhusu filamu hiyo inahusu nini, lini tutaanza kufanya 'shooting', washiriki wamelipwa kiasi gani cha pesa na picha zake zitachukuliwa maeneo gani, itatolewa na waandaaji,"alisema

Msanii huyo nguli wa muziki wa kizazi kipya alisema anaamini filamu hiyo itakuwa babu kubwa kutokana na maelezo aliyopewa na waandaaji wake.

 "Haitakuwa kama hizi filamu zilizozoeleka,"alisema msanii huyo, ambaye amewahi kushinda tuzo kadhaa za muziki za Kilimanjaro.

Diamond alisema amewahi kuombwa na watu mbalimbali kucheza filamu zao, lakini amekuwa akiwatolea nje kutokana na kutoridhishwa na maudhui yake na mazingira ya uandaaji wake.

Alisema lengo lake ni kuifanya filamu hiyo atakayoicheza kwa kushirikiana na Wema, iwe katika kiwango cha juu ili aweze kuuza jina lake kimataifa.

Licha ya kukubali kucheza filamu hiyo, Diamond alisema anahisi kutatokea matukio mengi ya ajabu wakati wa kupiga picha za filamu hiyo katika maeneo husika.

"Nina hakika baadhi ya wakati mpenzi wangu atakuwa akija kwenye maeneo ya kupiga picha za filamu hiyo kila atakapopata nafasi, hivyo kutakuwa na vijembe na maneno ya hapa na pale,"alisema.

"Hii kazi nahisi itakuwa ngumu kuliko hata ya muziki, lakini namuomba Mungu anisaidie ili niweze kuimaliza salama,"aliongeza msanii huyo.

Japokuwa hakutaka kuweka wazi kuhusu wasiwasi alionao wa kutokea matukio ya ajabu wakati wa upigaji wa picha za filamu hiyo, kauli yake hiyo inamuhusisha Wema na mpenzi wake wa sasa, Penny.

Diamond ana wasiwasi kuwa, iwapo Penny atakuwa akimtembelea katika maeneo watakayokuwa wakipiga picha za filamu hiyo, huenda akakwaruzana na Wema na kurushiana vijembe.

"Si unajua kila mtu analinda chake. Nina hakika yataripotiwa mambo mengi wakati wa kupiga picha za filamu hiyo,"alisema.

Alipoulizwa ni msanii yupi wa filamu wa kike anayevutiwa naye, Diamond hakusita kumtaja Wema.

"Napenda sana uigizaji wa Wema, si kwa sababu alikuwa mpenzi wangu. Waswahili wanasema palipo na ukweli, hakuna haja ya kuficha mambo. Wema anaigiza vizuri sana,"alisema.

Kwa upande wa wacheza filamu wa kiume, Diamond alimtaja msanii anayemvutia kuwa ni Jacob Steven, maarufu kwa jina la JB.

Diamond amewataka watanzania kujenga tabia ya kuwasamehe wasanii pale wanapoteleza na kufanya matendo mabaya mbele ya jamii. Alisema inasikitisha kuona kuwa, matendo mabaya yanavuma zaidi kuliko mazuri.

"Mimi kama Diamond nimekuwa nikifanya mambo mengi mazuri, lakini hayaonekani. Lakini inapotokea nimefanya kitu kidogo chenye mwonekano mbaya, kinakuzwa sana,"alisema.

No comments:

Post a Comment