KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 14, 2010

'Wasanii wa kiume wanawadhalilisha wenzao wa kike'


KIONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Twanga Pepeta International, Luiza Mbutu amedai kuwa, wasanii wa kiume wamekuwa chanzo kikubwa cha kudhalilishwa kwa wenzao wa kike nchini.
Luiza alitoa madai hayo wiki hii katika semina ya Jukwaa la Sanaa, iliyofanyika mwanzoni mwa wiki hii kwenye ukumbi wa ofisi za Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Ilala, Sharrifu Shamba, Dar es Salaam.
Alisema hali hiyo imekuwa ikisababisha wasanii wa kike, hasa wacheza shoo wa bendi mbalimbali, waonekane hawana maadili mema katika jamii na washutumiwe kwa kuwadhalilisha wanawake wenzao.
Luiza alisema hali imekuwa mbaya kiasi kwamba wasanii wa kike wamejikuta wakifanya mambo kinyume cha maadili ili kukidhi matakwa ya wasanii wa kiume na baadhi ya wapenzi wa muziki wa dansi hapa nchini.
Akitoa mfano wa udhalilishaji huo, Luiza alizungumzia tabia chafu ya wapenzi wa muziki wa dansi kuwatuza fedha wanenguaji wa kike wawapo kwenye maonyesho kwa kuwawekea kwenye matiti yao au makalio, kitendo alichokiita kuwa ni cha kidhalilishaji.
“Wanenguaji wa kiume wamekuwa wakituzwa fedha kwa kupewa mikononi au mifukoni, lakini wale wa kike wamekuwa wakiwekewa kwenye matiti na makalio, kitu ambacho kimekuwa ni cha kiudhalilishaji sana,” alilalamika Luiza.
Aliitaja pia tabia ya wanamuziki wa kiume kwenye bendi kuponda mawazo ya wenzao wa kike, hasa wanapotaka kutunga nyimbo, hali ambayo imekuwa ikisababisha wawe wakipitisha nyimbo zao pekee na kuwaacha nyuma wanawake kimaendeleo.
Kiongozi huyo wa Twanga Pepeta pia alilalamikia baadhi ya wazazi, ambao wamekuwa wakiwakataza watoto wao wa kike kushiriki kwenye shughuli za sanaa, hivyo kuwafanya wawe wakitoroka usiku wa manane na kushindwa kurudi majumbani baada ya kuomba hifadhi kwa wanaume na hivyo kuishia kupata mimba zisizotarajiwa na watoto wa mitaani.
Wakichangia mada ya udhalilishaji, baadhi ya wachangiaji walilalamikia vitendo vya rushwa ya ngono, ambavyo walidai kuwa vimekuwa vimekithiri na kuwadhalilisha wasanii wa kike.
Walisema wasanii wengi wa kike kila wanapohojiwa na vyombo vya habari, wamekuwa wakilalamikia rushwa ya ngono, wanazoombwa na wenzao wa kiume waliokwishapata umaarufu nchini pamoja na wakuzaji wa muziki.

No comments:

Post a Comment