KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, August 22, 2015

TAIFA STARS KWENDA UTURUKI JUMAMOSI



Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inatarajiwa kuondoka nchini siku ya jumamosi usiku kuelekea Muscat Oman, kucheza mchezo wa kirafiki kabla ya kuunganisha kuelekea Istambul Uturuki kwa kambi ya wiki moja.

Taifa Stars imepata mwaliko wa kucheza mchezo wa kirafiki na timu ya Taifa ya Oman tarehe 24 Agosti, 2015 usiku, ambapo baada ya mchezo huo timu itasafiri kuelekea nchini Uturuki katika jiji la Istambul.

Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini Oman (OFA) liliomba kucheza mchezo wa kirafiki na Taifa Star kabla ya kuwavaa Turkemebistan katika mchezo wa kuwania kufuzu kwa Kombe la Dunia Septemba 03, 2015 kwa bara la Asia, ambapo kocha wake mkuu Mfaransa Paul Leguen aliomba kucheza na vijana wa Charles Mkwasa kujiandaa na mechi hiyo.

Mara baada ya mchezo huo Taifa Stars itaelekea Istambul katika mji wa Kocael hoteli ya Kartepe kwa kambi ya wiki moja, ikiwa nchini Uturuki Stars inatarajiwa kucheza michezo miwili ya kirafiki kabla ya kurejea nchini kucheza na Nigeria Septemba 05, 2015 mchezo wa kuwania kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika.

Kocha mkuu wa Taifa Stars, Charles Mkwasa anatarajiwa kutoa orodha ya kikosi chake cha wachezaji 22 mwishono mwa wiki watakaosafiri kuelekea nchini Uturuki kwa kambi ya hiyo ya kujiandaa na mchezo dhidi ya Nigeria.

Mshambuliaji Adi Yussuf anayechezea klabu ya Mansfield Towny ya Uingereza alitarajiwa kujiunga na timu nchini Uturuki, lakini kutokana na majeruhi aliyoyapata hivi karibuni katika michezo ya ligi, uongozi wa Mansfield umeomba mchezaji huyo kutojiunga na timu ya Taifa kwa ajili ya kupata mataibabu zaidi.

Adi aliumia wiki iliyopita katika mchezo dhidi ya Nottingham Forest ambapo kwa sasa anaendelea na matibabu chini ya uangalizi wa klabu hiyo, na pindi atapokuwa fit atapata nafasi ya kujumuika na kuitumika timu ya Taifa ya Tanzania.

Sunday, August 16, 2015

SIMBA YAWAPA RAHA MASHABIKI WAKE, YAITUNGUA URA 2-1



Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM

BAO la dakika ya 82 la beki wa kimataifa wa Uganda, Juuko Murushid limeipa Simba SC ushindi wa 2-1 dhidi ya URA ya Uganda katika mchezo wa kirafiki jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Beki huyo ‘mbishi’ alifunga bao hilo kwa guu lake la kushoto baada ya kuuwahi mpira ulioparazwa na kipa Brian Bwete kufuatia kona maridadi iliyochongwa na kiungo Mwinyi Kazimoto Mwitula.

Katika mchezo huo uliochezeshwa na Refa Israel Mujuni wa Dar es Salaam, Simba SC ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa mshambuliaji wake mpya, Kelvin Ndayisenga dakika ya nne aliyemalizia krosi ya Mrundi mwenzake, Emery Nimubona.

Juuko Murushid (kulia) akishangilia mbele ya mashabiki wa Yanga na Ibrahim Hajib baada ya kuifungia Simba SC bao la ushindi

Hata hivyo, bao hilo halikudumu sana, kwani URA walisawazisha dakika ya 20 kupitia kwa Frank Kalanda, aliyefumua shuti la juu lililompita kiulaini kipa, Peter Manyika.

Kipindi cha pili, timu zote zilifanya mabadiliko na mchezo ukazidi kuwa mtamu kutokana na mashambulizi na kosakosa za pande zote mbili.

Wachezaji Peter Mwalyanzi wa Simba SC na Jimmy Kulaba wa URA waligongana wakati wakigombea mpira wa juu na wote kushindwa kuendelea na mchezo, wakipelekwa katika zahanati ndoto ya uwanjani hapo kupatiwa huduma ya kwanza.

URA walimuingiza Deo Otieno baada ya kutoka Jimmy Kulaba wakati Simba SC ilimalizia mchezo pungufu kutokana na kuwa imemaliza wachezaji wa kubadili.

Huo unakuwa mchezo wa saba mfululizo wa kirafiki, Simba SC inashinda chini ya kocha wake mpya,
Muingereza Dylan Kerr, baada ya awali kuzifunga 2-1 Kombaini ya Zanzibar, 4-0 Black Sailor, 2-0 Polisi, 3-0 Jang’ombe Boys, 3-2 KMKM zote za Zanzibar na 1-0 SC Villa ya Uganda.

Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Peter Manyika, Emery Nimubona/Hassan Kessy dk46, Samih Haji Nuhu/Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ dk46, Juuko Murudhid, Said Issa/Hassan Isihaka dk46, Abdul Banda/Justuce Majabvi dk46, Simon Sserunkuma/Peter Mwalyanzi dk46/, Awadh Juma/Said Ndemla dk46, Kevin Ndayisenga/ Ibrahim Hajib dk67, Danny Lyanga/Mussa Mgosi dk68 na Issa Abdallah/Mwinyi Kazimoto dk46.

URA: Bwete Brian, Massa Simon, Sekito Sam, Samuel Senkoom, Kasozi Bob, Agaba Oscar, Kagimi Sadiq/ El Kanah Mkugwa dk67, Kyeyune Said, Oniamucha Villa, Kalanda Frank/Ronald Kigonyo dk72 na Lutimba Yayo/Jimmy Kulaba dk51/Deo Otieno dk72.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BINZUBEIRY

TFF YAIRUHUSU DRFA KUENDELEA NA UCHAGUZI WA TEFA



Shirikisho la mpira wa miguu nchini Tff imekiruhusu chama cha soka mkoa wa Dar es salaam DRFA kuendelea na mchakato wa uchaguzi wa viongozi wa chama cha soka wilaya ya Temeke (TEFA) kama ulivyopangwa na kamati ya uchaguzi ya  chama hicho.

Baada ya ruhusa hiyo Uongozi wa DRFA umemuandikia barua katibu wa TEFA Kasim Mustapha ili aijulishe kamati ya uchaguzi ya chama hicho kuendelea na mchakato huo kama kawaida.

Awali TFF iliiandikia barua DRFA kushauri kusimamishwa kwa uchaguzi huo,kutokana na kile kinachoonekana kuwepo na malalamiko kuhusu mchakato wake lakini maada ya mashauriano kati ya pande hizo mbili,sasa ni ruksa kwa uchaguzi huo kufanyika kesho jumapili Agosti 16,2015 kama ulivyopangwa.

Aidha DRFA imewaomba wapiga kura wote kujitokeza kwenye uchaguzi,huku ikisisitiza amani na utulivu itawale katika zoezi hilo muhimu la kuwapata viongozi watakaokiongoza chama cha soka Temeke,ili kuleta maendeleo ya mpira wa miguu mkoa wa Dar es salaam

TWIGA STARS YAENDELEA KUJIFUA ZANZIBAR


Kikosi cha timu ya Taifa ya Wanawake (Twiga Stars) kilichoweka kambi kisiwani Zanzibar, kujiandaa na fainali za Michezo ya Afrika (All Africa Games) kimeendelea kujifua kutwa mara mbili katika viwanja wa Aman na Fuoni kabla ya safari ya kuelekea nchini Congo – Brazzavile mwezi ujao.

Twiga Stars chini ya kocha mkuu Rogasian Kaijage inatarajiwa kucheza mchezo wa kirafiki na timu ya Taifa ya Kenya (Harambee Starlets) Agosti 23  katika uwanja wa Amani kisiwani Zanzibari ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya michezo ya hiyo ya Afrika (All Africa Games).

Kaijage amesema anashukru vijana wake wanafanya mazoezi kwa morali ya hali ya juu, wachezaji wanaonekana kuyashika vizuri mafunzo yake na kumpa imani kuwa sasa kikosi chake kimeiva na anachosubiri ni mchezo wa kirafiki dhidi ya Kenya ili kuweza kuona uwezo wa kikosi chake kabla ya safari ya kuelekea nchini Congo-Brazzavile.

Akiongeleaa maendeleo ya kambi ya Twiga Stars, Mkuu wa Msafara Blassy Kiondo amesema timu ipo katika hali nzuri, wachezaji wanafanya mazoezi  kwa morali ya hali ya juu, hakuna majeruhi kikubwa wanachosubiri kwa sasa ni huo mchezo wa kirafiki dhidi ya Kenya mwishoni mwa wiki ijayo.

MALINZI AMPONGEZA  NDIKURIYO
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), Jamal Malinzi ametuma salamu za pongezi kwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini Burundi (FBF) Reverien Ndikuriyo kwa kuchaguliwa kuwa spika wa bunge la Seneta nchini humo.

Katika salam hizo za pongezi kwa Rais wa FBF na nakala zake kwenda CECAFA, CAF na FIFA, Malinzi ameelezea imani yake kwa Seneta Ndikuriyo na amemtakia kila la kheri na mafanikio katika nafasi hiyo mpya aliyochaguliwa.

Thursday, August 13, 2015

VIGOGO WAPIGWA CHINI UCHAGUZI WA TEFA



MAAMUZI YA KAMATI YA UCHAGUZI YA DRFA KUHUSU RUFANI ZA WAGOMBEA WA NAFASI MBALIMBALI  ZA UONGOZI WA CHAMA CHA SOKA WILAYA YA TEMEKE (TEFA) KUPINGA MAAMUZI YA KAMATI YA  UCHAGUZI YA TEFA.      ZILIZOSIKILIZWA TAREHE 10/08/2015 KATIKA  HOTELI YA PR TEMEKE.

WAJUMBE WALIOHUDHURIA NI:
1.      RASHID SAADALLAH-MWENYEKITI
2.      FAHAD F.A. KAYUGA-KATIBU
3.      JUMA PINTO-MJUMBE
4.      HAJI BECHINA-MJUMBE


 1. RASHID SALIM-NAFASI YA MWENYEKITI WA TEFA
-Kashindwa kuleta vielelezo kuthibitisha uzoefu wake katika masuala ya mpira kama Ibara ya 31(1)(j) inavyosema,  alidai kuwa amekuwa kiongozi wa Tandika FC kwa muda wa miaka saba lakini hukuweza kuthibitisha maelezo yake kwa vielelezo. Kwa hivyo kamati inakubaliana na maamuzi ya kumuengua ya kamati ya uchaguzi TEFA.



 2. PETER STEPHEN MUHUNZI-NAFASI YA MWENYEKITI WA TEFA
-Kathibitisha kigezo cha elimu kwa maana ya kumaliza kidato cha nne ingawa kuna pingamizi la matumizi mabaya ya fedha na ubadhirifu, haya kamati yangu haina mamlaka ya kuyatolea maamuzi hivyo yanapelekwa kwenye kamati ya maadili ya DRFA.

   3. AZIZ MOHAMED KHALFAN-NAFASI YA MWENYEKITI WA TEFA
 -kamati imegundua kwamba alienda kwenye mchakato wa uchaguzi akiwa hana sifa kwa sababu alifungiwa na kamati ya nidhamu na usuluhishi ya kutokushiriki au kujihusisha na mpira kwa muda wa miezi kumi na mbili (12) na TEFA hata hivyo hakukata rufaa juu ya kifungo hicho na badala yake alikwenda kupeleka malalamiko yake TFF. Kiutaratibu baada ya kufungiwa na kamati tajwa alipaswa akate rufaa katika kamati ya rufaa ya TEFA, na kama asingeridhika na maamuzi ya kamati ya rufaa ya TEFA ndiyo angeweza kukata rufaa katika kamati ya uchaguzi ya DRFA. Kwa maana hiyo kamati inamuengua kwa sababu rufaa yake imeshindwa kuzingatia kanuni na taratibu za kukata rufaa.
       
4. SIZZA CHENJA-NAFASI YA MWENYEKITI WA TEFA
-kamati imempitisha aendelee na mchakato wa uchaguzi baada ya kuthibitisha kuwa ana uzoefu wa kutosha katika uongozi wa mpira wa miguu kama katiba ya TEFA Ibara ya (31)(1)(j) inavyotaka. Kwani mnamo mwaka 2009 alikua kiongozi katika klabu ya soka ya Tp Vita vilevile ameweza kushiriki ugombea katika nafasi ya ujumbe wa kamati ya utendaji wa DRFA katika vipindi tofauti ikiwemo mwaka 2012 ambapo alishindwa kupata nafasi hiyo.

5. OMARY. A. KAPILIMA-NAFASI YA MAKAMU YA KWANZA WA  MWENYEKITI
-kaweza kuthibitisha uzoefu wa uongozi wa mpira lakini kashindwa kuleta cheti cha kidato cha nne kinachotambulika na Baraza la Mitihani la Taifa yaani (NECTA). Hivyo maamuzi ni kuwa kashindwa kukidhi kigezo cha elimu kama inavyotakiwa na Ibara ya 31(1)(b) ya katiba ya TEFA.

 6. SALEHE MOHAMED SALEHE-NAFASI YA MAKAMU WA KWANZA WA MWENYEKITI
Kamati inamuengua katika mchakato wa uchaguzi kwa kushindwa kuthibitisha kiwango chake cha elimu kwa  kushindwa kuleta cheti cha kidato cha nne(Academic Certificate) kama inavyotakiwa na Ibara ya 31(1)(b) ya katiba ya TEFA. Pia  kulikuwa na madai ya ubadhirifu wa fedha na kuuza timu ya Tesema FC akiwa kama makamu wa kwanza wa mwenyekiti wa TEFA, haya kamati inayapeleka katika kamati ya maadili ya DRFA kwa ufafanuzi na maamuzi.

7. SHUFAA JUMANNE- NAFASI YA MAKAMU WA KWANZA WA MWENYEKITI
-Kamati inampitisha aendelee na mchakato wa uchaguzi baada ya kuridhika na uthibitisho wa uzoefu wa zaidi ya miaka mitatu katika uongozi wa soka. Ameweza kuithibitishia  kamati kwa vielelezo kuwa amekuwa kiongozi wa Tale FC kwa zaidi ya miaka mitatu. Vilevile ameleta vielelezo kuthibitisha kuwa Tale FC ni mwanachama hai wa TEFA kinyume na madai ya mpingaji.

8. DAUDI FRANCIS MUMBULI-NAFASI YA MAKAMU WA KWANZA WA MWENYEKITI
-Kamati inaitupilia mbali rufani hii baada muweka pingamizi kushindwa kutokea mbele ya kamati kuthibitisha madai yake. Hivyo maamuzi ya kamati ya uchaguzi y a TEFA yanabaki kama yalivyo. .

9. BAKILI M. MAKELE-NAFASI YA MAKAMU WA PILI WA MWENYEKITI
-Kamati imemuengua katika mchakato wa uchaguzi kwa kigezo cha elimu, kama inavyotakiwa na Ibara ya 31(1)(b) ya katiba ya TEFA . Mgombea amekiri kwamba elimu yake ni ya darasa la saba.

10. AMACK NABOLA- NAFASI YA UJUMBE SOKA LA WANAWAKE NA VIJANA
-Kamati inamuengua katika mchakato kwa kukosa sifa ya elimu ya kidato cha nne kama ibara ya 31(1)(b) ya katiba ya TEFA inavyotaka. Amack Nabola anagombea nafasi ya ujumbe wa soka la wanawake na vijana hivyo halindwi na ibara ndogo katika ibara ya 31 ambayo inatoa sifa za mgombea nafasi ya ujumbe wa kamati ya utendaji  kwa kumtaka mjumbe awe na elimu isiyo chini ya darasa la saba.  Ibara hii ipo kwa ajili ya wagombea wanaogombea nafasi za ujumbe wa kamati ya utendaji na si wajumbe wa makundi mbali mbali kama vile kundi la wanawake na vijana.

11. FIKIRI MAGOSO-NAFASI NI MJUMBE WA KAMATI YA UTENDAJI 
-Kamati inampitisha kugombea nafasi hii kwa sababu anakidhi vigezo kwa kuwa na cheti cha darasa la saba kama katiba ya TEFA anavyomtaka mgombea wa nafasi ya ujumbe wa kamati ya utendaji kuwa na elimu isiyo chini ya darasa la saba.

12. MUHIBU KANU MSHANGAMA- MAKAMU MWENYEKITI NA MJUMBE KAMATI YA UTENDAJI.
- Kamati inamuengua kwa sababu  ni kinyume cha kanuni za uchaguzi za TFF za mwaka 2013 (TFF ELECTORAL CODE) Ibara 10(9) ambayo inakataza mgombea kugombea nafasi zaidi ya moja. Muhibu Kanu Mshangama anagombea nafasi ya makamu mwenyeki wa pili na mjumbe wa kamati ya utendaji kupitia kanda tandika.

MWENYEKITI
RASHID SADALA (ADVOCATE)

TFF, VODACOM ZASAINI MKATABA MPYA


Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini Tanzania (TFF) limesaini mkataba mpya wa miaka mitatu (3) wa udhamini wa Ligi Kuu Tanzania bara (VPL) wenye thamani ya shilingi bilioni sita (tsh bilioni 6.6) na kampuni ya simu ya Vodacom, halfa hiyo imefanyika leo katika ofisi za makao makuu ya kampuni hiyo eneo la Mlimani City jijini Dar es salaam.

Akiongea wakati wa kusaini mktaba huo mpya, Mkurugenzi wa masoko wa kampuni ya simu ya Vodacom Kelvin Twissa, amesema kampuni yao inafurahia kuendelea kuwa sehemu ya udhamini ya ligi kuu nchini, mafanikio ya timu bora na kufanya vizuri katika michuano ya kimataifa inatokana na kuwa na ligi bora ambayo inadhaminiwa na Vodacom.

Naye Rais wa TFF, Jamal Malinzi amewashukuru kampuni ya Vodacom kwa kukubali kuendelea kuidhamini ligi kuu kwa kipindi kingine cha miaka mitatu (3) na kuongeza sehemuya udhamini wao kwa asilimia 40%.

Tunaishukuru kampuni ya Vodacom kwa kuendelea kuwa sehemu ya mafanikio ya mpira wa miguu nchini, udhamini wanaotupatia unavisaidia vilabu kujiandaa na kujiendesha na mikikimikiki ya ligi na kuifanya ligi kuwa na ushindani wa hali ya juu, msimu huu ligi itakua na timu 16 tunatarajia kuendelea kushuhudia uhondo huo chini ya udhamini wa kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom.

Mkataba huo mpya wa udhamini kwa kipindi cha miaka mitatu, umeboreshwa na kuwa na ongezeko la asilimia 40% kutoka katika mkataba wa awali uliomalizika.

Ligi Kuu ya Vodacom inatarajiwa kuanza kutimua vumbi Septemba 12, 2015.

TFF YAMPONGEZA JAJI MAMBI
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), Jamal Malinzi amempongeza Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Adam Mambi kwa kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu nchini.

Katika Salam zake kwa Jaji Mambi, Malinzi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta Jakaya Kikwete kwa kumteua mwanafamilia huyo wa mpira wa miguu nchini kushika wadhifa huo.

TFF kwa niaba ya familia ya mpira wa miguu na watanzania wote inamtakia kila la kheri Jaji Adam Mambi katika majukumu yake mapya ya Ujaji katika Mahakama Kuu nchini Tanzania.

TRA KUENDESHA SEMINA YA KODI
Mamlaka ya Kodi na Mapato nchini (TRA) inatarajiwa kuendesha semina ya kodi kwa viongozi wa vilabu viliyopo jijini Dar es salaam, siku ya ijumaa tarehe 14 Agosti katika hoteli ya Tiffany iliyopo eneo la Kisutu.

TRA itaendesha semina hiyo kwa vilabu vilivyopo ligi kuu, ligi daraja la kwanza na ligi daraja la pili ambapo viongozi wakuu wa vilabu hivyo, Katibu Mkuu, Mwenyekiti, na Mhasibu wanapaswa kuhudhuria semina hiyo.

Kwa kuanzia TRA itaendesha semina hiyo jijini Dar es salaa, na baadae kuendelea na semina hizo kwa vilabu vilivyopo mikoani kwa lengo la viongozi wa vilabu kutambua umuhimu wa ulipaji kodi kwa wachezaji, makocha wanaowaajiri katika vilabu vyao.

Semina hiyo itaanza saa 3 asubuhi mpaka saa 5 kamili asubuhi katika hoteli ya Tiffany iliyopo eneo la Kisutu jijini Dar es salaam, vionggozi wa vilabu vya ligi kuu, ligi daraja la kwanza, ligi daraja la pili waliopo jijini Dar es salaam mnaombwa kuhudhuria semina hiyo.

Tuesday, August 11, 2015

UAMUZI WA KAMATI YA RUFAA YA TFF


 Mwomba rufani, Dr. Devota John Marwa, (Mrufani) ni msomi mbobezi katika taaluma ya michezo, akiwa ni mhadhiri katika kitengo kinachojihusisha na taaluma ya michezo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Akiamini kwamba anakidhi vigezo vilivyowekwa kwa nafasi ya mgombea uenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu wa Wanawake(TWFA), alichukua fomu ya kuomba kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa Chama hicho.

Maombi hayo yalikumbana na pingamizi zilizoletwa na wakereketwa wawili wa soka la Wanawake, Bi. Chichi Mwidege na Bi. Mwajuma Noty, ambao kwa pamoja walimwekea pingamizi Mrufani, kwamba hakidhi matakwa ya kanuni za ugombea wa nafasi ya Mwenyekiti.

Waleta mapingamizi walidai kuwa Mrufani hakuwa na sifa zilizoainishwa katika Kanuni za Uchaguzi za T.F.F. (TFF Electoral Code) Ibara ya 9 (tisa) kipengele cha 3 (tatu), kinachomtaka mgombea awe amejihusisha na uongozi wa mpira wa miguu kwa muda usiopungua miaka mitano.

Aidha Ibara ya 28 (ishirini na nane) kipengele cha 3 (tatu), kinamtaka mgombea awe amejihusisha japo miaka 2 (miwili) katika shughuli za maendeleo ya mpira wa miguu nchini.  Kamati ya Uchaguzi iliridhia mapingamizi hayo na kuliondoa jina la Mrufani katika orodha ya wagombea wa nafasi hiyo ya Mwenyekiti. Rufani hii ni matokeo ya uamuzi huo wa Kamati ya Uchaguzi uliotolewa taraehe 22 Julai, 2015.

Kwa ujumla, sababu za kupinga maamuzi ya Kamati ya Uchaguzi zinaweza kuhesabiwa kuwa ni mbili. Moja ni iliyojikita juu ya hitilafu katika kuamua kwamba Mrufani hakuwa na uzoefu katika uongozi wa soka kwa muda ulioainishwa. Sabau nyingine ni kwamba Kamati ya Uchaguzi illibua sababu ambayo haikuwa katika Hati ya pingamizi iliyoletwa na Mleta pingamizi.

Wakati ambapo Mleta pingamizi alijikita katika kipengele cha 28(3), Kamati iliibua kipengele cha 28(8), cha Katiba ya TWFA kinachomtaka mgombea awe ametimiza uzoefu wa uongozi wa miaka mitano, ambacho hakikuwemo katika hoja za pingamizi zilizowasilishwa na mleta pingamizi.

Katika kufikia uamuzi wake, Kamati ya Rufani ilizipitia sababu za Mrufani kama zilivyoletwa, na baada ya kusikiliza maelezo ya Mrufani na hoja za Mwakilishi wa TFF, Wakili Msomi Edward Augustino, na imeamua kama ifuatavyo. Tutaanza na hoja ya mwisho.

Je, Kamati ilikuwa sahihi kuibua kipengele ambacho hakikuletwa katika hati ya mapingamizi? Kamati inaweza kuibua kipengele hicho endapo kwa kufanya hivyo, itakuwa imejielekeza katika nia njema ya maslahi ya suala linalozungumziwa.

Sharti jingine ni kwamba hoja hiyo inyoibuliwa isiwe na athari hasi(prejudicial) kwa mhusika. Kaika suala hili hata hivyo, hoja iliyoletwa na Mleta pingamizi, yaani hoja chini ya kifungu cha 28 (3), imeainisha kipindi kifupi cha uzoefu (miaka 2), na hoja iliyoibuliwa na Kamati inahitaji uzoefu wa miaka 5.

Endapo Mrufani angekuwa na uzoefu wa miaka 3 hadi 4, bado angekwama kutokana na hoja iliyoibuliwa na Kamati. Hii kwa vyovyote ingekuwa ni athari hasi (negative impact) katika harakati za Mrufani. Ni vema

Kamati zinazosikiliza malalamiko zikajikita kwenye malalamiko yaliyoletwa na wahusika wenyewe. Kama pigamizi lingekuwa liko juu ya kipengele hicho tu, tusingesita kukubaliana na sehemu hii ya rufani. Hata hivyo, takwa la uzoefu wa miaka 5 limeainishwa pia katika Ibara ya 9 (3), ambayo ilikuwa ni sehemu ya mapingamizi yaliyokuwepo kwenye hati ya mapingamizi.

Kwa sababu hiyo, Kamati ya Rufani haioni kama hoja hiyo ina mashiko. Haitaitilia maanani. Hoja kuu ndani ya rufaa hii ni je, Kamati ya Uchaguzi ilijielekeza vema kuhusu suala la uzoefu wa uongozi ulioainishwa na Katiba?

Mrufani ameieleza Kamati ya Rufani mlolongo wa shughuli ambazo amekuwa akizifanya, nyingi zikiwa zimejikita zaidi katika taaluma. Miongoni mwa shughuli hizo ni kuandaa Mpango Mkakati wa kuendeleza soka la wanawake. Mpango huu uliridhiwa na kuwasilishwa Makao Makuu ya Shirikisho la Mpira Duniani, yaani FIFA.

Maelezo mengine ni kushiriki katika kuongoza timu mbali mbali kule Chuo Kikuu, zingine zikiwa za watoto wadogo ambao baadhi ya matunda yake ni wachezaji walioibukia kwake kama vile Simon Msuva. Alisema zaidi kuwa alishiriki kuandaa warsha ilizoandaliwa kwa ushirikiano kati ya FIFA na TFF.

Aidha. Alisema kuwa amekuwa kiongozi tangu akiwa bado kwenye vyuo vya ualimu, na baadaye alipohitimu na kufanya kazi kama Mwalimu, kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliko mpaka sasa. Akasema, hata alipokuwa Sweden kwa masomo ya juu pia lijihusisha na programu za maendeleo ya soka la wanawake.

Wakili msomi wa TFF akijibu hoja hizo, alikubaliana na uamuzi wa Kamati ya Uchaguzi kuwa Mrufani hajaonesha popote kwamba amewahi kuongoza soka, akasema Mrufani ni mtaalamu tu kama msomi, jambo linaloweza kufanywa na msomi yoyote. Akamalizia kwa kuiomba Kamati ya Rufani za Uchaguzi kuitupilia mbali rufaa ya Mrufani kwa kukosa mashiko.

Tofauti na Kamati ya Uchaguzi, Kamati ya Rufani imeona kuwa kwa maslahi mapana ya mchezo wa soka katika ujumla wake, ni vema kuweka tafsiri pana (wide interpretation) juu ya sifa zinazozungumzwa, badala ya kuweka tafsiri finyu (restricted/narrow interpretation) kama ilivyofanya Kamati ya Uchaguzi.

Baada ya kufanya hivyo, kuhusiana na Mrufani, Kamati imeona kuwa ana sifa zinazostahili. Kupitia sababu alizozitoa, na vielelezo vyake, Kamati ya Rufani haina wasiwasi kuwa Mrufani ana uzoefu mbali mbali sio katika soka tu, bali pamoja na michezo katika ujumla wake.

Tumeshuhudia katika maelezo yake kwetu kwamba ushiriki wake katika hatua mbali mbali, japo hakuwahi kuchaguliwa, sio ushiriki wa kitaaluma tu, kama msomi mwingine yeyote. Ni ushiriki wenye dhamira ya dhati ya kuleta mabadiliko/maendeleo katika soka la wanawake.

Maelezo yake kuwa aliaandaa programu ya maendeleo ya soka la wanawake, hayakupingwa. Kamati ya Uchaguzi ingeangalia namna ambavyo “visheni” iliyomo katika programu ile ambavyo ingeweza kutekelezwa na mtu aliyeaiandaa. Kwa hiyo, katika hoja hii, Kamati inakubaliana kuwa Mrufani anazo sifa stahiki, na kukatwa kwa sababu hii, Kamati ya Uchaguzi haikujielekeza vema. Kwa hiyo, Mrufani ameshinda rufaa yake? Kamati ya Rufani inachelea kujibu swali hili moja kwa moja. Utaratibu wa kuwasilisha rufani ulikiukwa, na hapa ndipo rufaa hii inapokwaa kisiki.  Chini ya Ibara ya 13 (1) cha Kanuni ya

Uchaguzi (Electoral Code), mgombea ambaye hakuridhika na maamuzi, atawasilisha rufaa yake ndani ya siku 3 (tatu) tangu uamuzi anaoupinga ulipotolewa.

Kipengele cha 3 (tatu) cha ibara hiyo kinasema kwamba Mrufani yoyote atakuwa na uhalali endapo rufaa yake imewasilishwa kwa mujibu wa kanuni hizo.  Uamuzi unaolalamikiwa ulitolewa tarehe 22 Julai 2015, sababu za rufaa ziliandaliwa tarehe 27 Julai na sababu hizo za rufaa zililipiwa tarehe 28 Julai, 2015. Ni dhahiri kwamba rufaa ililetwa nje ya muda uliowekwa na kanuni, na kwa hiyo inakosa uhalali kisheria na kikanuni.

Japo katika mwenedo na maamuzi yake Kamati ya Rufani za Uchaguzi haifungwi na taratibu za kimahakama, suala la muda wa kuwasilisha rufani sio miongoni mwa mambo ambayo Kamati inaweza kutoyazingatia. Kwa sababu hiyo, Rufaa hii imetupwa, lakini kwa sababu tofauti na zile za Kamati ya Uchaguzi.

Pamoja na uamuzi huu, Kamati ya Rufani za Uchaguzi inapenda kwa namna ya kipekee kumpongeza Mrufani kwa jitihada alizozionesha kutaka kuitumikia TWFA. Ni matumaini ya Kamati kuwa hatokata tama, na kwamba atakuwa tayari, akitakiwa kufanya hivyo, kupitia taalum yake, kushirikiana na wenzake katika jitihada za kuendeleza soka la akina mama lililo na changamoto lukuki.

Imetolewa na,
JULIUS M. LUGAZIYA
Mwenyekiti-Kamati ya Rufani za Uchaguzi

DIRISHA LA USAJILI LASOGEZWA


Dirisha la usajili limeongezwa toka tarehe 06 Agosti hadi tarehe 20 Septemba, baada ya muda huo klabu itakayochelewesha kuleta usajili wake itatozwa kiasi cha shilingi laki tano (Tsh 500,000) kwa kila mchezaji itakayemsajili mpaka siku ya tarehe 30 Agosti.

Mwisho wa kufanya uhamisho wa kimataifa wa wachezaji kwa njia ya mtandao TMS ni tarehe 6 Septemba.

Kikao cha kamati ya sheria kitakaa tarehe 28 kwa ajili ya kuupitisha usajili na kitakaa tena tarehe 8/9/2015 kwa ajili ya kupitisha usajili.

Kuanzia tarehe 21 hadi 27 itakuwa ni wiki ya pingamizi, ambapo majina yatabandikwa TFF Karume na kuwekwa kwenye mtandao ili kuwezesha vilabu vyenye pingamizi kuwawekea wachezaji mapingamizi.

Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inatarajiwa kuanza tarehe 12 Septemba 2015, Daraja la kwanza (FDL) ikitarajiwa kuanza Septemba 17 na Ligi Daraja la pili inatarajiwa kuanza Oktoba 16 mwaka huu.

MICHUANO YA COPA COCA-COLA 2015
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) bado linaendelea na mazungumzo na wadhamini wa michuano hiyo (Coca-Cola). Kutokana na mazungumzo hayo, ratiba ya michuano hiyo itachelewa kutoka.

Hivyo, tunawaomba kuwa na uvumilivu wakati mchakato wa mazungumzo hayo yanayokaribia ukingoni ukiendelea.

TWIGA STARS KUIVAA HARAMBEE STARLETS


Timu ya Taifa ya  Tanzania ya Wanawake (Twiga Stars) iliyopo kambini kisiwani Zanzibar, inatarajiwa kucheza mchezo wa kirafiki na timu ya taifa ya Wanawake kutoka Kenya (Harambee Starlets) Agosti 23, 2015.

Mchezo huo wa kirafiki utachezwa katika uwanja wa Aman Kisiwani Zanzibar, ikiwa ni sehmu ya maandalizi ya kikosi hicho kujiandaa na fainali za Michezo ya Afrika (All Africa Games) zitakazofayika nchini Congo-Brazzavile kuanzia Septemba 4 – 19, 2015.

Twiga Stars inaendelea na mazoezi kutwa mara mbili katika viwanja vya Aman na Fuoni chini ya kocha wake mkuu Rogasian Kaijage kujiandaa na fainali hizo za michezo ya afrika, wachezaji wote waliopo kambini wapo katika hali nzuri wakiendelea kujifua na michezo ya Afrika.

TAIFA STARS YAANZA MAZOEZI



Kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) kimeanza mazoezi katika uwanja wa Karume kujiandaa na mchezo dhidi ya Nigeria kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika mwaka 2017 nchini Gabon.

Wachezaji wa Taifa Stars chini ya kocha wake mkuu Charles Mkwasa watakua wakijifua mara mbili kwa siku asubuhi na jioni katika uwanja wa Karume katika kujiweka fit na maandalizi ya mchezo huo.

Kufuatia baadhi ya wachezaji kuwa na majukumu na timu zao kujiandaa na mchezo wa Ngao ya Hisani utakaochezwa Agosti 22, Mkwasa amewaongeza wachezji wengine kumi (10) kutoka katika orodha yake ya akiba.

Lengo la kambi hii ya awali ya siku tano, ni kocha mkuu pamoja na benchi lake la ufundi kupata nafasi ya kuwaona wachezaji katika mazoezi hayo kabla ya safari ya kuelekea nchini Uturuki Agosti 23 mwaka huu kwa kambi ya siku kumi.

Wachezaji walioitwa na kuanza mazoezi leo ni Said Mohamed, Vicent Andrew (Mtibwa Sugar), Mohamed Hussein, Ibrajim Hajibu (Simba SC), Hamis Ali, Juma Mbwana (KMKM), Tumba Sued (Coastal Unioni), Samuel Kamuntu (JKT Ruvu), Ibrahim Hilka (Zimamoto– Zanzibar) na Mohamed Yusuf (Prisons).

Wachezaji wengine waliopo kambini ni Said Ndemla, Hassan Isihaka, Abdi Banda(Simba SC), Rashid Mandawa (Mwadui FC), Michael Aidan (Ruvu Shooting), Orgeness Mollel (Aspire Academy) na Abdulhaman Mbambi (Mafunzo).

Monday, August 10, 2015

WATANZANIA SABA WAULA KAMATI ZA CAF


Kikao cha Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la mpira barani Afrika (CAF ) kilichokutana mwishoni mwa wiki jijini Cairo nchini Misri, kimewateua watanzania saba kuwa wajumbe wa kamati zake mbali mbali kwa kwa kipindi cha miaka miwili 2015-2017.

Walioteuliwa pamoja na kamati zao katika mabano ni:

1. Leodeger Tenga- (Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Makamu Mwenyekiti Kamati ya Fedha, Mjumbe wa Kamati ya Uendeshaji Mashindano ya fainali za Mataifa Afrika kwa Wachezaji wa ndani (CHAN), Mwenyekiti wa Kamati ya Mpira wa Wanawake na Mjumbe wa Kamati ya Ushauri na Vyama Wanachama).
2. Jamal Malinzi - (Mjumbe kamati ya Uendeshaji Mashindano ya Vijana Umri chini ya miaka 20)
3. Mwesigwa Selestine - (Mjumbe Kamati ya Uendeshaji Mashindano ya Vijana Umri chini ya Miaka 17).
4. Richard Sinamtwa -(Mjumbe Kamati ya Rufaa)
5.Dr Paul Marealle -(Mjumbe Kamati ya Tiba)
6. Lina Kessy -(Mjumbe ya Soka la Wanawake)
7. Crescentius Magori-(Mjumbe Kamati ya Soka la Ufukweni na Soka la Ndani)

Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania - TFF linawapongeza wajumbe wote walioteuliwa kuingia katika kamati mbali mbali na linawatakia kila la kheri wanapoiwakilisha nchi yetu.

KIHANGA MWENYEKITI FA MOROGORO


Chama cha Mpira wa Miguu mkoa wa Morogoro (MRFA) jana kilifanya uchaguzi wa viongozi wake katika nafasi ya mwenyekiti, makamu mwenyekiti, katibu, mweka hazina, mjumbe wa mkutano mkuu pamoja na wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

Katika uchaguzi huo Paschal Kihanga aliibuka na ushindi katika nafasi ya mwenyekiti, huku Gracian Max Makota  akishinda nafasi ya makamu mwneyekiti, nafasi ya katibu mkuu imechukuliwa na Charles Mwakambaya na katibu msaidizi Jimmy Lengme.

Nafasi ya Mweka Hazina imechukuliwa na Peter Mshigati, Mjumbe wa mkutano mkuu ni Hassan Mamba na mwakilishi wa vilabu ni Ramadhani Wagala, Kamati ya utendaji wamechaguliwa Mrisho Javu, Rajabu Kiwanga na Boniface Kiwale.

TFF inawapongeza viongozi wapya waliochaguliwa kuongoza chama cha soka mkoa wa Morogoro (MRFA) na kuahidi kuendelea kushirikiana nao katika kazi za kila siku za maendeleo ya mpira wa miguu nchini.

TOTO AFRICAN KUCHAGUANA OKTOBA 2015
Klabu ya Toto African ya Mwanza inatarajiwa kufanya uchaguzi wa kujaza nafasi zilizo wazi katika kamati yake ya utendaji ifikapo tarehe 11 Oktoba 2015. Katika barua yake kwa Katibu Mkuu wa Toto African, Katibu Mkuu wa TFF ameuagiza uongozi wa Toto African kuwasiliana na Kamati yao ya Uchaguzi ili tangazo la uchaguzi litolewe si chini ya siku sitini (60) kabla ya tarehe ya kufanyika uchaguzi.

Kwa muda mrefu kumekuwa na mvutano katika klabu ya Toto na suala kubwa likiwa ni kuhusu ujazaji wa nafasi zilizo wazi. Awali TFF ilipokea maombi ya wanachama na wadau wa Toto African wakitaka ufanyike uchaguzi ili kumaliza mvutano ndani ya klabu.

TFF ilishauri uchaguzi huo kusubiri klabu kukamilisha mchakato wa usajili.

Vilevile TFF imewataka wadau wote wa klabu hiyo kongwe ya mjini Mwanza kuheshimu uongozi uliopo madarakani kwani ndio unaotambulika na ndio utaendelea kuiongoza Toto African katika kipindi cha kuelekea uchaguzi uchaguzi.

TFF YATUMA SALAM ZA RAMBIRAMBI MALAWI
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), Jamal Malinzi ametuma salam za rambi rambi kwa Rais wa Chama cha Soka nchini Malawi (FAM), Walter Nyamilandu kufutia kifo cha aliyekua Rais wa chama hicho John Zingale.

John Zangale alifariki dunia baada ya kuugua kwa muda mfupi wiki iliyopita katika hospitali ya  Mlambe iliyopo Blantyre nchini Malawi na kuzikwa mwishoni mwa wiki alikuwa Rais wa FAM mwaka 1998- 2002.

 Katika salam zake kwenda kwa Rais wa FAM, Malinzi amewapa pole familia ya marehemu pamoja na chama cha soka nchini Malawi kwa msiba huo, na kusema TFF kwa niaba ya Watanzania iko pamoja nao katika kipindi hicho cha maombelezo.


TWIGA STARS YAELEKEA ZANZIBAR


Kikosi cha timu ya Timu ya Taifa ya Wanawake (Twiga Stars) kimeodoka leo saa 6 mchana jijini Dar es salaam kuelekea kisiwani Zanzibari, ambapo kitaweka kambi ya mwezi mmoja kujiandaa na fainali za Michezo ya Afrika (All Africa Games) mwezi Septemba.

Msafara wa Twiga Stars umeondoka na boti ya Azam (Kilimanjaro) ukiwa na watu 32, wakiwemo wachezaji 25, benchi la ufundi 6 pamoja na kiongozi wa msafara, ambapo TFF imegharamia kambi hiyo ya mwezi mmoja

Wachezaji waliosafiri leo ni Fatuma Omari, Belina Julius, Happiness Hezron, Fatuma Hassan, Anastazia Anthony, Fatuma Bashiru, Fatuma Issa, Fatuma Khatibu, Maimuna Hamis, Donizia Daniel, Sofia Mwasikili, Etoe Mlenzi.

Wenigine ni Amina Ally, Thereza Yonna, Mwanahamisi Omari, Stumai Abdallah, Shelder Boniface, Asha Rashid, Najiat Abbas, Estha Chabruma, Mwajuma Abdallah na Fatuma Mustapah.

Twiga Stars itakua kambini kisiwani Zanzibar kwa kipindi cha mwezi mmoja, kujiandaa na fainali hizo za michezo ya afrika, ambapo imepangwa kundi A pamoja na wenyeji Congo – Brazzavile, Ivory Coast na Nigeria.

Fainali za Michezo ya Afrika  (All Africa Games) zinatarajiwa kuanza kutivua vumbi Septemba 4 – 19 nchini Congo-Brazzavile.

DIRISHA LA USAJILI SASA KUFUNGWA AGOSTI 20


Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) limesogezwa mbele kufungwa kwa dirisha la usajili wa wachezaji kwa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Ligi Daraja la Kwanza (FDL) na Ligi Daraja la Pili (SDL) mpaka Agosti 20 mwaka huu.

Awali dirisha la usajili lilikua lifungwe leo Agosti 6, na usajili mdogo wa ndani ungefungwa Septemba 5, 2015 lakini sasa usajili wote kwa jumla utafungwa Agosti 20, 2015.

Tarehe 21- 28 Agosti, 2015 ni kipindi cha pingamizi, tarehe 29-30 Agosti 2015, Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji itapitia na kupitisha usajili.

Dirisha la uhamisho wa wachezaji wa Kiamataifa (FIFA –TMS) litafungwa tarehe 06 Septemba, 2015 na Ligi Kuu ya Vodacom inatarajiwa kuanza kutimua vumbi Septemba 12, 2015.

TFF inavitaka vilabu kukamilisha usajili huo katika muda huo uliowekwa, ili kupunguza usumbufu wa kufanya usajili dakika za mwisho,na dirisha litakapofungwa Agosti 20, litafunguliwa tena wakati wa dirisha dogo mwezi Novemba 15 mwaka huu.

MKWASA ATANGAZA 29 WA TAIFA STARS



Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), Charles Boniface Mkwasa leo
ametangaza kikosi cha wachezaji 29 watakaongia kambini siku ya Jumapili tarehe 9,
Agosti katika hoteli ya Tansoma iliyopoe eneo la Gerezani kwa ajili ya kambi ya wiki moja ya
mazoezi.

Katika kikosi hicho alichokitangaza cha wachezaji 29, Mkwasa amewajumuisha wachezaji
watano wanaocheza soka la kulipwa nje ya nchi (Proffesional), ambao baadae
watajumuika kwa kambi ya kujiandaa kucheza na Nigeria mwezi Septemba 2015 nchini
Uturuki.

Taifa Stars inatarajiwa kuweka kambi ya siku kumi jijini Istambul - Uturuki, ambapo
itacheza michezo miwili ya kirafiki na timu za Taifa za Libya na Kuwait kabla ya kurejea
nchini kuwavaa Nigeria.

Wachezaji watakaongia kambini jumapili ni magolikipa, Ally Mustafa (Yanga SC) na Aishi
Manula (Azam FC), walinzi wa pembeni: Shomari Kapombe (Azam FC), Michael Aidan
(Ruvu Shooting), Juma Abdul, Mwinyi Haji (Yanga SC) na Abdi Banda (Simba SC).

Walinzi wa kati; Hassan Isihaka (Simba SC), Nadir Haroub, Kelvin Yondani (Yanga SC),

Viungo wakabaji: Himid Mao, Frank Domayo, Mudathir Yahya (Azam FC), Viungo
washambuliaji ni Salum Telela (Yanga SC) na Said Ndemla (Simba SC).

Washambuliaji wa pembeni; Orgenes Mollel (Aspire – Senegal), Abdrahman Mbambi
(Mafunzo), Deus Kaseke, Saimon Msuva (Yanga SC), Ramdhani Singano, Farid Musa
(Azam FC), huku washambuliaji wa kati wakiwa ni John Bocco, Ame Ally (Azam FC) na
Rashid Mandawa (Mwadui FC).

Wachezaji wa kimataifa waliojumuishwa katika kikosi hicho ambacho Agosti 23 kitaelekea
kambini nchini Uturuki kwa kambi ya siku kumi ni Mbwana Samata, Thomas Ulimwengu (TP
Mazembe – DR Congo), Mrisho Ngasa (Free State - Afrika Kusini) na Hassan Sembi
(Santos FC – Afrika Kusini) na Adi Yussuf (Mansfield Town – Uingereza)

Wednesday, August 5, 2015

TWIGA STARS KUWEKA KAMBI ZANZIBAR KESHO



Timu ya Taifa ya Tanzania ya Wanawake (Twiga Stars) inatarajiwa kuingia kambini kesho kisiwani Zanzibar kujiandaa na Fainali za Michezo ya Afrika (All Africa Games) zitakazofayika mwezi Septemba mwaka huu nchini Congo Brazzavile.

Kikosi hicho cha wachezaji 25 chini ya Kocha Mkuu Rogasian Kaijage, tayari kimeanza mazoezi kujiandaa na michuano hiyo ambapo Tanzania ilikata tiketi ya kushiriki fainali hizo baada ya kuiondoa Zambia kwa jumla ya mabao 6-5.

Twiga Stars inaingia kambini  kwa gharama za TFF, huku jitihada za TFF kuwasiliana na Kamati ya Olimpiki nchini (TOC) zikiendelea kuona ni jinsi gani kamati hiyo inaihudumia timu hiyo ya Taifa kwa ajili ya maandalizi ya michuano hiyo ya Michezo Afrika.

TFF inatambua TOC ndio wana jukumu la kuhudumia timu za Taifa kuelekea kwenye michuano hiyo ya Michezo ya Afrika ikiwemo Twiga Stars.

Twiga Stars ambayo imefuzu kwa Fainali za Michezo ya Afrika itakayoanza kutimua vumbi Septemba 04 – 17 imepangwa kundi A na wenyeji Congo Brazaville na Nigeria pamoja na Ivory Coast.

DIRISHA LA USAJILI KUFUNGWA KESHO



Dirisha la Usajili kwa wachezaji wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Ligi Daraja la kwanza (FDL), na Ligi Daraja la Pili (SDL) linatarajiwa kufungwa kesho Alhamis saa sita usiku.

Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), linavikumbusha vilabu vyote vinavyoshirki msimu mpya wa 2015/2015 kuhakikisha vinakamilisha usajili wa wachezaji wao kabla ya dirisha la usajili kufungwa kesho.

Kipindi cha dirisha la usajili kwa timu za Ligi Kuu, Daraja la Kwanza na Ligi Daraja la Pili kilifunguliwa Juni 15, 2015 na kitamalizika kesho kwa awamu ya kwanza ya usajili.


Tuesday, August 4, 2015

MALINZI AMSHUKURU TENGA

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), Jamal Malinzi amemshukuru Rais wa CECAFA, Leodgar Tenga kwa kuipa Tanzania uenyeji wa mashindano ya Vilabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kagame Cup) iliyomalizika jana kwa klabu ya Azam FC kutawazwa Mabingwa wapya wa michuano hiyo.

 Aidha Malinzi ameishukuru Kamati ya Ndani ya Uendeshaji ya Michuano hiyo (LOC) kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kuandaa na kuhakikisha michuano hiyo inafanyika na kumalizika katika hali ya usalama na amani.

Malinzi pia amewapongeza wapenzi, washabiki na wadau wa soka nchini waliojitokeza kushuhudia michezo ya michuano hiyo na kuonyesha nidhamu ya hali ya juu ndani nan je ya uwanja kipindi chote cha michuano.

Rais Malinzi ameipongeza klabu ya Azam FC kwa kutwaa Ubingwa Kagame, kwa kutwaa ubingwa huo imeweza kuweka historia ya kutwaa Ubingwa huo kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwake na pia kuwa klabu iliyocheza michuano hiyo na kuwa Bingwa bila kuruhusu nyavu zake kutikisika.

Pia Malinzi amewashukuru waandishi wa habari/vyombo vya habari kwa sapoti yao wakati wa michuano hiyo. Shukrani hizo pia zimepelekwa kwa klabu za Yanga SC, KMKM kwa kushiriki mashindano hayo.

U-15 YAREJEA KUTOKA ZANZIBAR
Kikosi cha timu ya Taifa ya Vijana wenye umri chini ya miaka 15 (U-15), kimerejea leo asubuhi kutokea kisiwani Zanzibar kilipokwenda kucheza michezo ya kujipima nguvu na kombani ya U-15 ya kisiwani humo.

Katika michezo miwili iliyocheza kisiwani humo, iliweza kushinda michezo yote miwili, (4-0 ), (1-0), huku kocha Bakari Shime akiwapongeza vijana wake na kusema wanaendelea kuimarika kuelekea kujiandaa  na kuwania kufuzu kwa fianali za Mataifa Afrika chini ya miaka 17 mwakani.

Baada ya kurejea jijini Dar es salaam leo, kambi ya timu hiyo imevunjwa na vijana hao watakutana tena mwisho wa mwezi wa Agosti kama ilivyo katika program yao ya kukutana kila mwisho wa mwezi na kucheza michezo ya kirafiki.

Mwishoni mwa mwezi Agosti timu hiyo ya vijana inatarajiwa kuelekea mkoani Tanga kucheza michezo ya kirafiki na kombani ya mkoani humo, ambapo kocha wake Shime pia anatumia nafasi hiyo kutazama wachezaji wengine wenye uwezo mzuri katika timu za kombaini za mikoa kwa ajli ya kuwaongeza katika kikosi chake.

Mpaka sasa timu hiyo ya vijana chini ya miaka 15 (U15) imeshafanya ziara na kucheza michezo katika miji ya Mbeya na kisiwani Zanzibar.

Monday, August 3, 2015

AZAM BINGWA KOMBE LA KAGAME


MABAO mawili yaliyofungwa na John Bocco na Kipre Tchetche, moja katika kila kipindi, jana yaliiwezesha Azam kuandika historia mpya katika soka ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati baada ya kuizabua Gor Mahia ya Kenya mabao 2-0 na kutwaa ubingwa wa Kombe la Kagame.

Azam imekuwa timu ya tatu kutoka Tanzania Bara kushinda kombe hilo baada ya Simba na Yanga. Simba inaongoza kwa kulitwaa mara tano ikifuatiwa na Yanga iliyolitwaa mara nne.

Ushindi huo umeiwezesha Azam kutwaa kitita cha Dola za Marekani 30,000 wakati Gor Mahia imezawadiwa Dola 20,000 kwa kushika nafasi ya pili. KCCA ya Uganda imetwaa kitita cha Dola 10,000 kwa kushika nafasi ya tatu.

Fedha hizo zimetolewa na Rais Paul Kagame wa Rwanda, ambaye ni mdhamini mkuu wa mashindano hayo. Rais Kagame hutoa Dola 60,000 kila mwaka kwa ajili ya zawadi za washindi watatu wa kwanza,

Iliwachukua Azam dakika 16 kuhesabu bao la kwanza lililofungwa na Bocco na kudumu hadi mapumziko. Bao la pili lilifungwa na Tchetche dakika ya 63.

Azam ilitinga fainali ya michuano hiyo baada ya kuichapa KCCA bao 1-0 wakati Gor Mahia iliilaza Al Khartoum ya Sudan mabao 2-1.

Sunday, August 2, 2015

TAARIFA YA KAMATI YA UTENDAJI TFF


Kikao cha Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) kilichokutana leo kimepitia na kutoa maamuzi yafuatayo:

(i)           Kila mkoa utakua na kituo cha kukuza na kuendeleza vipaji vya watoto (Regional Sports Centre). Mapato ya mchezo wa Ngao ya Hisani msimu huu yatatumika kuagiza kontena la vifaa (mipira size 3, 4, bips na cones) ambavyo vitasambazwa katika vituo vyote vya michezo vya mikoa.

(ii)         Ubovu wa viwanja – Kamati ya Utendaji imeiagiza sekretariat kuwaandikia barua wamiliki wa viwanja vyenye mapungufu, kufanyia kazi marekebisho hayo haraka kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa ligi nchini. Kiwanja ambacho hakitafanyiwa marekebisho hakitatumika kwa michezo ya ligi msimu huu.

(iii)       Twiga Stars – Timu ya Taifa ya Wanawake ya mpira wa miguu nchini Tanzania (Twiga Stars) inatarajiwa kuingia kambini tarehe 04 Agosti kisiwani Zanzibar kwa gharama za TFF kujiandaa na Fainali za Michezo ya Afrika (All Africa Games) zitakazofanyika nchini Congo Brazaville mwezi Septemba mwaka huu. Aidha Kamati ya Utendaji imeiagiza sekretariet kuwasiliana na Kamati ya Olympic nchini (TOC) kuweza kujua mchango wao katika maandilizi hayo ya michezo ya Afrika.

(iv)        Kamati ya Utendaji imeipongeza Kamati ya ndani ya Uendeshaji wa Michuano ya Kombe la Kagame (LOC) kwa kuandaa michuano hiyo vizuri kuanzia mwanzo mpaka sasa inapoelekea mwishoni kesho kwa mchezo wa Fainali.  Aidha Kamati inaipongeza klabu ya Azam FC kwa kufika hatua ya fainali ya michuano hiyo na kuitakia kila la kheri katika mchezo wa kesho ili iweze kulibakisha kombe hilo nyumbani. Kamati hiyo pia imeipongeza klabu ya Yanga kwa kufika hatua ya robo fainali ya michuano hiyo.

(v)          Aidha Kamati ya utendaji imeiagiza sekretariat kuandika barua kwenda kwa uongozi wa CECAFA juu ya masikitiko na mapungufu yaliyoenekana katika michuano hiyo. Timu ya Gor Mahia pamoja na washabiki wake wamekuwa wakifanya vitendo vya utovu wa nidhamu huku CECAFA ikiwatazama pasipo kuwapa adhabu yoyote.

(vi)        Kikao hicho cha Kamati ya Utendaji pia kimepitia na kupitisha mapendekezo ya rasimu ya kanuni za uendeshaji wa Bodi ya ligi nchini (TPLB), yaliyowasilishwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria, Katiba na Hadhi za Wachezaji Wakili, Idd Mandi.

DIRISHA LA USAJILI KUFUNGWA AGOSTI 6
Dirisha la Usajili kwa Vilabu vya Ligi Kuu (VPL), Ligi Daraja la Kwanza (FDL) na Ligi Daraja la Pili (RCL) linatarajiwa kufungwa tarehe 06 Agosti, 2015.

Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) linavikumbusha vilabu vyote kufanya usajili wa wachezaji wao mapema kabla ya kufungwa kwa dirisha hilo, ili kuondokana na usumbufu wa kufanya usajili dakika za mwisho.

Pindi dirisha hilo litakapofungwa Agosti 06, hakuna klabu au timu yoyote itakayoweza kufanya tena usajili wake, hivyo ni vyema vilabu vitahakikisha vinamaliza mausala ya usajili mapema kabla ya siku ya mwisho.

U15 KUJIPIMA LEO ZANZIBAR
Kikosi cha timu ya Taifa cha vijana wenye umri chini ya miaka 15 (U-15) leo kinatarajiwa kushuka dimbani kisiwani Zanzibar kucheza michezo wa kirafiki na kombani ya kisiwani humo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika mwaka 2017.

Timu ya vijana ya Taifa wenye umri chini ya miaka 15 (U15) imekua ikiingia kambini kila mwisho wa mwezi kwa ajili ya kucheza michezo ya kirafiki ya kujipima nguvu, na kocha kupata nafasi ya kuona maendeleo ya vijana na kuongeza wachezaji wengine wanaonekana katika kuboresha kikosi hicho.

Kikosi hicho cha Vijana cha U-15 kilichopo chini ya kocha mzawa Bakari Shime, kinajumuisha wachezaji 22 waliopo kambini, na kinatarajiwa kucheza michezo miwili kisiwani Zanzibari leo jumamosi na jumapili, kabla ya kurejea jijini Dar es salaam.